Chama cha Kikatoliki cha Uamsho wa Roho Mtakatifu, kinamshukuru Baba Mtakatifu Francisko
kwa kuombea mradi wa Kituo cha Familia Kimataifa kilichoko mjini Nazareti wakati wa
Sala ya Malkia wa Mbingu, kwenye Uwanja wa Pango la Mtoto Yesu, Jumapili tarehe 25
Mei 2014 wakati wa hija yake ya kitume Nchi Takatifu. Baba Mtakatifu ameonesha nia
ya kutembele Nazareti mahali ilipoishi Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu panapo
majaliwa!
Kituo cha Familia Kimataifa kilianzishwa na Baraza la Kipapa la Familia
na kukikabidhi kwa Chama cha Kikatoliki cha Uamsho wa Roho Mtakatifu kukiendesha.
Mradi huu mkubwa utakapokamilika, unatarajiwa kuwa ni kituo cha majiundo ya tasaufi
ya familia; mahali ambapo familia mbali mbali zinazofanya hija Nchi Takatifu zinaweza
kupata malazi ya muda. Hapa waamini watapata majiundo makini na endelevu kuhusu tunu
msingi za maisha ya ndoa na familia.
Wafanyakazi katika utume wa ndoa na familia
wataweza kujinoa kwenye kituo cha Familia Kimataifa. Kwa ufupi, hapa ni mahali ambapo
Familia za Kikristo zitaandaliwa kwa ajili ya kushiriki kikamilifu katika mchakato
wa Uinjilishaji Mpya, kwa kutoa kipaumbele cha pekee kwa tunu msingi za maisha ya
kifamilia.
Kituo hiki cha Kimataifa kitatoa kozi maalum za ndoa na familia
kwa ajili ya waamini wanaoishi ndani na nje ya Nchi Takatifu, kwa kushirikiana na
Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Duniani pamoja na vyuo vikuu vya Kanisa Katoliki; lengo
ni kutoa huduma makini ya kiroho na kimwili kwa ajili ya familia. Kituo hiki kinatarajiwa
kuwa ni faraja kwa familia zinazokabiliana na hali ngumu ya maisha, kwa kutumia mfuko
maalum kwa ajili ya familia.