Vijana changamkieni maendeleo ya sayansi na teknolojia!
Patriaki Batholomeo wa kwanza hivi karibuni amewataka vijana wa kiorthodox kuachana
na tabia ya kuwa na misimamo mikali ya kiimani na utaifa usiokuwa na tija wala mashiko
na badala yake, wachangamkie kujifunza na kutumia maendeleo ya sayansi na teknolojia
ya mawasiliano, ili kuweza kujifunza zaidi mambo msingi yanayotokea ulimwenguni.
Misimamo mikali
ya kidini, kitaifa na kimataifa ni jambo ambalo linaendelea kupewa msukumo wa pekee
huko Mashariki ya Kati, lakini ikumbukwe kwamba, limepitwa na wakati. Hii ni kutokana
na ukweli kwamba, misimamo mikali ya kidini ni chanzo cha vita, vurugu, kinzani na
maafa kwa watu wasiokuwa na hatia, kama hali inavyojionesha huko Mashariki ya Kati,
mahali ambako Ukristo ulianza kuota mizizi yake katika mioyo na maisha ya watu, lakini
leo hii wanalazimika kuzikimbia nchi zao kutokana na misimamo mikali ya kidini.
Patriaki
Bartolomeo wa kwanza anawataka wananchi wanaoishi huko Mashariki ya Kati kujenga na
kudumisha misingi ya maridhiano, haki, amani, upendo na mshikamano kwa ajili ya kutafuta
maendeleo, ustawi na mafao ya wengi. Vijana wanapaswa kufahamishwa tatizo la kuwa
na misimamo mikali ya kidini kwani wao mara nyingi wamekuwa wakitumiwa na baadhi ya
wanasiasa au hata viongozi wa kidini kwa mafao yao binafsi.
Patriaki Bartlomeo
ameyasema hayo kwenye Jukwaa la Vijana Kimataifa lililokamilika hivi karibuni. Anasema,
leo hii kuna Wakristo ambao wanaishi katika hali ya wasi wasi kutokana na kuenea kwa
vitendo vya kigaidi, madhulumu na nyanyaso za kidini. Jukwaa hili liliwashirikisha
Mapadre na walei wanaojihusisha na majiundo kwa vijana katika Kanisa la Kiorthodox.
Lengo
ni kuhakikisha kwamba, Kanisa la Kiorthodox linajitahidi kuwafunda vijana watakao
kuwa ni Wakristo kweli kwa kuzingatia maadili na maisha ya Kikristo. Ndiyo maana kuna
haja ya kuwa na viongozi wa maisha ya kiroho pamoja na kujifunza vizuri na kwa ufasaha
matumizi ya mitandao ya kijamii, kwa ajili ya ustawi na maendeleo yao kiroho na kimwili.
Kanisa linatambua kwamba, kuna vitabu vingi vinavyoweza kuwapotosha vijana
katika maisha yao, lakini Kanisa halina uwezo wa kuwazuia waandishi wa vitabu kufanya
kazi zao. Jambo la msingi kwa vijana ni kuwa na dhamiri nyofu itakayowawezesha kupembua
mema ya kufuata na mabaya ya kuachana nayo katika maisha yao. Kuna mambo machafu pia
kwenye mitandao ya kijamii, lakini vijana wawajibike kimaadili na kiutu katika matumizi
yake, kama kielelezo cha ukomavu wa maisha! Bila ukomavu, vijana wengi wataendelea
kuwa ni watu wanaofuata mkumbo na matokeo yake wanapoteza dira na mwelekeo wa maisha.