Kardinali Jean Louis Tauran, Rais wa Baraza la Kipapa la Majadiliano ya kidini katika
mahubiri yake kwenye Ibada ya Misa Takatifu kama sehemu ya maadhimisho ya Jubilee
ya miaka 50 tangu kuanzishwa kwa Baraza la Kipapa la majadiliano ya kidini hapo tarehe
19 Mei 2014 anasema kwamba, kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kudumisha majadiliano
ya kidini ili kujenga amani, umoja, upendo na mshikamano kati ya watu.
Kwa
sasa kuna mwelekeo mkubwa kwamba, vita, chokochoko na kinzani sehemu nyingi duniani
zinachukua mwelekeo wa kidini, jambo ambalo ni hatari kabisa kwa ustawi na maendeleo
ya watu!
Watu wengi anasema Kardinali Tauran wanamhubiri Mungu ambaye anajengeka
katika mawazo na muundo wa kibinadamu, kumbe kuna haja ya kuendelea kuhimiza kwamba,
binadamu ni viumbe wa mwenyezi Mungu na kwamba, watu wana amini kwa Mungu ambaye ni
Muumbaji anayeendelea kuzungumza na binadamu kwa njia ya matukio mbali mbali ya maisha,
ili kuonesha ukaribu wake kwa binadamu.
Kardinali Tauran anasema, Baraza la
Kipapa la majadiliano ya kidini ni mashahidi wa mchakato wa majadiliano unaofanywa
na Mama Kanisa kwa kutambua utajiri mkubwa wa tunu msingi za maisha ya kiroho zilizopatikana
katika kipindi cha miaka hamsini iliyopita. Ni jambo la muhimu kwa Wakristo kujiuliza
ikiwa kama majadiliano haya ya kidini yamewasaidia kukua na kukomaa katika maisha
yao ya kiroho.
Kardinali Tauran anasema Mtumishi wa Mungu Papa Paulo VI alianzisha
mchakato wa majadiliano ya kidini na walimwengu, Mtakatifu Yohane Paulo II akayakita
majadiliano katika amani kati ya watu; Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI akalielekeza
Kanisa kujadiliana na waamini wa dini mbali mbali kwa njia ya upendo katika ukweli
na kwa sasa Baba Mtakatifu Francisko analichangamotisha Kanisa kujielekeza zaidi katika
majadiliano ya urafiki unaojikita katika ujasiri, hekima, uvumilivu na udumifu kwa
kumtegemea Roho Mtakatifu.
Kardinali Tauran anasema, hata katika zile nyakati
ambazo mambo yalikuwa magumu kiasi kwamba, watu kukutana na kujadiliana ilikuwa ni
ndoto, lakini bado katika kipindi cha miaka hamsini kumekuwepo na matukio ambayo yameonesha
nia ya kutaka kujadiliana, kushirikiana pamoja na kutafuta muafaka kwa yale ambayo
yalikuwa yanawatatiza watu.
Baraza la Kipapa la majadiliano ya kidini limekuwa
ni msaada mkubwa kwa Makanisa mahalia kukutana na kujadiliana na waamini kutoka katika
dini mbali mbali. Baraza hili pia limechapisha hati mbali mbali zinazoweza kulisaidia
Kanisa katika mchakato wa majadiliano ya kidini. Ikumbukwe kwamba, majadiliano ya
kidini na Uinjilishaji ni chanda na pete kama ilivyo pia katika maisha na utume wa
Kanisa.
Padre Miguel Angelo Ayuso Guixot, Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la
majadiliano ya kidini amewashirikisha watu walioshiriki katika maadhimisho ya kumbu
kumbu ya miaka 50 tangu Baraza hili kuanzishwa mchango uliotolewa na Mababa wa Mtaguso
mkuu wa Pili wa Vatican katika kujenga na kukuza majadiliano ya kidini na waamini
wa dini mbali mbali duniani.
Anasema, hii ni sehemu ya mkakati wa ushuhuda
wa Injili ya Kristo unaomwilishwa katika matendo, kwa kuwasikiliza waamini wa dini
mbali mbali ili kwa pamoja waweze kuishi katika haki, amani, utulivu na udugu. Baraza
hili limepitia hatua mbali mbali katika uwepo wake kwa kipindi cha miaka hamsini iliyopita.
Viongozi wakuu wa Baraza la Kipapa la majadiliano ya kidini katika kipindi cha miaka
hamsini wamejikita katika kutembelea waamini wa dini mbali mbali na kufanya nao majadiliano
ya kidini; wameandika hati na nyaraka mbali mbali na kubadilishana mawazo.
Mtakatifu
Yohane Paulo II kwa mara tatu aliitisha mkutano wa viongozi wakuu wa kidini, ili kukusanyika
na kusali pamoja naye mjini Assisi. Kwa mara ya kwanza mkutano huu ulifanyika mwaka
1986, 1993 na mwaka 2002. Viongozi thelathini kutoka katika dini mbali mbali walihudhuria.
Tarehe 27 Oktoba 2011 Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI aliitisha mkutano huu wa
sala na kuhudhuriwa na wawakilishi wa dini mbali mbali 180.