2014-05-30 12:16:53

Nyanyaso za kijinsia zina madhara makubwa kwa watoto!


Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya linasema kwamba, nyanyaso za kijinsia dhidi ya watoto wadogo zinawaathiri sana watoto katika makuzi na malezi yao kwa sasa na kwa siku za baadaye. Nyanyaso hizi zinagusa undani wa utu na heshima ya mwanadamu pamoja na utakatifu wake, kwani mwanadamu ameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu! Kanisa Katoliki nchini Kenya katika mwongozo wake wa Mwaka 2011 linasema kwamba, linataka kusimamia na kuwalinda watoto.

hayo yamebainishwa hivi karibuni na Padre Daniel Rono, Katibu mkuu Msaidizi wa Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya wakati akitoa hotuba kwa washiriki wa semina ya ulinzi wa watoto wadogo iliyohudhuriwa na wakufunzi kutoka Majimbo yote yanayounda Kanisa Katoliki nchini Kenya pamoja na wageni waalikwa kutoka Zimbabwe.

Padre Rono anasema, waamini na watu wote wenye mapenzi mema wanaalikwa na kuchangamotishwa na Mama Kanisa kusimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu tangu pale mtoto anapotungwa mimba tumboni mwa mama yake hadi mauti ya kawaida yanapomfika kadiri ya mapenzi ya Mungu. Maisha ni matakatifu kwa sababu ni zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu ambayo binadamu amekabidhiwa kuilinda, kuitunza na kuiendeleza. Kumbe, kuna haja kwa Kanisa kuwa macho zaidi dhidi ya nyanyaso kwa watoto wadogo!

Nyanyaso zina madhara makubwa kwa watoto kwani zinaharibu taswira yao, uwezo wao wa kuhusiana na watu wengine hata watakapokuwa watu wazima; wanaathirika katika masomo na makuzi yao na matokeo yake wanaweza kujikita kwamba, wametumbukia katika matumizi haramu ya dawa za kulevya na ukahaba, mwendelezo wa utumwa mamboleo kwa watu wa nyakati hizi. Ni watu wanaweza kukumbwa na msongo wa mawazo na hatimaye, kutema zawadi ya maisha kwa kujinyonga! Haya ni baadhi ya madhara ambayo anaweza kupata mtoto aliye nyanyaswa kijinsia.

Kanisa nchini Kenya linataka kuhakikisha kwamba, watoto wanaopata huduma mbali mbali katika taasisi zake wanakuwa salama, kwani wameumbwa na Mwenyezi Mungu, ni wema na watakatifu; wanapendwa na kuthaminiwa na Mungu mwenyewe na kwamba, wana fursa ya kuanzisha mchakato wa maisha yao kwa siku za usoni. Watoto wafundishwe kuwatambua watu wanaoweza kuwanyanyasa kijinsia kwa njia za ulaghai.







All the contents on this site are copyrighted ©.