Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda amepokea msaada wa mabati 350 yenye thamani
ya milioni 17.2 ikiwa ni mchango kutoka Mfuko wa Hifadhi ya Jamii wa GEPF kwa ajili
ya ujenzi wa shule ya msingi Kakuni iliyoko katika kijiji cha Kibaoni, Wilayani Mlele,
Mkoani Katavi. Waziri Mkuu amepokea mchango huo Jumatatu, Mei 26, 2014 kwenye eneo
la shule hiyo wakati akiwa njiani akitokea Sumbawanga, Rukwa ambako alimwakilisha
Rais Jakaya Kikwete kwenye ibada ya kumuweka wakfu Askofu Mteule Conrad Nguvumali
wa Kanisa la Moravian Tanzania, Jimbo la Rukwa. Akitoa taarifa fupi ya ujenzi wa
shule hiyo, Katibu Tawala wa Mkoa wa Katavi, Mhandisi Emmanuel Kalobelo alisema shule
hiyo mpya inajengwa ili iwe mbadala wa shule ya zamani ambayo alisoma Waziri Mkuu
Mizengo Pinda mwishoni mwa miaka ya 50. “Wazo la kujenga shule hii upya lilitoka
kwako wewe mwenyewe hasa kwa kuzingatia uchakavu wa majengo ya shule, ufinyu wa eneo
ilipo shule kwa sasa ukilinganisha na wingi wa wanafunzi na mahitaji ya kielimu na
kuongezeka kwa mahitaji na miundombinu muhimu kulingana na mahitaji ya shule kwa sasa,”
alisema Bw. Kalobelo. Bw. Kalobelo alisema kutokana na wazo hilo, uongozi wa Serikali
ya Kijiji ulitoa ekari 66 kwa hiari yao ili shule hiyo mpya ijengwe. “Sisi kama Serikali
ya Mkoa tunakushuru kwa wazo lako hili ambapo unaendelea kuwezesha ujenzi wa Shule
hii kupitia michango ya wadau mbalimbali,” aliongeza. Bw. Kalobelo alisema shule
hiyo itakuwa ya kwanza Kimkoa kwa kuwa na miundombinu ya kisasa kwani kutakuwa na
madarsa 14, jengo la utawala, maktaba ya wanafunzi na walimu, vituo vya ICT viwili
(kimoja cha wanafunzi na kingine cha walimu), kumbi za mikutano mbili na bwalo la
chakula. Alitaja vitu vingine kuwa ni viwanja vya michezo vya kisasa, nyumba za
walimu tisa, vyoo vyenye matundu 48, maji na umeme, eneo la maduka (Shopping Centre),
karakana za ufundi ushonaji nguo na viatu, useremela na ufundi makenika, shule ya
awali ya kisasa na sehemu ya shughuli za kilimo cha bustani (Elimu ya Kujitegemea). Akiwasilisha
mchango huo, Mkurugenzi Mtendaji wa GEPF, Bw. Daudi Msangi alisema wamekabidhi kwanza
mabati 151 na kofia 40 na watakamilisha mabati mengine 200 baada ya muda mfupi. “Awali
tulipanga kuchangia mabati kwa ajili ya jengo la TEHAMA lakini kwa vile bado halijaanza
kujengwa, tumeamua kuchangia jengo la utawala pamoja na madarasa mawili yaliyobakia,”
alisema. Naye Mwenyekiti wa Kijiji cha Kibaoni, Bw. Gaston Kamine alisema wanashukuru
kwa msaada huo na wanasubiri kwa hamu kukamilika kwa ujenzi wa shule hiyo. Alisema
kama kijiji, wako tayari kutoa msaada wowote wakati wakihitajika kufanya hivyo. Akitoa
shukrani kwa Mfuko wa GEPF, Waziri Mkuu Pinda alisema mchango walioutoa ni msaada
mkubwa sana na utachangia kukamilisha jengo la utawala ambalo ujenzi wake umekaribia
kwenye linta. Hadi sasa, ujenzi wa shule hiyo ambao ulianza mwishoni mwa kama
2013, umekamilika kwa kujenga madarasa 12 na mawili yatakamilika baada ya jengo la
utawala kukamilika.