Mpendwa msikiliziaji wa Kipindi chetu pendevu cha Kanisa la Nyumbani, Tumsifu Yesu
Kristo! Karibu katika mwendelezo wa mada yetu ‘maisha baada ya Pasaka’. Lengo letu
ni kukumbushana, sisi kama Wakristo tuishi vipi upasaka wetu.
Kipindi kilichopita
tulisema kwamba, maisha yetu ya kipasaka yaongozwe na matendo mawili makuu ya Kristo.
Tendo la kuweka Ekaristi, ambapo tunamtazama Kristo aliyejisadaka, aliyejimega kwa
ajili yetu na akaagiza tufanye vile vile kwa kumkumbuka yeye, na tendo la kuwaosha
miguu wanafunzi wake, napo pia anaagiza akisema, nimewapeni mfano, ili ninyi nanyi
mfanye vilevile. Kipindi kilichopita tulitafakari zaidi Uekaristi wetu katika familia
(hasa wazazi) na katika mazingira yetu ya kazi.
Tunakazia maarifa kusema,
sisi wakristo ni wabebakristo-wachukuakristo. Hivyo sote tuna wito wa pamoja kama
wa-Kristo, kumdhihirisha Kristo huyo kwa watu nyakati zote. Kumchukua Kristo na kumpeleka
katika mazingira ya maisha yetu ya kila siku. Neno kuu ni hili, tuwe tayari kujitoa
sadaka kwa ajili ya wenzetu. Tuwe tayari kujimega ili kuchangia hali njema ya mwanadamu.
Ni hivyo tu, tutamtambulisha na kumuenzi Kristo Yesu aliye sadaya ya wokovu wetu.
Na wakati huohuo tufanyapo hivyo, sisi hatuwi tu Wakristo, bali tunakuwa nasi sadaka
kwa ajili ya wokovu wa wengine.
Leo tuendelee na tafakari yetu kwa kutazama
sehemu ile ya pili, yaani tendo la kuwaosha miguu wanafunzi wake. Ili ujumbe ufike
kikamilifu, tuchukue maana ile mmoja tu ya kawaida yaani, katika tendo lile, kristo
bwana anawafundisha wanafunzi wake utumishi mnyenyekevu. Watumikiane kwa upendo, wasaidiane,
wainuane, watakasane, wanyenyekeane. Ni kwa njia hiyo tu wataweza kueneza vema ujumbe
wa Injili.
Ndiyo maana anawapa swali zito sana akisema “"Je, mmeelewa hayo
niliyowatendeeni?” (Yoh 13:12). Anaendelea kusema “Nimewapeni mfano, ili nanyi pia
mfanye kama nilivyowafanyieni” (Yoh. 13:15). Sisi nasi tunataka maisha yetu
ya kipasaka, yapambwe na Utumishi mwema na mnyenyekevu. Hatuwezi kuwa wainjilishaji
kama hatupo tayari kutumikiana. Tutumikie kama Yesu alivyotufundisha.
Utumishi
wetu unalenga kuwagusa wanadamu wote katika hali mbalimbali. Lengo la kufanya hivyo
ni kumfanya Kristo aendelee kujulikana kwa watu na Injili yake imwilike katika maisha
ya kila siku. Huduma yetu kwa watu hatusemi iwafanye watu kuwa Wakristo, hapana! Ila
tunataka joto la upendo wa Kristo, liwaguse na kuwafariji wote.
Mambo yanayosaliti
utumishi wetu: Mpendwa msikikilizaji, kwa uchache tuyaangazie baadhi ya mambo
yanaweza kufisha utumishi wetu na hivyo kupelekea kutokuwa mabalozi wa kweli wa Kristo
Bwana aliyekuja kutumikia na sio kutumikiwa. Tukumbuke aliposema, nimewapeni mfano,
ili ninyi nanyi mtende vivyo hivyo.
Kupenda ajira kuliko utumishi Katika
mazingira yetu ya kila siku, tunajikuta katika hali ambayo wengi tunatafuta ajira.
Baadhi yetu wanabahatika kuajiriwa na wengine bado wanaendelea kutafuta. Na wakati
wa kutafuta ajira, kila mmoja anajawa na hamu ya kupata kazi ya kufanya. Anafuata
masharti yote hata kama ni magumu ali mradi apate ile ajira. Ajabu sasa, mtu akipata
tu ajira, haoneshi tena moyo na moto wa kuichangamkia huduma kwa watu. Katika kazi
yako, na ajira hiyo uwaone watu, tumikia watu kwa unyenyekevu wote.
Hukuajiriwa
tu kwa ajili yako, ni kwa ajili ya huduma. Na tunaomba kukumbusha hapa, ajira yako,
ni uwanja mpana zaidi wa kutangaza upendo wa mungu. Sasa kuna wale wenye bahati mbaya
kubwa, wanaotumia ajira zao kama ndio kitu cha kuwanyanyasa na kuwadharau wengine.
Tukiyakuta mazingira kama hayo katika familia, tuaona baba kabla hajapata ajira
alikuwa mtulivu, mwenye mshikamano na familia yake. Lakini mara tu alipopata ajira,
ameanza kuwa jeuri, hatulii nyumbani, warsha kila baada ya nusu saa, anadharau mke
wake na majirani, haendi kanisani tena nk. Mama naye kabla ya kupata ajira au kibarua
alikuwa mama mwema, mke mwema, msikivu na mnyenyekevu. Lakini baada ya kupata kazi,
anasahau familia yake. Nyumbani hafanyi kazi ya mama tena. Lugha za jeuri na matusi-mkuki
zinaanza, kisa?? Ameajiriwa siku hizi, naye anashika hela yake, yupo huru!!! Ndugu,
kazi yako isikunyang’anye utu wato!! Ajira yako ikuunganishe zaidi na wanadamu wenzako,
na Mungu pia. Huo ndiyo mfano aliotuachia Yesu.
Ubaguzi na upendeleo
Jambo
la pili linalosaliti utumishi wetu ni dhana ya ubaguzi na upendeleo inayoendelea kutamadunishwa
katika mazingira yetu ya kila siku. Tukumbuke kuwa upendeleo sio upendo. Upendeleo
hufukia haki. Jinsi Mungu wetu anavyowaangazia jua lake watu wabaya kwa wema, wenye
haki na wasio haki, Kristo naye aliwahubiria neno lake watu wote. Na sisi ametutuma
kwa watu wote wa mataifa yote. Ni aibu sana kama Mkristo katika hudumia anakuwa mbaguzi
na mwenye upendeleo. Katika mahali pa kazi kama msimamizi, unalundika ndugu zako tu
na marafiki zako, hata kama hawana uadilifu wala viwango vya kazi, hapo unaharibu
utumishi.
Kama tutawabagua wengine bila sababu halali, hapo tunaharibu utumishi.
Leo hii ofisi zetu nyingi zimepooza na kuudhi watu, kwa sababu ya ubaguzi na upendeleo.
Yesu aliwaosha miguu wote waliokuwako pale karamuni, hata wale wabishi. Utumishi mwema
na mnyenyekevu hauna ubaguzi wala upendeleo, bali umejaa upendo wa Yesu.
Kukosa
uadilifu katika kazi
Uadilifu ni tunu msingi katika kazi, inayoyengwa katika
dhamiri safi, imani kwa Mungu na uwajibikaji. Leo wengi tunashindwa kufanya kazi kiadilifu;
utamaduni wa uhovyohovyo na roho ya bora liende, ndiyo vinatawala kazi zetu, hasa
kazi za ajira, utumishi wa umma. Kukosa uadilifu kunajionesha zaidi katika roho ya
tamaa ya mali, kutojali muda wa kazi, kutojali watu tunaowahudumia, kuwa na madai
makubwa mno ya mishahara yasiyotazama wanyonge, roho ya ubadhilifu wa mali ya umma
bila kujali maslahi ya wote, roho ya uwongo-unganishi katika kazi na mambo kama hayo,
yanatufanya tusimwakilishe Kristo katika utumishi wetu. Mtumishi mwema na mwaminifu,
hujali ubora wa huduma, huheshimu muda, huheshimu watu na mali ya mafaa kwa wote,
na zaidi ya yote, humwona Kristo ndani ya watu wote!!
Utumishi wenye hila/ajenda
za siri
Mpendwa msikilizaji, mara nyingi, tumeathirika na roho ya kutafuata
faida binafsi katika mambo yote. Jambo hili linaharibu kabisa hata maana ya matendo
mema tunayoyatenda. Hii roho ya kutafuta faida binafsi ndiyo inayotupelekea kwenye
mitaala ya rushwa, na utamaduni wa ‘kitu kidogo’!! Katika hali hiyo, yule asiyeweza
kutoa kitu kidogo hatahudumiwa, na atakufa na shida zake hivyohivyo. Utumishi wa kweli
humlenga mtu kama mtu, na huelekezwa kwake huyo atumikiwaye bila kutegemea kupata
chochote kutoka kwake.
Hila katika utumishi tunaweza kuiona wazi katika mifano
ifuatayo:- Wizi: kuna watu wamejizoesha hivi, katika kazi yoyote lazima aibe tu, walao
hata kidogo tu!! Hiyo ni hila. Mwalimu, askari, muuguzi nk, amejizoesha kupokea rushwa
tu, hata kama ni ya pera moja. Huwa inakuwaje pale ambapo, baba unajitolea kusomesha
yatima, halafu mwisho wa siku huyo yatima anakuwa mke wako. Sasa ulikuwa unamsomesha
au ulikuwa na ajenda ya ten parsenti? Huo ndio utumishi wenye ajenda zilizofichika.
Yesu hakutufundisha hivyo. Sijui unafanya hivyo kwa kumkumbuka nani?? Migogoro
na migongano ya kazini
Wazee wetu walitufundisha wakisema, migogoro na
migongano ya kazini ni ukosefu wa nidhamu. Kuna nyakati tunashindwa kuwa watumishi
wema wa watu kwa sababu ya migogoro na migongano ya daima, inayojengwa katika ajenda
binafsi. Kutokana na migogoro na migongano hiyo, watumishi wengi tunakuwa wenye hasira
na "sura ndefu kazini", kiasi kwamba wakija watu kutaka huduma wanayostahili, wanaambulia
matusi, lugha korofi na huduma za kuparazaparaza. Kila mmoja ajitahidi sana kujenga
amani katika maeneo ya kazi, ili tuwezeshane kuwahudumia watu vizuri.
Utashangaa
muda mwingi wa kazi tunatumia kwa ajili ya vikao vya kusulihisha wafanyakazi wakarofi,
wavivu, wapiga majungu na wazushi. Katika hili kanuni ni mmoja, tukitaka kufanya kazi
vizuri, tutenganishe kati ya tabia zetu na wajibu. Tunapopaswa kutekeleza wajibu na
tufanye hivyo. Usilete tabia za nyumbani kwako au za ukoo wako mahali pa kazi. Utaleta
harufu mbaya mahali pa utumishi.
Kugubikwa na mitaala ya kishetani
Hili
ni jambo linaloitesa sana jamii yetu ya sasa. Wengi tumeingiliwa sana na mitaala ya
kishetani na imani kwa nguvu za giza. Hilo lipo kwa wote, wasomi na wasio wasomi.
Dhana kama hizo zikijengeka mahali pa kazi, watumishi tutashindwa hata kupeana mikono,
tutashindwa kuwahudumia watu vizuri. Na wapo wenye bahati mbaya kubwa zaidi, wale
ambao ni waamini haswa wa ushetani na wamemvaa na kumnywa shetani na tabia zake zote.
Matokeo yake wanakuwa na virusi vya vurugu kila wakati. Akija kazini tu, amani imetoweka,
wenzake hawasalimiani, vitu vinapoteapotea nk. Kumbe ni shetani ndiyo anafanya kazi
ndani mwake.
Shetani hakupi chochote zaidi ya kiburi, hofu, ukorofi na kila
aina ya uharibifu. Tufanye nini basi? Katika hili, tuimarishe imani yetu kwa Mungu,
tusimame imara katika imani yetu, tufanye kazi kwa jina la Mungu, kwa nguvu ya Mungu
na katika uwepo wake. Hapo kweli tutaweza kuwatumikia watu kama alivyotufundisha Yesu.
Mashindano, ubishi, kujiona bora kuliko wengine, hakuna tija kazini. Neno la Mungu
linatuimarisha likisema
Mwishoni mwa ainisho hili, kila mmoja ajiulize katika
Ukristo wake, ‘hayo unayoyatenda na hivyo unavyotenda, ni kwa mfano wa nani? Yanamtangaza
Kristo kweli?
Katika somo lilopita, na somo hili la leo, tunajaribu kujiweka
sawa maisha yetu ya kipasaka yaweje. Tumeona kwamba ili kweli tuwe watu wa Kipasaka,
waliotoka makaburini, wanajibudisha kutorudi tena makaburini, ni vema tuishi maisha
ya kiekaristi, maisha ya kujimenga na kujisadaka kwa ajili ya wengine, na maisha ya
utumishi mwema, utumishi mnyenyekevu kwa wengine. Ni kwa njia hiyo tu maisha yetu
mazima yatakuwa ni ukumbusho wa uwepo wa Yesu mwenyewe kati ya wanadamu.
Tunamwomba
Kristo Bwana aliyependa kuwa kielelezo kwetu, kielelezo cha Utumishi mnyenyekevu,
atupe nguu ya kupenda aliyopenda yeye, kutumikia alivotumikia yeye, ili mwisho wa
hija yetu, sote tukastahili kupata tuzo la mtumishi mwema na mwaminifu. Kutoka katika
Studio za Radio Vatican, ni mimi Padre Pambo Martin Mkorwe OSB.