Jiungeni na vyama vya kitume ili kuyatakatifuza malimwengu!
Askofu mstaafu Alfred Rotich wa jimbo la Kijeshi nchini Kenya, amewataka waamini kujiunga
na vyama vya kitume ndani ya Kanisa, ili kusaidia mchakato wa kuyatakatifuza malimwengu
kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao adili na matakatifu.
Kwa njia hii waamini
wataweza kuimarisha imani yao kwa Kristo na Kanisa lake kwa njia ya huduma makini.
Kwa waamini waliojiandikisha katika vyama mbali mbali vya kitume wanahamasishwa kuhakikisha
kuwa wanashiriki kikamilifu na wala si kuwa ni wanachama wa majina tu. Vyama vya kitume
ni kielelezo makini cha tafakari ya kina kuhusu Fumbo la Umwilisho na kwamba, kujiunga
na vyama vya kitume ni jambo la maana linalosaidia kuimarisha imani kwa Kristo na
Kanisa lake.
Waamini walei wasimame kidete kulinda na kutetea tunu msingi
za maisha ya Kikristo na utu wema na kwa njia hii watakuwa kweli ni chumvi na mwanga
wa dunia ambayo kwa sasa imegeuka kuwa kama tambara bovu! Askofu mtsaafu Rotich ameyasema
haya hivi karibuni wakati akizungumza kwenye Nyumba ya Watoto yatima inayomilikiwa
na kuendeshwa na Shirika la Masista Fukara kutoka Bergamo wanaotekeleza utume wao
Jimbo kuu la Nairobi.
Askofu Rotich amewapongeza Masista hawa kwa kujimega
bila ya kujibakiza kwa ajili ya kuwahudumia watoto yatima katika maisha, malezi na
makuzi yao! Shirika hili lilifika nchini Kenya kunako Mwaka 1998 na kuanzisha Jumuiya
yake ya kwanza, Jimbo kuu la Nairobi.