2014-05-23 07:26:23

Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya 6 ya Kipindi cha Pasaka


Karibuni ndugu msikilizaji wa Radio Vatican katika kipindi cha Liturujia ya Neno la Mungu, tukiwa tayari Dominika VI ya Kipindi cha Pasaka, ambamo tunasikia na kuona Bwana mfufuka akihaidi zawadi ya Roho Mtakatifu. RealAudioMP3

Mpendwa mwana wa Mungu, katika somo la kwanza (Mdo, 8: 5-8, 14-17) tunakutana na Filipo ambaye yuko mji wa Samaria akihubiri habari njema huko. Katika mahubiri yake hayo au tuseme kazi zake za kichungaji atatenda ishara nyingi na mojawapo ya ishara hizi ni watu kunasuliwa toka pepo wachafu, waliopooza kuponywa na ishara nyingine kama hizo zilengazo kuleta uhuru katika maisha ya watu.

Kwa hakika watu walifurahi kama mwandishi anavyosema “ikawa furaha kuu katika mji ule”. Mitume waliposikia kuwa Samaria wamepokea Neno la Mungu waliwatuma Petro na Yohane ili wawawekee mikono kwa ajili ya kushukiwa na Roho Mtakatifu, maana walikuwa wamebatizwa tu kwa jina lake Bwana Yesu.

Mpendwa msikilizaji yafaa kuweka jambo hili katika mazingira yake; yaani tunatambua kwa njia ya historia yakuwa, kwa miaka 6 hivi baada ya kifo cha Yesu Kristu, hakukuwa na shughuli yoyote ya kueneza Neno la Mungu nje ya Yerusalemu. Ndiyo kusema Mitume na wafuasi wengine walikuwa wakipiga kazi yao palepale nyumbani. Ilikuwaje sasa wakaweza kutoka nje ya mji wao? Sababu mojawapo kuu ni mchanganyiko katika jumuiya yaani Wayunani na Waebrania.

Pole pole kukawepo madhulumu dhidi ya Wayunani ambao walionekana kuwa hatari kwa maana walikuwa na mawazo mapya tofauti na ya Waebrania na hivi wakaanza kutimuka na kuondoka Yerusalemu na kuelekea wengine Siria, wengine Antiokia, wengine sehemu nyingine za utawala wa Kirumi. Jambo hili lilipamba moto hasa wakati wa madhulumu ya Shemasi Stefano. Basi wale wote waliotimuka kila walipofika kwa ajili ya maficho walianza palepale kuhubiri habari njema. Ndiyo kusema tayari Kanisa si tena la Kiebrania bali kwa ajili ya Mataifa.

Mpendwa msikilizaji wa Neno la Mungu, katika kukimbia huko ndipo tunakutana na Filipo ambaye alikuwa Myunani kati ya wale mashemasi 7. Huyu alijikuta huko Samaria alikokimbilia kuepuka kuuawa kama Mt Stefano. Basi akijikuta huko alianza kuhubiri na kubatiza na mahubiri yake yalijaa Roho wa Mungu.

Kwa sababu ya kazi njema hiyo taarifa zilipelekwa Yerusalemu na kwa kuwa ni Yerusalemu ni Mama Kanisa, Mitume waliona ni vema waendeleze umoja kati ya Yerusalemu na Makanisa mapya na hivi walienda huko wakwawekea mikono wakristu wapya ili washukiwe na Roho Mtakatifu. Katika hili mtu aweza kuuliza hivi hawakuwa wamempokea Roho Mtakatifu? Tayari walikuwa naye lakini kwa kuwa katika Kanisa la mwanzo kushuka kwa Roho Mtakatifu Kuliambatana na ishara mbalimbali kama kunena kwa lugha, kutenda miujiza basi alama hizi zilikuwa bado kuchukua nafasi yake kwa Wasamaria mpaka walipokwenda Mitume.

Aidha katika hili Mungu apenda kusema kuwa, jumuiya mpya huzaliwa kwa utume wa Neno lakini haziwezi kukua pekepeke hata kama zimeanzishwa ni lazima daima zijifungamanishe na Jumuiya Mama. Lazima kuwepo na umoja kamili na unaoonekana katika jumuiya zote.

Katika Somo la pili (1Mt Petro 3:15-18) Mtakatifu Petro anawaalika watu kuwa tayari kushuhudia IMANI kwa upole na hofu kwa yeyote awaulizaye habari za tumaini lililo ndani yao. Daima kuweni na dhamiri njema ili uweza kushinda madhulumu yawajiayo pasipo haki. Ni vema kuteswa kwa sababu ya mapenzi ya Mungu kuliko kutenda mabaya. Mfano wa uvumilivu ni Kristu aliyeteswa pasipo dhambi ili awaokoe wenye kustahili kuteswa; lakini akahuishwa na Mungu.

Mpendwa mwana wa Mungu, tunajiuliza kwanini Mt Petro anakuja na mahubiri kama haya! Anatoa mahubiri haya kuwatia moyo wakristu kwa sababu ya madhulumu ambayo yalianza wakati huo ambayo kihistoria yatadumu kwa miaka 250 hivi baadaye. Anawaasa wakristu kujifungamanisha na Kristu Masiha asiyeweza kuwaacha katika taabu yao. Anataka pia kupenyeza ndani ya Wakristu hali na moyo wa utayari kujibu maswali yanayowajia wakiulizwa kwanini wanayo matumaini na kipi kinawasukuma kuwa na tumaini hilo?

Ili kuweza kujibu vema na kwa ufasaha maswali ya wasioamini lazima kuwa na imani thabiti yaani inayosimikwa katika moyo ikiangazwa na Kristu mwanga wa kweli. Ni lazima kuwa na sababu na vigezo kwanini unaamini! Na kwa namna hiyo basi utaweza kusuka majibu yako ya kiimani si kwa hekima yako bali hekima ya kimungu. Njia nyingine mwafaka ni maisha yako ya nje yanayoambatana na imani yako, kama yako sahihi ni majibu tosha kwa wasioamini.

Mpendwa msikilizaji, Mtakatifu Petro anasonga mbele na mahubiri yake akisema mkristu yampasa kuwa na lugha nyololo na tamu, yaani hapaswi kuwa na lugha chafu au ya matusi au tuseme lugha kali mbele ya awaye yote awe mtesi au awe anayetaka kujua juu ya imani yetu. Lugha ya mkristu hualika na kukaribisha awaye yote kwa furaha na utulivu.

Haya yote si mapya bali yametendwa na Bwana mwenyewe katika utume wake mpaka anapokata roho, lugha yake ni laini na ya msamaha kwa watesi wake. Mpendwa wanateologia wanaona sehemu hii ya barua ya Mtakatifu Petro kama ndio mwanzo wa Taalilim msingi inayotafuta kuhakikisha kwamba imani si kinyume na maisha yetu ya kawaida bali ni zawadi hakika ambayo mwanadamu aweza kuishi akimwelekea Mungu.

Katika Injili (Yn 14:15-21) tunakutana na Bwana akiweka wajibu wa kuzishika amri zake kama kipimo cha mapendo kwake. Kisha hilo anahaidi kumpeleka Roho Mtakatifu, Roho wa ukweli, mwalimu, na msaidizi wa kukaa nasi milele. Pamoja na ahadi hiyo anaona hatari iliyopo yakwamba ulimwengu haumpokei Roho Mtakatifu, lakini hata hivyo twampokea sisi maana akaa ndani yetu. Bwana anasonga mbele akisema hawezi kutuacha yatima bali aja kwetu, cha msingi ni kumpenda naye atatupenda na kujidhihirisha kwetu daima.

Mafundisho haya ni sehemu ya wosia wakati wa chakula cha jioni kabla ya kuteswa kwake. Mitume wamekwisha elewa kwamba Bwana ataondoka na hivi wanafadhaika. Bwana akijua hilo anawahaidi Roho Mtakatifu atakayekaa nao mpaka mwisho wa nyakati.

Mpendwa msikilizaji, Bwana anaweka sharti la kumpokea Roho Mtakatifu, sharti la upendo kwa Mungu. Sharti hili ni kuzishika amri za Mungu. Katika hili Bwana atatoa tahadhari akisema, Kwa kuwa ulimwengu hautaki kuzishika amri za Mungu basi hautaweza kumtambua kamwe Roho wa Mungu.

Ulimwengu anaoutaja Bwana unaweza kufikirika kama ni ulimwengu wa wasioamini, lakini ataka kumaanisha ile sehemu katika mioyo yetu ambayo bado imejifungamanisha na uovu, na hivi Roho wa Mungu hawezi kuingia hapo! Hivyo yafaa daima kukagua mioyo yetu kama kweli bado kuna sehemu kama hiyo. Kwa hakika namna ya kuona hilo ni pale tunaposhindwa kuwapenda ndugu zetu, ni pale tunaposhindwa kuwa mawakili wa ukweli katika maisha ya kila siku.

Mpendwa mwana Kanisa, Bwana anahaidi Roho msaidizi, Roho wa ukweli na mwalimu. Huyu ni kwa ajili ya kuwasaidia Mitume wakati wote wa utume wao na hasa wakati wa taabu. Ni Yule ambaye atawafanya wawe na furaha na tumaini katika maisha yao yote. Ndiyo kusema ni kinyume kukutana na mkristu asiye na furaha moyoni mwake wakati amempokea Roho wa Mungu, aliye Roho mfariji. Mitume na wakristu wa kwanza hawataogopa matisho toka nje au ndani ya jumuiya yao. Hawatakata tamaa hata wakitenda dhambi bali watasimama haraka na kuomba TOBA.

Kwa ujio wa Roho wa Mungu, Roho wa ukweli Kanisa linapata uhakika yakwamba Neno la Mungu kamwe halitaingiliwa na virusi na kupoteza uhalisia wake. Ndiyo kusema wakristu hata hivi leo watambue Neno na ukweli ni uleule tangu ulipopandwa na Kristu mwenyewe. Miaka 2000 zaidi ya ukristu yatosha kuhakikisha jambo hilo, yaani Kanisa limesafiri na wakati fulani kuyumbishwa toka ndani na nje lakini daima Habari njema na ukweli ni hakika.

Mpendwa msikilizaji wa Neno la Mungu Roho Mtakatifu hafanyi tu kazi ya kulikinga Kanisa, bali hata ile ya kuliongoza katika kuelekea au kutafuta ukweli. Roho Mt. huandaa moyo wa mtu aweze kupokea kwa uhuru kamili ufunuo wa Mungu. Roho Mtakatifu huongoza Kanisa linaposafiri kupitia nyakati mbalimbali, ili yale ambayo Bwana aliyasema kwa namna bila kuyafunua katika ukomo wake yaweze kueleweka na Mitume na hivi Kanisa linaweza kutambua kile alichotaka Bwana kwa wakati ule. Mpendwa mwana wa Mungu, kazi yako daima ni kumwomba Roho Mtakatifu akuangazie ili uweze kutambua ile kweli ya Bwana na hivi ukapate furaha ikupelekayo katika uzima wa milele.

Nakutakieni furaha tele katika Dominika hii ya VI ya Pasaka na Mungu azidi kuwa nawe, nawe ukitekeleza mapenzi yake na hivi ukiongozwa na Roho mwalimu, Roho wa ukweli na mfariji katika maisha yako yote. Tukutane tena Dominika ijayo, yaani katika siku-sikukuu ya KUPAA BWANA MBINGUNI. Tumsifu Yesu Kristu. Tafakari hii imeletwa kwako na Padre Richard Tiganya C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.