2014-06-03 09:03:57

Kanisa linaomboleza kifo cha Kardinali Lourdusamy


Kardinali Simon Duraisamy Lourdusamy, Mwenyekiti mstaafu wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makanisa ya Mashariki aliyefariki duniani tarehe 2 Juni 2014 anatarajiwa kuzikwa Alhamisi tarehe 5 Juni 2014 katika Ibada ya mazishi itakayoongozwa na Kardinali Angelo Sodano, Dekano wa Makardinali na baadaye, Baba Mtakatifu Francisko atahitimisha kwa Ibada ya Maziko.

Baba Mtakatifu Francisko amemtumia salam za rambi rambi Askofu mkuu Anthony Anandarayar wa Jimbo kuu la Pondicherry na Cuddalore kufuatia kifo cha Kardinali Lourdusamy na kuwahakikishia wote walioguswa na msiba huu uwepo wake wa karibu kwa njia ya sala na sadaka yake.

Baba Mtakatifu anamshukuru Mwenyezi Mungu kwa maisha na utume wa Kardinali Lourdusamy, aliyejitosa kimasomaso kwa ajili ya kutangaza Injili kwanza kabisa nchini India na baadaye kwa Kanisa la Kiulimwengu akitekeleza dhamana mbali mbali hadi pale alipoteuliwa kuwa ni Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makanisa ya Mashariki kuanzia mwaka 1993 hadi mwaka 1999. Anamwombea huruma kutoka kwa Mwenyezi Mungu ili aweze kumkirimia amani na furaha ya mbinguni. Baba Mtakatifu anatoa baraka zake za kitume kwa wote wanaoomboleza msiba huu mkubwa.

Marehemu Kardinali Lourdusamy alizaliwa kunako tarehe 5 Februari 1924 huko Kalleri, India. Baada ya masomo na majiundo yake ya Kikasisi, akapadrishwa tarehe 21 Novembe 1951. Tarehe 2 Julai 1962 akateuliwa kuwa ni Askofu msaidizi wa Jimbo Katoliki la Bangalore na kuwekwa wakfu kama Askofu tarehe 22 Agosti 1962. Tarehe 9 Novemba 1964 akateuliwa kuwa Askofu mwandamizi wa Jimbo kuu la Bangalore na kusimikwa hapo tarehe 11 Januari 1968.

Tarehe 2 Machi 1970 atateuliwa kuwa ni Katibu mwambata wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa Watu. Tarehe 26 Februari 1973 akateuliwa kuwa Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa Watu na Rais wa Mashirika ya Kimissionari ya Kipapa sanjari na kuwa ni Mkuu wa Chuo Kikuu cha Kipapa cha Urbaniana.

Mtakatifu Yohane Paulo II akamteuwa kuwa Kardinali tarehe 25 Mei 1985. Akateuliwa kuwa Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makanisa ya Mashariki tarehe 30 Oktoba 1985 hadi tarehe 24 Mei 1991 alipong'atuka kutoka madarakani.







All the contents on this site are copyrighted ©.