Waandishi 70 wako kwenye msafara wa Papa Nchi Takatifu
Baba Mtakatifu Francisko wakati akiwa njiani kuelekea Amman nchini Yordan, amezungumza
na waandishi wa habari walioko kwenye msafara wake na kuwashukuru kwa kazi kubwa wanaoifanya
katika utekelezaji wa majukumu yao! Hija yake ya kitume imesheheni mambo mazito si
tu kwake kama mhusika mkuu hata pia kwa waandishi wa habari ambao wanafuatilia ziara
hii kwa ukaribu zaidi. Baba Mtakatifu anasema anawakumbuka katika sala zake.
Baba
Mtakatifu anasema, baada ya hija yake, ana wazo la kuzungumza na waandishi wa habari
watakaokuwa kwenye msafara wake. Padre Federico Lombardi msemaji mkuu wa Vatican anabainisha
kwamba, huu ni muujiza wa Papa Francisko kwani hata baada ya pilika pilika na ratiba
ngumu kiasi hiki bado atakuwa na nafasi ya kuzungumza na waandishi wa habari wakati
akirejea mjini Vatican.
Baba Mtakatifu amewashukuru waandishi wa habari 70
ambao wako kwenye msafara wake kwamba, anatambua ugumu wa hija hii, lakini ana amani
na utulivu mkubwa moyoni mwake!