2014-05-20 09:46:59

Jengeni utamaduni wa watu kukutana na kudumisha amani!


Baba Mtakatifu Francisko, Jumatatu tarehe 19 Mei 2014 amekutana na kuzungumza na Baraza la Maaskofu Katoliki Mexico kwa kuwataka kujenga na kudumisha utamaduni wa watu kukutana pamoja na kujenga amani. Ili Kanisa liweze kuendelea kuwajengea watu imani na matumaini, halina budi kushikamana na wahanga wa biashara haramu ya dawa za kulevya pamoja na maskini!

Baba Mtakatifu anasema, hakuna sababu ya Kanisa kuogopa au kutishwa na nguvu za giza, bali linapaswa kusimama kidete na kwa ujasiri pamoja na watu wanaoendelea kuteseka, kwa kutetea haki zao msingi pamoja na kushiriki katika mchakato wa kuwaletea maendeleo endelevu yanayomlenga mtu mzima: kiroho na kimwili. Mambo haya yanajikita katika mchakato wa Uinjilishaji pamoja na kutafuta mafao ya wengi.

Baba Mtakatifu anasema, Mexico kwa sasa imegubikwa na vitendo vya uhalifu wa kila aina unaowahusisha vijana, changamoto kwa Kanisa kuanzisha mchakato wa kutafuta na kudumisha misingi ya haki, amani na utulivu kati ya watu. Hapa kunahitajika utamaduni wa watu kukutana na kujadiliana kuhusu mustakabali wa nchi yao, ili kwa pamoja waweze kujikita katika ujenzi wa amani ya kudumu.

Baba Mtakatifu Francisko amegusia kwa namna ya pekee umuhimu wa waamini waleikushiriki katika maisha na utume wa Kanisa; umuhimu wa majiundo endelevu ya vijana pamoja na kuwa na mikakati makini inayolinda na kudumisha tunu msingi za maisha ya ndoa na familia. Waamini wanakumbushwa kwamba, Parokia ni muhimu sana katika ukuaji wa mtu kiroho na kimwili. Hapa pawe ni mahali pa maisha ya Kisakramenti na Sala, changamoto ya kujikita katika utume wa familia ili kudumisha Injili ya uhai dhidi ya utamaduni wa kifo.

Baba Mtakatifu anawaalika Makleri katika ujumla wao kutojizamisha katika malimwengu kwa kupenda anasa, mali na madaraka, bali daima wajifunze kwa maneno na matendo yao kuwa ni wafuasi amini wa Yesu Kristo. Maaskofu wawasaidie watawa kutekeleza dhamana yao katika maisha na utume wa Kanisa, kwa kujenga upendo mkalimifu. Wajitahidi kuhamasisha miito mitakatifu na kuitunza kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa.







All the contents on this site are copyrighted ©.