Jubilee ya Miaka 100 ya Uinjilishaji Jimbo kuu la Bamenda, Cameroon!
Kardinali Fernando Filoni, Rais wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa watu yuko nchini
Cameroon kwa ajili ya maadhimisho ya Jubilee ya miaka 100 ya Ukristo Jimbo kuu la
Bamenda. Akiwa nchini Cameroon, Kardinali Filoni anakutana na walezi pamoja na majandokasisi
kutoka Seminari kuu ya Nkolbisson, Yaounde.
Kardinali Filoni atapata pia fursa
ya kuzungumza na Baraza la Maaskofu Katoliki Cameroon na wakati wa maadhimisho ya
Siku kuu ya Kupaa Bwana mbinguni, hapo tarehe 29 Mei 2014, ataadhimisha Ibada ya Misa
Takatifu kama kilele cha kufunga Jubilee ya Miaka 100 ya Ukristo Jimbo kuu la Bamenda.
Hapa Mashemasi 9 watapewa Daraja Takatifu la Upadre na Waseminari 7 wapatata Daraja
la Ushemasi.
Kardinali Filoni, tarehe 30 Mei anatarajiwa kutembelea Kanisa
kuu la Bikira Maria Mkingiwa dhambi ya asili na tarehe 31 Mei 2014 ataadhimisha Ibada
ya Misa Takatifu akishirikiana na Maaskofu na Mapadre kutoka Guinea. Jioni atakutana
na kuzungumza na Maaskofu pamoja na Makleri wa Guinea. Jumapili tarehe Mosi, Juni,
Kardinali Filoni atatembelea Seminari kuu ya Falsafa, mahali majandokasisi wanaponolewa
kwa falsafa. Jumatatu, tarehe 2 Juni 2014 atahitimisha hija yake ya kichungaji na
kurejea mjini Vatican kuendelea na utume wake.