2014-05-21 16:08:01

Papa anasali kwa ajili ya China, Bosnia, Erzegovina na Serbia


Kwa mara nyingine tena, Baba Mtakatifu Francisko mara baada ya kuhitimisha Katekesi yake, ameelekeza fikira zake kwa wananchi wa Bosnia, Erzegovina na Serbia ambao wameathirika vibaya kutokana na mafuriko ambayo hadi sasa yamesababisha maafa makubwa kwa maisha ya watu na mali zao. Hali inaendelea kuwa mbaya zaidi!

Baba Mtakatifu anachukua fursa hii kuwaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kwanza kabisa kujiunga pamoja naye kwa njia ya sala, ili kuwaombea wote waliofikwa na majanga haya. Ni matumaini yake kwamba, Jumuiya ya Kimataifa itajitahidi kutoa msaada wa hali na mali kwa waathirika wa mafuriko haya.

Baba Mtakatifu Francisko anakumbusha kwamba, tarehe 24 Mei ni Kumbu kumbu ya Bikira Maria Msaada wa wakristo, Kanisa linasali kwa ajili ya kuiombea China na kwa namna ya pekee, waamini kutoka China watamiminika kwa wingi kwenye Madhabahu ya Bikira Maria wa Sheshan yaliyoko mjini Shangai kwa ajili ya kusali. Baba Mtakatifu anawaomba waamini wote kusali ili kwa njia ya maombezi na tunza ya Bikira Maria Msaada wa Wakristo, Waamini Katoliki nchini China waendelee kuamini, kupenda na kutumainia, wakijitahidi kudumisha maelewano mazuri na jirani zao.

Baba Mtakatifu anasema, Jumamosi Ijayo, tarehe 24 Mei 2014, Kanisa litawatangaza Watumishi wa Mungu: Padre Mario Vergara na Isidori Ngei Ko Lat, Mwamini mlei na Katekista waliouwawa kwa chuki za kidini huko Birmania kunako mwaka 1950. Ujasiri na uaminifu wao kwa Kristo na Kanisa lake viwatie shime Wamissionari lakini zaidi Makatekista ambao wanatekeleza utume wenye thamani kubwa katika maisha na utume wa Kanisa mahalia.







All the contents on this site are copyrighted ©.