2014-05-25 10:55:12

Jimbo kuu la Dar es Salaam lazindua Mwaka wa Familia


Jumamosi ya tarehe 24 Mei 2014, umati wa waamini zaidi ya elfu kumi wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, walishiriki katika adhimisho la kufungua Mwaka wa Familia. Adhimisho hili lilifanyika katika Kituo cha Hija Pugu. Askofu Mkuu wa Jimbo kuu la Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo ndiye aliyeongoza adhimisho hili, akisaidiwa na maaskofu wasaidizi: Eusebius Nzigilwa na Titus Mdoe, pamoja na mapadri na mashemasi kadhaa. Tukio hili liliandaliwa na Umoja wa Wanaume Wakatoliki (UWAKA).

Katika homilia yake, Mwadhama alisisitiza umoja katika familia, kwani si baba au mama ama mtoto anayeweza kufanikisha malengo ya familia, isipokuwa ushirikiano wa wao wote. Usikivu kwa sauti ya Mungu na utii kwa sauti hii ndani ya familia ni kitu cha muhimu sana katika kukuza tunu za kifamilia. Wanafamilia walionywa juu ya mashindano ya kutaka kujinufaisha wenyewe, kwani ubinafsi ni sumu ya upendo wa familia.

Mwadhama, alimuweka mbele ya waamini Mtakatifu Yosefu ambaye ni msimamizi wa Jimbo, kuwa kioo cha familia zetu. Mt. Yosefu alikuwa msikivu na alijitoa kwa familia yake. Waamini walipewa changamoto, hasa akina baba, kama Mt. Yosefu angemkana mtoto Yesu, kuwa si wa kwake, Je, ukombozi wetu ungekuwa wapi? Vivyo, hivyo, kusiwe na maelekeo haya katika familia zetu, kukataa au kuwabagua baadhi ya watoto.

Mtakatifu huu, alifafanuliwa zaidi, kwa kuelezewa kuwa ni mtakatifu mkimya akuna mfano wake, hatusikii neno lolote toka mdomoni mwake. Lakini matendo yake yamewezesha ukombozi wa wanadamu wote kutimia. Katika maisha yake, hakuwa mbinafsi, hata alipofariki na kuwaacha Maria na Yesu, hakuwaacha katika hali ya masikitiko au kusambaratika kutokana na ubinafsi wake.

Mwadhama, aliwasihi waamini, si tu katika ngazi ya familia, lakini hata katika ngazi ya familia kuu ya jimbo, yale ambayo Familia Takatifu ya Nazarethi imetufundisha tuyaweke katika matendo yetu ya kila siku.

Adhimisho hili, lilifungamanishwa na matendo mbalimbali, kuwasha Mshumaa wa Familia, makundi na vyama mbalimbali vya kitume (wanawake, wanaume, vijana, wastaafu, watoto, Moyo Mtakatifu wa Yesu, Legio Maria na wanakwaya) waliweka maazimio ambayo watayaishi katika Mwaka huu, hasa kuwa tayari kubadilika na kushiriki katika uinjilishaji mpya.

Sala ya Mwaka wa Familia ilisaliwa na wanafamilia wote wa jimbo. Aidha, kulifanyika uzinduzi wa kitabu Mfahamu Mtakatifu Yosefu, ambacho kinamwelezea Mtakatifu huyu pamoja katika uhusiano aliokuwa nao na wanafamilia takatifu wa Nazarethi. Mwadhama alikipendekeza kitabu hicho, kiwe mwongozo kwa waamini katika Mwaka huu.

Matukio mengine ambayo yamepangwa ni uzinduzi wa Mwaka huu katika kila Parokia mwezi Juni. Aidha, kila familia itapana nafasi kutembelewa na wakleri ili kubarikiwa na kusimikwa kwa Msalaba na Biblia katika nyumba zao. Kardinali ameomba makundi matatu mengine yaandae adhimisho ambapo nao kama UWAKA walivyoandaa tukio hili na kuialika familia nzima, navyo vikundi hivyo vifanye hivyo hivyo. Makundi haya ni akina mama wakatoliki, watoto na wakreli katika Mwaka huu wa Familia.

Tukio hili, limekuwa ni mwendelezo mzuri wa Mwaka wa Imani, na waamini wengi baada ya adhimisho hili, wameonesha kufarijika kwao kwa Kanisa kuzijali na kutaka kuzijengea msingi imara familia zao.

Na Padre Stefano Kaombe,
Jimbo kuu la Dar es Salaam.








All the contents on this site are copyrighted ©.