2014-05-22 08:03:18

Vijana changamkieni maendeleo ya sayansi na teknolojia!


Patriaki Batholomeo wa kwanza hivi karibuni amewataka vijana wa kiorthodox kuachana na tabia ya kuwa na misimamo mikali ya kiimani na utaifa usiokuwa na tija wala mashiko na badala yake, wachangamkie kujifunza na kutumia maendeleo ya sayansi na teknolojia ya mawasiliano, ili kuweza kujifunza zaidi mambo msingi yanayotokea ulimwenguni. RealAudioMP3

Misimamo mikali ya kidini, kitaifa na kimataifa ni jambo ambalo linaendelea kupewa msukumo wa pekee huko Mashariki ya Kati, lakini ikumbukwe kwamba, limepitwa na wakati. Hii ni kutokana na ukweli kwamba, misimamo mikali ya kidini ni chanzo cha vita, vurugu, kinzani na maafa kwa watu wasiokuwa na hatia, kama hali inavyojionesha huko Mashariki ya Kati, mahali ambako Ukristo ulianza kuota mizizi yake katika mioyo na maisha ya watu, lakini leo hii wanalazimika kuzikimbia nchi zao kutokana na misimamo mikali ya kidini.

Patriaki Bartolomeo wa kwanza anawataka wananchi wanaoishi huko Mashariki ya Kati kujenga na kudumisha misingi ya maridhiano, haki, amani, upendo na mshikamano kwa ajili ya kutafuta maendeleo, ustawi na mafao ya wengi. Vijana wanapaswa kufahamishwa tatizo la kuwa na misimamo mikali ya kidini kwani wao mara nyingi wamekuwa wakitumiwa na baadhi ya wanasiasa au hata viongozi wa kidini kwa mafao yao binafsi.

Patriaki Bartlomeo ameyasema hayo kwenye Jukwaa la Vijana Kimataifa lililokamilika hivi karibuni. Anasema, leo hii kuna Wakristo ambao wanaishi katika hali ya wasi wasi kutokana na kuenea kwa vitendo vya kigaidi, madhulumu na nyanyaso za kidini. Jukwaa hili liliwashirikisha Mapadre na walei wanaojihusisha na majiundo kwa vijana katika Kanisa la Kiorthodox.

Lengo ni kuhakikisha kwamba, Kanisa la Kiorthodox linajitahidi kuwafunda vijana watakao kuwa ni Wakristo kweli kwa kuzingatia maadili na maisha ya Kikristo. Ndiyo maana kuna haja ya kuwa na viongozi wa maisha ya kiroho pamoja na kujifunza vizuri na kwa ufasaha matumizi ya mitandao ya kijamii, kwa ajili ya ustawi na maendeleo yao kiroho na kimwili.

Kanisa linatambua kwamba, kuna vitabu vingi vinavyoweza kuwapotosha vijana katika maisha yao, lakini Kanisa halina uwezo wa kuwazuia waandishi wa vitabu kufanya kazi zao. Jambo la msingi kwa vijana ni kuwa na dhamiri nyofu itakayowawezesha kupembua mema ya kufuata na mabaya ya kuachana nayo katika maisha yao. Kuna mambo machafu pia kwenye mitandao ya kijamii, lakini vijana wawajibike kimaadili na kiutu katika matumizi yake, kama kielelezo cha ukomavu wa maisha! Bila ukomavu, vijana wengi wataendelea kuwa ni watu wanaofuata mkumbo na matokeo yake wanapoteza dira na mwelekeo wa maisha.








All the contents on this site are copyrighted ©.