2014-05-27 14:14:12

Jitokezeni kuchangia maendeleo ya elimu!


Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda amepokea msaada wa mabati 350 yenye thamani ya milioni 17.2 ikiwa ni mchango kutoka Mfuko wa Hifadhi ya Jamii wa GEPF kwa ajili ya ujenzi wa shule ya msingi Kakuni iliyoko katika kijiji cha Kibaoni, Wilayani Mlele, Mkoani Katavi.
Waziri Mkuu amepokea mchango huo Jumatatu, Mei 26, 2014 kwenye eneo la shule hiyo wakati akiwa njiani akitokea Sumbawanga, Rukwa ambako alimwakilisha Rais Jakaya Kikwete kwenye ibada ya kumuweka wakfu Askofu Mteule Conrad Nguvumali wa Kanisa la Moravian Tanzania, Jimbo la Rukwa.
Akitoa taarifa fupi ya ujenzi wa shule hiyo, Katibu Tawala wa Mkoa wa Katavi, Mhandisi Emmanuel Kalobelo alisema shule hiyo mpya inajengwa ili iwe mbadala wa shule ya zamani ambayo alisoma Waziri Mkuu Mizengo Pinda mwishoni mwa miaka ya 50.
“Wazo la kujenga shule hii upya lilitoka kwako wewe mwenyewe hasa kwa kuzingatia uchakavu wa majengo ya shule, ufinyu wa eneo ilipo shule kwa sasa ukilinganisha na wingi wa wanafunzi na mahitaji ya kielimu na kuongezeka kwa mahitaji na miundombinu muhimu kulingana na mahitaji ya shule kwa sasa,” alisema Bw. Kalobelo.
Bw. Kalobelo alisema kutokana na wazo hilo, uongozi wa Serikali ya Kijiji ulitoa ekari 66 kwa hiari yao ili shule hiyo mpya ijengwe. “Sisi kama Serikali ya Mkoa tunakushuru kwa wazo lako hili ambapo unaendelea kuwezesha ujenzi wa Shule hii kupitia michango ya wadau mbalimbali,” aliongeza.
Bw. Kalobelo alisema shule hiyo itakuwa ya kwanza Kimkoa kwa kuwa na miundombinu ya kisasa kwani kutakuwa na madarsa 14, jengo la utawala, maktaba ya wanafunzi na walimu, vituo vya ICT viwili (kimoja cha wanafunzi na kingine cha walimu), kumbi za mikutano mbili na bwalo la chakula.
Alitaja vitu vingine kuwa ni viwanja vya michezo vya kisasa, nyumba za walimu tisa, vyoo vyenye matundu 48, maji na umeme, eneo la maduka (Shopping Centre), karakana za ufundi ushonaji nguo na viatu, useremela na ufundi makenika, shule ya awali ya kisasa na sehemu ya shughuli za kilimo cha bustani (Elimu ya Kujitegemea).
Akiwasilisha mchango huo, Mkurugenzi Mtendaji wa GEPF, Bw. Daudi Msangi alisema wamekabidhi kwanza mabati 151 na kofia 40 na watakamilisha mabati mengine 200 baada ya muda mfupi.
“Awali tulipanga kuchangia mabati kwa ajili ya jengo la TEHAMA lakini kwa vile bado halijaanza kujengwa, tumeamua kuchangia jengo la utawala pamoja na madarasa mawili yaliyobakia,” alisema.
Naye Mwenyekiti wa Kijiji cha Kibaoni, Bw. Gaston Kamine alisema wanashukuru kwa msaada huo na wanasubiri kwa hamu kukamilika kwa ujenzi wa shule hiyo. Alisema kama kijiji, wako tayari kutoa msaada wowote wakati wakihitajika kufanya hivyo.
Akitoa shukrani kwa Mfuko wa GEPF, Waziri Mkuu Pinda alisema mchango walioutoa ni msaada mkubwa sana na utachangia kukamilisha jengo la utawala ambalo ujenzi wake umekaribia kwenye linta.
Hadi sasa, ujenzi wa shule hiyo ambao ulianza mwishoni mwa kama 2013, umekamilika kwa kujenga madarasa 12 na mawili yatakamilika baada ya jengo la utawala kukamilika.








All the contents on this site are copyrighted ©.