2014-05-21 09:22:15

Utamu wa Neno la Mungu!


Kama sehemu ya maandalizi ya hija ya kitume ya Baba Mtakatifu Francisko katika nchi Takatifu inayoongozwa na kauli mbiu, ili wote wawe wamoja, Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican imekuwa ikikuletea tafakari ya sehemu muhimu za historia ya ukombozi wa mwanadamu. RealAudioMP3

Leo ndani ya nyumba, tunaye Padre Benno Michael Kikudo kutoka Jimbo kuu la Dar es Salaam anayewahamasisha Makleri pamoja na waamini kutembelea Nchi Takatifu kwani imesheheni utajiri mkubwa wa historia na imani ya Kanisa! Anasema kwa kutembelea Nchi Takatifu mwamini atapata fursa ya kufahamu Jiografia ya Nchi Takatifu na madhari yake, kikolezo muhimu sana katika kuyafahamu Maandiko Matakatifu.

Katika nchi Takatifu mwamini anapata fursa ya kugundua unyenyekevu wa Neno wa Mungu aliyefanyika mwili kwa ajili ya ukombozi wa mwanadamu, katika mambo yote akawa mwanadamu isipokuwa hakutenda dhambi. Katika nchi Takatifu waamini wanaweza kujionea mahali alipozaliwa, alipobatizwa, alipokulia, alipoteswa, kufa na kufufuka. Hapa mwamini anagusa ukuu wa Mungu unaojionesha katika maisha ya mwanadamu.

Hii ni historia ya Mwenyezi Mungu anayeshirikiana na binadamu katika kutekeleza historia ya ukombozi. Padre Benno Michael Kikudo ambaye ametembelea Israeli kwa zaidi ya mara moja anasema, kila wakati anapata changamoto ya kutaka kurudi tena kuweza kujitajirisha na maeneo yaliyobarikiwa na kutakatifuzwa kwa uwepo wa Yesu Kristo Mkombozi wa ulimwengu.

Kwa kuangalia maeneo ya kihistoria tangu wakati wa Agano la Kale hadi Agano Jipya utagundua kwamba, kweli Neno la Mungu li hai na kwamba, kuna haja ya kumfahamu kwa ukaribu zaidi Yesu Kristo, Jiwe kuu la pembeni!







All the contents on this site are copyrighted ©.