Ili wote wawe wamoja ndiyo kauli mbiu inayoongoza Hija ya kitume ya baba Mtakatifu
Francisko katika Nchi Takatifu kuanzia tarehe 24 hadi tarehe 26 Mei 2014, kama sehemu
ya Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 50 tangu Papa Paulo VI alipokutana na kusali pamoja
na Patriaki Anathegoras wa Yerusalemu, tarehe 5 Januari 1964.
Baba Mtakatifu
anatarajiwa kuondoka mjini Roma, Jumamosi, tarehe 24 Mei 2014 majira ya Saa 2:15 asubuhi
na kuwasili Amman, Yordani saa 7:00 mchana na baadaye yatafuatia mapokezi ya heshima
yatakayofanyika kwenye Jumba la Mfalme Al – Husseini majira ya Saa 7: 45. Baba Mtakatifu
anatarajiwa kukutana na kuzungumza na viongozi wa Serikali ya Yordani majira ya saa
8:20 na baadaye Saa 10: 00 anatarajiwa kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye uwanja
wa Kimataifa wa Amman. Jioni Baba Mtakatifu atatembelea kwenye eneo la Ubatizo wa
Yesu, Ng’ambo ya Mto Yordan. Baadaye atakutana na kuzungumza na wakimbizi, wahamiaji
na vijana walemavu.
Jumapili tarehe 25 Mei 2014, Baba Mtakatifu ataondoka kwa
Elkopta kuelekea Bethlehemu anako tarajiwa kuwasili majira ya saa 3:30 asubuhi na
kupokelewa Ikulu, atakapokutana na kuzungumza na Rais wa Palestina Bwana Abu Mazen
na baadaye atazungumza na viongozi wengine wa Palestina.
Majira ya saa 5:00
mchana, Baba Mtakatifu ataadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa la Pango
la Mtoto Yesu na kufuatiwa na Sala ya Malkia wa mbingu. Baba Mtakatifu atapata chakula
cha mchana na baadhi ya Famili za Kipalestina kwenye nyumba mpya ya Wafranciskani
iliyoko mjini Bethlehemu. Baadaye, Baba Mtakatifu anatarajiwa kufanya matembezi binafsi
kwenye Pango la Mtoto Yesu na baadaye kutembelea kambi ya wakimbizi ili kusalimiana
na watoto wanaohifadhiwa kambini hapo.
Baba Mtakatifu majira ya saa 10: 00
Jioni ataondoka kwa Elkopta kuelekea kwenye Uwanja wa ndege wa kimataifa Ben Gurion,
Tel Aviv na anatarajiwa kuwasili saa 10: 30 na kupokelewa na viongozi wa Serikali
ya Israeli. Majira ya Saa 11:15 jioni, Baba Mtakatifu ataondoka kwa Elkopta kuelekea
mjini Yerusalemu na hapo atakutana na kuzungumza kwa faragha na Patriaki Bartolomeo
wa kwanza na hapo kwa pamoja watatia mkwaju kwenye Tamko la Kiekumene.
Saa
1:00 za usiku, kutafanyika mkutano wa kiekumene kama kilele cha maadhimisho ya Jubilee
ya Miaka 50 tangu Papa Paulo VI alipokutana na Patriaki Anathegoras wa Yerusalemu.
Baba Mtakatifu na ujumbe wake watapata chakula cha usiku nyumbani kwa Patriaki Bartolomeo
wa kwanza pamoja na Maaskofu wa Kanisa Katoliki madhehebu ya Kilatini.
Baba
Mtakatifu Francisko ataianza siku yake ya tatu ya hija ya kichungaji, Jumatatu tarehe
26 Mei 2014 kwa kumtembelea Mufti mkuu wa Yerusalemu. Atapata fursa ya kutembelea
Eneo la Msikiti mkuu, na baadaye atakwenda kuweka shada la maua kwenye Ukuta ulioko
kwenye Mlima Herzl pamoja na kutembelea Jumba la Makumbusho la Yad Vashem. Saa 4:45
ratiba inaonesha kwamba, Baba Mtakatifu anatarajiwa kukutana na kuzungumza na viongozi
wakuu wa dini ya Kiislam na baadaye kukutana na Rais Shimon Peres majira ya Saa 5:45,
kwenye Ikulu ya Israeli.
Baadaye, Saa 7:00 mchana Baba Mtakatifu Francisko
anatarajiwa kukutana na kuzungumza na waziri mkuu wa Israel Bwana Benjamin Netanyahu
na baadaye, jioni atamtembelea tena Patriaki Bartolomeo wa kwanza. Akiwa kwenye Kanisa
la Getsemani, atakutana na Makleri, Watawa na Majandokasisi. Saa 11: 20 jioni Baba
Mtakatifu anatarajiwa kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu na viongozi wakuu wa Makanisa
ya Kikatoliki Nchi Takatifu. Baadaye ataondoka kwa Elkopta kuelekea mjini Tel Aviv
tayari kuagana na wenyeji wake wa Israeli na hivyo kuondoka kurejea tena mjini Vatican.
Kimsingi hii ndiyo ratiba elekezi ya hija ya kichungaji ya Baba Mtakatifu
Francisko kwenye Nchi Takatifu kuanzia tarehe 24 hadi tarehe 26 Mei 2014. Idhaa ya
Kiswahili ya Radio Vatican, itaendelea kukujuza yale yatakayojiri katika hija hii
ya sala na kiekumene.