Hija ya Papa Francisko alama ya matumaini ya umoja wa Kanisa
Dr. Olav Fykse Tveit, Katibu mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni anasema mkutano
kati ya Baba Mtakatifu Francisko na Patriaki Bartolomeo wa kwanza wa Kanisa la Kiorthodox
la Costantinopoli, mwishoni mwa juma, ni tukio la kihistoria katika kukuza na kuendeleza
ari zaidi katika majadiliano ya kiekumene miongoni mwa Makanisa.
Mkutano wa
viongozi hawa wakuu wa Makanisa uliofanyika mjini Yerusalemu Jumapili tarehe 25 Mei
2014 kwa kushirikisha mang'amuzi na vipaumbele vyao ni hija ya maisha ya kiekumene
kuelekea katika ujenzi wa misingi ya haki na amani! Viongozi wa Makanisa katika tamko
lao la pamoja wanakiri kwamba, wako katika hija ya umoja wa Kanisa unaoongozwa na
Roho Mtakatifu katika umoja unaonesha tofauti za kweli. Haya ni mambo msingi yaliyojadiliwa
pia katika mkutano wa kumi wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni huko Korea ya Kusini.
Dr.
Tveit anasema, mkutano wa viongozi hawa wa Makanisa umekuwa na maana kubwa kwa wao
kukutana, kuzungumza na kusali mjini Yerusalemu kwenye Kaburi Takatifu, chemchemi
ya imani ya Kanisa. Kwa hakika anasema Dr. Tveit, waamini na wananchi wanaoishi huko
Mashariki ya Kati wameongezewa matumaini mapya katika hija ya maisha yao ya kiimani
pamoja na kuendeleza mchakato wa amani na utulivu huko Mashariki ya Kati.
Sala
na mkutano wa viongozi hawa ni changamoto kwa Makanisa kuendeleza mchakato wa haki
na amani kwa watu wanaoishi huko Mashariki ya Kati pamoja na kuendelea kuimarisha
maisha na utume wa Kanisa. Majadiliano ya kidini na waamini wa dini nyingine yamepewa
mkazo wa pekee katika tamko la viongozi hawa wa Makanisa, lakini majadiliano ya kidini
yana uzito wa pekee huko Mashariki ya Kati kutokana na kinzani za muda mrefu ambazo
zimesababisha maafa makubwa, kiasi kwamba, baadhi ya Wakristo wanalazimika kuzikimbia
nchi zao kutokana na madhulumu ya kidini.
Dr. Olav Tveit anasema hija ya Baba
Mtakatifu Francisko katika Nchi Takatifu kama kumbu kumbu ya Jubilee ya miaka 50 tangu
Papa Paulo VI alipokutana na kusali pamoja na patriaki Anathegoras wa Yerusalemu imekuwa
ni alama ya matumaini na umoja kwa Makanisa yote ulimwenguni!