2014-05-25 12:17:59

Papa asali kwenye ukuta wa utengano!


Padre Federico Lombardi, msemaji mkuu wa Vatican ambaye yuko kwenye msafara wa Baba Mtakatifu Francisko Nchi Takatifu anasema kwamba, Papa Francisko alipomaliza kuzungumza na viongozi wakuu wa Serikali ya Palestina, mjini Bethlehemu, wakati akielekea kwenye Uwanja wa Pango la Mtoto Yesu kwa ajili ya kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu, ameshuka kwenye gari na kusali kwa kitambo kidogo kwenye ukuta unaotenganisha Bethlehemu na Israeli.

Baba Mtakatifu Francisko wakati wa chakula cha mchana kilichoandaliwa kwa ajili yake, wameshiriki pia Familia za wananchi wa Palestina pamoja na wakimbizi. Baada ya mapumziko mafupi, Baba Mtakatifu alikwenda kutembelea Kanisa kuu la kuzaliwa kwa Bwana mjini Bethlehemu.

Majira ya jioni, Baba Mtakatifu ametembelea Kituo cha "Phoenix Centre" kinachotoa huduma za kijamii ndani ya Kambi ya wakimbizi. Kituo hiki kilibahatika kutembelewa na Mtakatifu Yohane Paulo II kunako mwaka 2000. Ujenzi wa kituo hiki ni ufadhili wa Mtakatifu Yohane Paulo II na kilifunguliwa wakati wa Jubilee ya miaka 25 ya Utume wa Yohane Paulo II kama Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Baba Mtakatifu Francisko amepata fursa ya kuonana na kusalimiana na watoto wanaotunzwa kituoni hapo pamoja na kusali nao na baadaye, Baba Mtakatifu Francisko alihitimisha hija yake ya kichungaji nchini Palestina na kuagwa kuelekea Israeli ambako amepokelewa rasmi kwenye Uwanja wa Ndege wa Ben Gourion ulioko Tele Aviv. Amekagua gwaride la heshima pamoja na kutoa hotuba yake ya kwanza nchini Israeli.







All the contents on this site are copyrighted ©.