2014-05-20 06:51:40

Wafundeni vyema vijana wa kizazi kipya katika maadili!


Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Jumuiya ya Ulaya, CCEE, hivi karibuni limehitimisha mkutano wa wakurugenzi wa shughuli za kichungaji kwenye Vyuo vikuu Barani Ulaya, mkutano uliokuwa unajadili pamoja na mambo mengine kuhusu umuhimu wa Katekesi kwenye taasisi za elimu ya juu na vyuo vikuu Barani Ulaya, kwa kuongozwa na kauli mbiu “Nini maana ya kuishi kwa furaha?”. RealAudioMP3

Wajumbe wamepembua kwa kina na mapana maisha ya vijana wa kizazi kipya Barani Ulaya na kutoka sehemu nyingine za dunia. Hili ni kundi la vijana waliozaliwa nyakati za matandao, kiasi kwamba, ni vigumu kumwona kijana ambaye hana simu ya kiganjani.

Ni vijana wanaotumia muda wao mwingi kuogelea kwenye mitandao ya kijamii, kiasi kwamba, mahusiano ya vijana wengi yako kwenye mitandao ya kijamii, kiasi cha kufanya mahusiano ya kawaida kati ya watu kulega lega. Wazazi na wazee hapo awali ndio waliokuwa na jukumu la kuwafundisha na kuwafunda watoto wao, lakini leo hii mambo yamebadilika, vijana wamegeuka kuwa ni waalimu wa wazazi na wazee wao.

Ufahamu umevuka mipaka na wala si jambo la kupimwa na umri na mang’amuzi ya mtu, bali ni juhudi za mtu katika kutafuta masuala haya kwenye mitandao. Mwelekeo huu wa maisha umesababisha mabadiliko makubwa katika utambulisho wa maisha ya vijana ni watu ambao hawana tena rejea kwa wazazi na watu wazima wanaowazidi umri pamoja na kuwatangulia katika maisha.

Matokeo yake vijana wa kizazi kipya wanashindwa kuchukua maamuzi magumu katika maisha yao kwa mfano maisha ya ndoa na familia, kupata watoto ni mambo ambayo hayana kipaumbele cha pekee kwa sasa na matokeo yake vijana wengi wa kizazi kipya wanakosa uaminifu na udumifu katika mipango na mikakati ya maisha.

Wajumbe wanasema, kufanya kazi na vijana wa kizazi kipya kunataka moyo kwani ni kundi linalobadilika kwa mwendo wa kasi kubwa. Kumbe, ili kuwashirikisha vijana ile Furaha ya Injili inayobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake. Injili ina nguvu na uwezo wa kuleta mvuto na mshiko kwa vijana, ikiwa kama wataandaliwa barabara.

Vijana wajengewe uwezo wa kujisomea na kulitafakari Neno la Mungu, kwa kutambua kwamba, kwa kumwamini Mungu watakuwa na uhuru wa kweli. Vijana wasaidiwe kujisikia kuwa ni sehemu muhimu sana ya maisha na utume wa Kanisa na kwamba, walitafute Kanisa kwa kuhamasishwa na Kristo mwenyewe katika Maandiko Matakatifu.

Vijana wafundishwe kujisadaka kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake. Vijana wakifundishwa kutumia vyema mitandao ya kijamii, wanaweza kuwa ni Wainjilishaji wazuri kwa vijana wenzao katika mitandao ya kijamii. Imani ya Kanisa inaweza kutangazwa kwa kutumia maneno machache tu na kufikia umati mkubwa wa vijana. Ushuhuda na utakatifu wa maisha ni nyenzo msingi katika Uinjilishaji Mpya miongoni mwa vijana, hili ni jambo ambalo linapaswa kutilia mkazo na viongozi wanaojihusisha na utume wa vijana kwenye taasisi za elimu ya juu na vyuo vikuu.
Imeandaliwa na
Padre Richard A. Mjigwa. C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.