2014-06-02 08:44:06

Mwanga una nguvu zaidi kuliko giza!


Baba Mtakatifu Francisko, tarehe 31 Mei 2014 amekutana na kuzungumza na kundi la watoto kutoka Kusini mwa Italia lililofika mjini Roma kama sehemu ya majadiliano ya kidini yanayoendeshwa na Baraza la Kipapa la utamaduni. Baba Mtakatifu amewashukuru watoto hawa kwa kumpatia zawadi mbali mbali, ikiwa ni udongo kutoka kwenye Makatakombe ya Mtakatifu Gennaro pamoja na mti wa mwanga ili kuifanya dunia kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi. Amewakumbusha kwamba, Mtakatifu Gennaro ni kati ya watakatifu wanaoheshimiwa sana mjini Napoli.

Udongo waliomletea Baba Mtakatifu uwasaidie kufukuza giza katika maisha yao, tayari kuwa ni watoto wema wanaotembea katika mwanga wa maisha mapya unaosheheni furaha na matumaini na kwamba jambo hili linawezekana kabisa. Baba Mtakatifu Francisko katika mtindo wa mahojiano ya maswali na majibu aliwataka kujitahidi kuondokana na chuki pamoja na uhasama wakijishikamanisha katika upendo kwa kusaidiana na kutaabikiana kama ndugu wamoja, kwani Mungu ni upendo. Watoto hawana budi kutembea katika mwanga wa upendo wakiwa na imani ya kuweza kukutana na Mwenyezi Mungu.

Baba Mtakatifu amewashukuru sana watoto hawa kwa kumtembelea na kwamba amefarijika sana. Watoto kwa upande wao wanasema, wamefurahi kupindukia kuonana na kuzungumza na Baba Mtakatifu Francisko. Mwishoni, amesali na kuwabariki ili kweli waweze kuwa ni vyombo vya upendo katika hija ya maisha yao!








All the contents on this site are copyrighted ©.