2014-05-21 07:39:49

Biashara haramu ya binadamu ni hatari kubwa!


Mtandao wa Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume Duniani, "Talitha kum", umezindua kampeni dhidi ya biashara haramu ya binadamu inayoongozwa na kauli mbiu "Cheza kwa ajili ya maisha, pinga biashara haramu ya binadamu" wakati huu Jumuiya ya Kimataifa inapojiandaa kwa ajili ya kushuhudia mashindano ya Kombe la Mpira wa Miguu Duniani yatakayofanyika nchini Brazil kwa mwaka 2014. Biashara haramu ya binadamu inawadhalilisha watu zaidi ya millioni ishirini sehemu mbali mbali duniani. RealAudioMP3

Kardinali Joao Braz de Aviz katika hotuba yake ya ufunguzi amesema kwamba, watawa ni watu wanaotekeleza utume wao kati ya maskini na watu wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii. Kwa njia hii wanagusa kwa mikono mahangaiko na mateso ya mwanadamu hususan kwa wale wanaotumbukizwa katika biashara haramu ya binadamu, kielelezo cha utumwa mamboleo.

Baba Mtakatifu Francisko anasema kwamba, biashara haramu ya binadamu ni janga katika maisha ya binadamu dhidi ya upendo wa Mungu unaokoa na kumkirimia mwanadamu maisha mapya.

Ubalozi wa Marekani mjini Vatican unaunga mkono pia kampeni hii dhidi ya biashara haramu ya binadamu na kwamba, Serikali ya Marekani inashirikiana kwa karibu zaidi na Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani ili kuwatambua watu ambao wametumbukizwa katika biashara hii na hatimaye, kuwapatia msaada wa hali na mali ili kuweza kuanza tena upya maisha!

Shirikisho la Mashirika ya Watawa wa Kike Kimataifa linasema kwamba, katika utekelezaji wa utume wake, limekutana na watoto, wasichana na wanawake waliotumbukizwa kwenye biashara ya ngono na kuuzwa kama bidhaa sehemu mbali mbali za dunia.

Hii inatokana na ukweli kwamba, biashara haramu ya binadamu inaendelea kuwapatia faida kubwa wahusika. Takwimu zinaonesha kwamba, faida inayotokana na boashara hii haramu imefikia kiasi cha dolla za kimarekani billioni 32 na faida hii inazidi kuongezeka mwaka hadi mwaka, kiasi cha kuanza kuipita biashara haramu ya silaha pamoja na dawa za kulevya.

Mtandao wa Talitha Kum, ulianzishwa kunako mwaka 2009, hadi sasa unajumuisha wanachama wa Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume kutoka katika nchi 79. Kuna watawa 800 kutoka katika Mashirika 240 wanaojihusisha na kampeni dhidi ya biashara haramu ya binadamu. Biashara hii inawahusisha "watu wazito", kumbe kuna haja ya kushirikiana kwa dhati ili kuwapatia watu matumaini ya maisha mapya.

Mashindano ya Kombe la Mpira wa Miguu Duniani yaliyofanyika nchini Ujerumani na Afrika ya Kusini yaliwapatia watu wengi fursa za ajira. Vijana wengi wakachangamkia nafasio hizi kutoka vijijini kuelekea mijini wakitumaini kupata fursa za ajira, matokeo yake wengi wao wakajikuta wakitumbukizwa kwenye biashara haramu ya binadamu, utu na heshima yao vikaingia mchanga!

Kampeni dhidi ya biashara haramu ya binadamu inapania kupiga vita biashara ya ngono ya utalii wanayofanyishwa watoto na wasichana, kazi za suluba pamoja na biashara haramu ya viungo vya binadamu. Hapa utu na heshima ya binadamu viko hatarini kutokana na baadhi ya watu kupenda mali na utajiri wa haraka haraka, Brazil inaongoza katika biashara hii. Watu wengi wana matumaini ya maisha bora, lakini wanapaswa kuwa macho ili wasije wakatumbukizwa kwenye biashara haramu ya binadamu na hapo ndoto na matumaini yao, yatafifia na kutoweka kabisa! Biashara haramu ya binadamu si jambo la kuchezea!







All the contents on this site are copyrighted ©.