2014-05-28 08:23:34

Je kustaafu kwa Papa Benedikto XV1, kunaweza kujenga utamaduni wa Mapapa kustaafu ?


Baba Mtakatifu Francisko , Jumatatu akiwa njiani kurejea Roma , alijibu maswali yote 11 yaliyoulizwa na waandishi wa habari. Kati ya maswali hayo ni iwapo kujiuzuru kwa Papa Benedikto XV1, kunaweza kujenga utamaduni kwa Kanisa kwa Mapapa kustaafu wakifikia umri fulani .
Katika maelezo yake Papa Francisko alisema, ni wazi pia yeye angependa kustaafu mapema kama mtangulizi wake Benedict XVI, badala ya kutawala maisha yake yote, na kuongeza inawezekana dhana ya " Papa kustaafu " usoni inaweza kuwa jambo la kawaida katika kanisa.
Hata hivyo, amesema, yeye mpaka sasa ataendelea kulitumia Kanisa kwa kadri Mungu anavyomjalia kiafya .Na anaweza kuachia ngazi iwapo afya yake haitamruhusu kuendelea kuliongoza kundi la Mungu la waamini wa Kanisa Katoliki wapatao bilioni 1.2 . Na kwamba kustaafu kwa Papa Benedikto XV1, isichukuliwe kama ni hatua ya kushangaza, lakini kama kufungua mlango kwa Mapapa kustaafu.
Papa Francisko mwenye umri wa miaka 77 aliwaambia wanahabari, akitafakari hali halisi kwamba, kwa sasa watu wengi wanaishi hadi umri mkubwa , na hii inaonyesha uwezekano kwa siku zijazo, Mapapa kujiuzuru kutokana na umri mkubwa na hasa sababu za kiafya . Lakini hili hakuna mwenye kujua kwa sababu afya ya Mtu ni kudra ya Mungu.
Kujiuzuru kwa hiari kwa Papa Benedikto XV1, Mwezi Februari mwaka jana, kuliandika historia mpya ya Papa kujiuzuru, tangu Zama za Nyakati za Kati. .
Salaam kwa Marais
Baba Mtakatifu pamoja na kujibu maswali ya waandishi wa habari, akisafiri kwa aina ya ndege B777 el Al, kuelekea Roma, pia alituma salaam zake za Matashi mema kwa kila Rais wa nchi ambako ndege yake ilipita.
Akipita katika anga la Nchi ya Cyprus, alipeleka salaam zake kwa Mheshimiwa Rais Nicos Anastasiades
Rais wa Jamhuri ya CYPRUS, na Rais Karolos Papoulias wa Ugriki, akisema, kwa mara ingine tena natoa salaam zangu kwako na kwa wananchi wa Cyprus, wakati ninaporejea Rome tokea Nchi Takatifu . Naomba Bwana, awabariki kila mmoja wenu kwa neema na amani na furaha .

Na pia ndege ya Papa ilipita katika anga la Albania, na kutoa salaam zake kwa Rais Bujar Nishani
Rais wa Jamhuri ya ALBANIA , na kwa Mheshimiwa Rais Giorgio Napolitano wa Italia, akisema, anarudi nchini Italia baada ya kukamilisha hija yake katika Nchi Takatifu, ambako alikwenda kuhamasisha njia ya amani na mapatano baina ya watu na dini. Na sasa kwake yeye Rais Napolitano na wananchi wa Italia, anamtolea Mungu ombi maalum, kwa manufaa ya taifa zima la Italia.
Na Rais Napolitano mara alijibu salaam za Papa kwa kuonyesha matumaini yake kwamba, mwaliko wa kihistoria wa Papa kwa Marais wa Israel na Palestina kukutana Vatican, kunatoa matumaini mapya utulivu na amani katika mtazamo wa kuanza kwa mazungumzo ya amani kisiasa na kati ya Wakristo, Wayahudi na Waislamu. Rais wa Jamhuri ya Italia, Giorgio Napolitano, katika telegram yake kwa Papa ameiita ziara ya Papa katika nchi Takatifu kuwa ya kukumbukwa na kugusa mioyo ya wale wote wanaopenda amani na utulivu duniani.
Papa alitua katika uwanja wa Ciampino (Rome) Jumatatu usiku na kurejea Vatican salama salimini.








All the contents on this site are copyrighted ©.