Janga la upungufu wa madawati Tanzania livaliwe njuga!
Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda ameutaka uongozi wa mkoa wa Rukwa uhakikishe
unamaliza tatizo la upungufu wa madawati ili watoto wa shule za msingi wasiendelee
kukaa chini. Ametoa agizo hilo Jumamosi, usiku, Mei 24, 2014 wakati akizungumza na
viongozi na watendaji wa mkoa wa Rukwa mara baada ya kupokea taarifa ya Mkoa huo,
Ikulu ndogo, mjini Sumbawanga.
Waziri Mkuu amewasili mkoani Rukwa akitokea
Dodoma ambapo anamwakilisha Rais Jakaya Kikwete kwenye ibada ya kumuweka wakfu Askofu
Mteule Conrad Nguvumali wa Kanisa la Moravian Tanzania Jimbo la Rukwa inayofanyika
Jumapili, Mei 25, 2014, kwenye Uwanja wa Nelson Mandela, mjini Sumbawanga.
Akifafanua
kuhusu tatizo la madawati, Waziri Mkuu alisema: “Lazima mjipange kama mkoa ili muweze
kusaidia juhudi za Serikali kupunguza tatizo la madawati kwa watoto wetu wa shule
za msingi”. “Lazima mje na mpango maalum… mathalani kwenye Halmashauri zenu huko,
angalieni hizo mbao zinazokamatwa. Badala ya kuziuza, hizo mbao ziende kutengeneza
madawati na yakikamilika yaamuliwe kabisa haya yanakwenda shule fulani, na utaratibu
uendelee hadi shule zimalizike,” aliongeza.
Alisema utaratibu huo unaweza kumaliza
tatizo la upungufu wa madawati kwa uhakika zaidi kwani hata Halmashauri zinapoamua
kupiga mnada mbao zilizokamatwa, fedha inayopatikana huwa haiendi kutengeneza madawati.
Kwa
mujibu wa taarifa kutoka idara za elimu za mkoa wa Rukwa, Halmashauri tatu za wilaya
za mkoa huo ambazo ni Nkasi, Kalambo na Sumbawanga Vijijini zinakabiliwa na upungufu
wa madawati 33,799, wakati mahitaji ya madawati ni 62,118 na yaliyopo ni 28,319. Manispaa
ya Sumbawanga ilisema ina upungufu wa madawati 675 bila kutaja yaliyopo ni mangapi
wala mahitaji yake ni kiasi gani.
Akizindua Wiki ya Elimu Kitaifa mjini Dodoma
Mei 3, mwaka huu, Waziri Mkuu aliitaka Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI ambayo inasimamia
sekta ya elimu iandae utaratibu wa kuzibana Halmashauri ziwe za mjini au vijijini
kwani zote zina uwezo wa kupunguza tatizo hilo kulingana na fursa zilizonazo. “Nasisitiza
jambo hili liwe ni ajenda ya kudumu,” alisema Waziri Mkuu.
Mei 14, 2014, wakati
akifungua Mkutano Mkuu wa 30 wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT) jijini
Tanga, Waziri Mkuu aliwataka Mameya na Wenyeviti wa Halmashauri kuhakikisha wanamaliza
tatizo la madawati kwani nyenzo wanazo kupitia Halmashauri wanazoziongoza.
Mapema,
akiwasilisha taarifa ya Mkoa wa Rukwa, Mkuu wa Mkoa huo, Mhandisi Stella Manyanya
alisema mkoa huo kupitia kamati za shule na uongozi wa kata umeweka mkakati wa kutatua
tatizo la madawati kama njia mojawapo ya kuboresha taaluma katika mpango wa Matokeo
Makubwa na ya Haraka (BRN).
Akizungumzia kuhusu hali ya miundombinu katika
Mkoa huo, Eng. Manyanya alisema kazi za ujenzi wa barabara za mkoa huo kwa kiwango
cha lami unaendelea sasa baada ya msimu wa mvua kumalizika na baadhi ya wakandarasi
kupatiwa fedha na Serikali.
Kuhusu usanifu wa Daraja la Mto Momba lililoko
mpakani mwa mikoa ya Rukwa na Mbeya, Eng. Manyanya alimweleza Waziri Mkuu kwamba kazi
hiyo imesimama kutokana na kina cha maji kupanda licha ya kuwa ilipaswa kukamilika
tangu Machi mwaka huu.
“Usanifu ulitarajiwa kukamilika Machi 2014, lakini kutokana
na kina cha maji kupanda, uchunguzi wa matabaka ya udongo chini ya maji umeahirishwa
mpaka maji yatakapopungua,” alisema.
Hata hivyo, Mkuu huyo wa Mkoa alisema
wanatarajia kazi ya usanifu na uandaaji wa nyaraka za zabuni utakamilika mwezi Mei
mwishoni na baada ya hapo zabuni kwa ajili ya ujenzi wa daraja hilo itatangazwa.