2014-05-21 10:41:50

Watoto wanaoishi katika mazinhira hatarishi wakatiwa bima ya afya!


Shirika la Wamissionari Wabenediktini wa Afrika katika Jimbo Katoliki la Mbeya kwa kushirikiana na Idara ya Caritas na maendeleo Jimbo Katoliki la Mbeya, katika kuonesha upendo na huruma ya kweli wamewasaidia misaada ya sare na vifaa vya shule, wanafunzi zaidi ya 50 katika shule mbalimbali jijini Mbeya.

Aidha wametoa wito kwa serikali, watanzania na wahisani wengine wenye mapenzi mema ndani na nje ya Nchi kuwasaidia watoto yatima na wanaoishi katika mazingira magumu mahitaji muhimu pamoja na kuwawezesha kiuchumi walezi wao ili waweze kuzingatia masomo na kuendelea vema kitaaluma.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti Bi .Margreth Mwashala ambaye ni msimamizi wa kitengo kinachojishughulisha na akina mama walea pekee (Single mother) kutoka Shirika la Caritas Mbeya anaelezea lengo la misaada hiyo kuwa ni kuwawezesha wanawake hao.

Kwa upande wake Brother Gasper Toke, OSB, kutoka Shirika la Kimisionari la Wabenediktini wa Afrika wanaofanya uchungaji wao Jimboni Mbeya amesema wameanza kutoa misaada hiyo kwa watoto 50 katika shule za msingi, Jijini Mbeya, ili kukabiliana na changamoto ya hali ngumu ya maisha inayoweza kuwatumbukiza tena katika umaskini mkubwa. Watoto hao wamekatiwa Bima ya Afya, ili waweze kuendelea na masomo yao bila wasi wasi.

Kwa upande wao wanafunzi waliopokea misaada hiyo Neema Immanuel na Kevin Chaula kwa niaba ya wenzao nao wamelishukuru shirika la Wabenediktini na Caritas Mbeya na kuiomba jamii iwaangalie kwa jicho la huruma ili waweze kuhitimu na kuendelea na masomo ya juu zaidi ili kuweza kujijengea uwezo wa kupambana na mazingira kwa siku za usoni.

Jumla ya watoto 50 kutoka katika shule za msingi Ikuti,Simike na Nsongi wamepatiwa misaada mbalimbali na shirika la kimisionari la wabenedikti wa waafrika kwa kushirikiana na Shirika la Caritas Mbeya kwa kuwakatia bima ya afya ikiwa ni mwendelezo wa misaada wanayoitoa ili kupunguza makali ya maisha kwa wazazi wao ambao ni walea pekee.

Na Thomson Mpanji,
Mbeya.








All the contents on this site are copyrighted ©.