2014-06-02 10:28:54

Haitoshi tu kulaani vitendo vya kigaidi!


Kikundi cha kigaidi cha Boko Haram kinachoendelea kusababisha maafa makubwa nchini Nigeria ni tatizo linalojikita katika masuala ya kijeshi, kiuchumi, kisiasa, kijamii na hata kidini. Hivi ndivyo anavyobainisha Sultan Muhammad Sa’ad Abubakar III kutoka Sokoto ambaye pia ni Rais wa Baraza kuu la Waislam nchini Nigeria wakati wa swala ya kuombea wasichana waliotekwa nyara nchini Nigeria ili waweze kuachiliwa!

Anasema, vitendo vya kigaidi havina nafasi katika dini ya Kiislam na kwamba, Waislam wote hawana budi kuungana kwa pamoja kupinga vitendo vya kigaidi sehemu mbali mbali za dunia, ili kuhakikisha kwamba, amani, utulivu na upendo vinatawala kati ya watu.

Kardinali John Onaiyekan wa Jimbo kuu la Abuja, Nigeria ameunga mkono tamko hili lililotolewa na Sultan Muhammad Sa’aad Abubakar III kutoka Sokoto kwa kuonesha ujasiri na nia njema kwa kile kinachoendelea kuzunguka katika mawazo na mioyo ya wananchi wengi nchini Nigeria. Wasichana 250 waliotekwa ni tatizo kubwa, lakini linaloonesha hali tete ya vitendo vya kigaidi ambavyo vimekuwa vikifanywa na Kikundi cha kigaidi cha Boko Haram nchini Nigeria.

Serikali ya Nigeria haina budi kulivalia njuga tatizo la Boko Haram ili kung’oa mzizi wake kwa kuzingatia ukweli kwamba, kuna masuala ya kidini yanayofumbatwa katika mashambulizi haya. Haitoshi kulaani vitendo vya kigaidi, lakini kuna haja ya kuendeleza mchakato wa majadiliano ya kidini yanayosimikwa katika ukweli, uwazi na mafao ya wengi, ili kweli amani iweze kupatikana nchini Nigeria.








All the contents on this site are copyrighted ©.