Ujumbe wa Siku ya 48 ya Upashanaji Habari Ulimwenguni kwa Mwaka 2014
Mama Kanisa tarehe Mosi Juni, 2014 anaadhimisha Siku kuu ya Kupaa Bwana Mbinguni sanjari
na Siku ya 48 ya Upashanaji Habari Ulimwenguni, inayoongozwa na kauli mbiu “Mawasiliano
katika huduma ya kweli ya utamaduni wa kukutana”.
Baba Mtakatifu
anasema kwamba, watu wanaishi katika ulimwengu ambao ni kama kijiji kwani watu wanakaribiana
sana, na njia za mawasiliano ya jamii zimeboreka zaidi katika ulimwengu wa utandawazi
kiasi kwamba, kuna mwingiliano mkubwa wa watu.
Lakini jambo la kusikitisha
anasema Baba Mtakatifu ni kuona kwamba, bado kuna migawanyiko katika Familia ya binadamu,
kuna pengo kubwa kati ya matajiri na maskini kiasi kwamba, tofauti hizi kubwa ambazo
zinapaswa kuonekana kuwa kashfa katika maisha ya binadamu, zimeanza kuzoeleka na kuwa
ni jambo la kawaida kabisa. Dunia inaendelea kuteseka kutokana na utengano, umaskini,
vita na kinzani zinazojikita katika masuala ya kiuchumi, kisiasa na hata wakati mwingine
kidini!
Ni matumaini ya Baba Mtakatifu Francisko kwamba, njia za mawasiliano
ya kijamii zinaweza kuwajengea watu ari ya umoja na mshikamano katika familia ya binadamu,
ili kukuza na kudumisha utu na heshima ya binadamu. Mawasiliano yanaweza kusaidia
kubomoa kuta za utengano kwa kujenga utamaduni wa kusikilizana na kujifunza kutoka
kwa wengine, ili hatimaye, kukuza majadiliano yanayowawezesha watu kufahamiana na
kuheshimiana. Utamaduni wa kukutana unadai watu kuwa tayari si tu kutoa bali pia kupokea.
Njia za mawasiliano ya kijamii ambazo zimeboreska kwa kiasi kikubwa kutokana na maendeleo
ya sayansi na teknolojia zinaweza kuwa ni msaada mkubwa unaotoa fursa ya watu kukutana
na kwamba, njia za mawasiliano kwa hakika ni zawadi kutoka kwa Mungu.
Baba
Mtakatifu anatambua matatizo na changamoto zinazoendelea kujitokeza katika njia za
mawasiliano ya kijamii hasa kutokana na kiasi kikubwa cha habari kinachotolewa na
watu kushindwa kupata fursa ya kucheua na kutolea maamuzi. Baadhi ya habari zina utata
na zinajikita katika masuala ya kisiasa na kiuchumi. Njia za mawasiliano ya kijamii
zina mchango mkubwa katika kukuza ufahamu wa watu au kuwavuruga; kuwaunganisha au
kuwatenganisha.
Ikumbukwe kwamba, kuna watu ambao kutokana na sababu mbali
mbali hawana nafasi katika matumizi ya mitandao ya kijamii, changamoto ya kutambua
kwamba, mawasiliano ni jambo la kibinadamu na wala si tu katika maendeleo ya digitali,
jambo linalohitaji ukimya, usikivu, uvumilivu kutokana na tamaduni pamoja na mapokeo
mbali mbali. Waamini wajifunze kuthamini na kuenzi tunu msingi za maisha ya binadamu
zinazopata chimbuko lake katika Ukristo, hasa kuhusiana na utu na heshima ya binadamu;
asili ya ndoa na familia, tofauti kati ya dini na siasa pamoja na mshikamano unaoongozwa
na kanuni ya auni.
Baba Mtakatifu Francisko anasema, utamaduni wa kukutana
unajikita katika dhana ya mtu kumtambua jirani yake katika mazingira yanayoundwa na
ulimwengu wa digitali kwa kuwa Wasamaria wema, ili kushiriki katika shida na mahangaiko
ya wengine, kwani wote ni watoto wa Mungu. Nguvu ya mawasiliano inajidhihirisha katika
ujirani.
Mawasiliano yanayojikita katika kuwavuruga na kuwachanganya wengine
kama inavyojionesha kwenye mfano wa Msamaria mwema, kwa baadhi ya watu ndani ya jamii
kutoguswa na mahangaiko ya jirani zao kwa sababu mbali mbali kuna hatari kwamba, watu
wakashindwa kuwaona jirani zao! Haitoshi kila wakati watu kuwa wameunganika kwenye
mitandao, lakini wanapaswa kukutana kweli kweli kwa kupenda na kupendwa pamoja na
kufarijiwa.
Kwa bahati mbaya mikakati ya vyombo vya mawasiliano havipanii
sana kuonesha uzuri, wema na ukweli katika mawasiliano, changamoto kwa vyombo hivi
kuonesha ubinadamu na huruma ili kuwaunganisha watu na wala si waya na kwamba wadau
wa njia za mawasiliano wanaweza kuwa ni msaada na rejea kwa wengine, watu wanaoaminiwa
katika mawasiliano. Ushuhuda wa Kikristo katika mitandao ya kijamii ni muhimu sana
ili kuwafikia hata wale walioko pembezoni mwa jamii!
Baba Mtakatifu Francisko
anasema, kuna umati mkubwa wa watu wanaoishi pembezoni mwa jamii, hawa ndio wanaopaswa
kupewa kipaumbele cha kwanza na kwamba, mchakato huu unaweza kukolezwa kwa njia ya
mitandao ya kijamii; hawa ni watu wenye madonda wanaohitaji, faraja na matumaini.
Kwa njia ya njia za mawasiliano ya kijamii ujumbe wa Kikristo unaweza kufika hata
miisho ya dunia. Makanisa na mitandao ya kijamii, iendelee kuwa wazi ili watu waweze
kuingia na kujichotea utajiri wa Neno la Mungu.
Mawasiliano ya kijamii iwe
ni fursa ya kuelezea wito wa kimissionari unaofumbatwa na Mama Kanisa, ili kuwasaidia
watu kutambua uzuri wa imani pamoja na kukutana na Yesu Kristo. Hata katika uwanja
wa mawasiliano ya jamii, Kanisa halina budi kusaidia kuleta joto na kuamsha ari miongoni
mwa watu, kwa kuonesha uwepo katika kutafuta ukweli na maana ya maisha ya mwanadamu.
Kanisa halina budi kujenga utamaduni wa majadiliano, ili kuwafahamu watu, kujua matumaini
na mashaka yao, ili hatimaye, kuwapekea Injili, Yesu Kristo, Neno wa Mungu aliyefanyika
mwili, akateswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu. Watu wawe makini na matukio
mbali mbali yanayowazunguka hasa katika maisha yao ya kiroho. Majadiliano ya kweli
yanajikita katika kuaminiana na kuthaminiana katika mchakato wa kushirikishana mawazo
kwani hakuna mtu anayeweza kujidai kwamba mawazo yake ndiyo ya kweli tu!
Baba
Mtakatifu Francisko anahitimisha ujumbe wake kwa siku ya 48 ya Upashanaji Habari Ulimwenguni
kwa kuwataka waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema kumwangalia Msamaria mwema,
ili aweze kuwa ni mfano bora wa kuiga katika kuganga madonda ya watu na kuufurahisha
moyo. Watu waguswe na mwanga wa upendo na huruma, ili kwa pamoja waweze kuwa kweli
ni raia wa ulimwengu wa digitali.
Kanisa halina budi kuwepo katika mitandao
ya kijamii ili kushiriki katika mchakato wa majadiliano na watu wa dunia ya sasa ili
waweze kukutana na Yesu. Kanisa lijitahidi kuwa ni mwenza wa safari katika maisha
ya mwanadamu. Mabadiliko na maendeleo ya sayansi na teknolojia katika njia za mawasiliano
ya jamii ni changamoto kubwa inayopaswa kufanyiwa kazi na Kanisa kwa kuwa na nguvu
mpya ili kuwashirikisha wengine uzuri wa Mungu.
Imehaririwa na Padre Richard
A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.