2014-06-03 07:17:39

Kanisa linawahitaji mashahidi wa Injili


Baba Mtakatifu Francisko, Jumapili tarehe 1 Juni 2014 ameshiriki katika kongamano la kimataifa la Chama cha Uamsho wa Kikatoliki kwenye Uwanja wa Michezo wa Olympic ulioko mjini Roma. Amesikiliza shuhuda za watu mbali mbali na kuombwa kutoa ushauri. Kwa Mapadre amewataka kuwa karibu zaidi na Yesu Kristo kwa njia ya Sala, Tafakari ya Neno la Mungu na Ibada ya Kuabudu Ekaristi Takatifu. Wawe karibu na Familia ya Mungu wanayoihudumia kwa njia ya upendo kamili.

Baba Mtakatifu anawataka vijana kutoka kifua mbele kutangaza Injili ya Furaha na kamwe ujana wao wasiufungie kwenye makabati, kwani utachakaa kama soli ya kiatu na kukosa uzuri na matumaini. Ujana unapendeza kwa kushirikishana na wengine ile furaha ya kukutana na Yesu Kristo pamoja na kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake!

Baba Mtakatifu amewakumbusha wanafamilia kwamba, wao ni Kanisa dogo la nyumbani, mahali ambapo palitoa fursa kwa Yesu kukua, akaongezeka nguvu, akajaa hekima na neema ya Mungu ilikuwa juu yake. Wanandoa wapende kukuza na kudumisha upendo kati yao kwa kutambua kwamba, Shetani yupo na hapendi kuziona familia zikistawi na kushamiri. Pamoja na udhaifu wao wa kibinadamu, wanandoa waendelee kuwa thabiti katika imani kwa kuwarithisha watoto wao imani kutoka kwa Kristo na Kanisa lake. Baba Mtakatifu anaziombea Familia katika shida na magumu, changamoto na fursa mbali mbali ziweze kudumu na kusonga mbele kwa ari na moyo mkuu zaidi.

Baba Mtakatifu anasema wagonjwa na walemavu ni sehemu muhimu sana ya Kanisa, kwani wao kwa namna ya pekee, wanaonja Fumbo la Mateso ya Kristo, changamoto ya kushuhudia imani na matumaini hata katika mahangaiko yao ya ndani. Wazee nao wana nafasi kubwa katika kurithisha imani kwa vijana wa kizazi kipya. Wazee waheshimiwe na kuthaminiwa katika maisha na utume wa Kanisa, kwani ni kisima cha hekima na furaha ya kweli.

Mwishoni, Baba Mtakatifu, amewaombea waamini waliokuwa wamekusanayika kwenye Uwanja wa Michezo wa Olympic, huku wakiendelea kumsubiri Roho Mtakatifu, ili wajazwe nguvu ya Roho Mtakatifu na kuwapatia zawadi ya kunena kwa lugha ya upendo na huduma kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Roho Mtakatifu awawezeshe kujenga na kudumisha umoja, upendo na mshikamano wa dhati badala ya kuwa na uchu wa madaraka; awasaidie kuwa wanyenyekevu na kulipenda Kanisa pamoja na kuwa na moyo wazi ili kupokea mapaji ya Roho Mtakatifu.








All the contents on this site are copyrighted ©.