Maendeleo ya sayansi na teknolojia ya vyombo vya upashanaji habari ni utamaduni unaoendelea
kuleta mabadiliko makubwa katika maisha ya mwanadamu kwani kuna mambo mazuri ambayo
yanapaswa kuendelezwa kwa ajili ya mafao ya wengi pamoja na kuangalia matatizo na
changamoto zinazotolewa na vyombo hivi vya habari katika maisha ya mwanadamu.
Vyombo
vya mawasiliano ya kijamii vinapaswa kujenga na kudumisha utamaduni wa watu kukutana
kama anavyokazia Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake kwa Siku ya 48 ya Upashanaji
habari Ulimwenguni iliyoadhimishwa tarehe 1 Juni 2014 wakati Mama Kanisa alipokuwa
anasherehekea Siku kuu ya Kupaa Bwana Mbinguni.
Hivi ndivyo Baraza la Maaskofu
katoliki Hispania linavyobainisha katika ujumbe wao kwa maadhimisho ya Siku ya Upashanaji
Habari Ulimwenguni. Kati ya changamoto kubwa zinazoendelea kujitokeza katika matumizi
ya vyombo vya mawasiliano ya jamii ni baadhi ya watu kutengwa, na wengine kuendelea
kuishi katika ulimwengu wa kufikirika, kiasi cha kushindwa kumwilisha upendo katika
maisha yao ya kawaida. Kuna ombwe kubwa kati ya vijana wa kizazi kipya na wazazi wao.
Maaskofu wa Hispania wanakiri kwamba, kuna faida kubwa katika matumizi ya
vyombo vya habari kwani watu waweza kupata habari nyingi kwa urahisi na wanaweza kubadilishana,
kushirikishana mang’amuzi na kujenga umoja na mshikamano kati yao! Maaskofu wanaendelea
kuwahimiza vijana kuhakikisha kwamba, wanajenga utamaduni wa kukutana, ili kweli teknolojia
mpya iwe ni kwa ajili ya huduma kwa kwa binadamu na mafao ya wengi.
Wadau
wa vyombo vya mawasiliano ya jamii wanayo dhamana kubwa katika utekelezaji wa majukumu
yao ya kila siku. Kuna haja kwa jamii kuwa na majiundo makini ya matumizi sahihi ya
vyombo vya mawasiliano ya jamii, ili kuwa na ufahamu wa kina kuhusu jamii inayowazunguka
na kufanya mang’amuzi ya kina ili kuchangia katika mchakato wa kueneza ukweli.
Baraza
la Maaskofu Katoliki Hispania linabainisha kwamba, wafanyakazi katika sekta ya mawasiliano
ya jamii wanafanya kazi katika mazingira magumu na yenye kinzani, wakati mwingine
kwa ajili ya kutafuta mafao binafsi, kuliko hata kuzingatia ukweli, uzuri, wema na
maadili, tunu msingi katika upashanaji habari. Uhuru, ukweli na maadili ni mambo yanayopaswa
kuzingatiwa badala ya kuendekeza umbea, uchochezi na kinzani za kijamii. Maaskofu
wanawapongeza wadau mbali mbali wanaotekeleza majukumu yao katika vyombo vya upashanaji
habari ulimwenguni!