2014-05-19 11:59:10

Majadiliano ya kidini na kiekumene ni sehemu ya mchakato wa Uinjilishaji mpya


Baraza la Makanisa Ulimwenguni limeanzisha mkakati wa shughuli za kichungaji unaotaka kuunganisha majadiliano ya kiekumene pamoja na majadiliano ya kidini kama sehemu ya ushuhuda wa Uinjilishaji mpya unaopaswa kutekelezwa na wanachama wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni katika nchi husika.

Ikumbukwe kwamba, majadiliano ya kiekumene yanajikita kwa namna ya pekee na Wakristo wa Makanisa mbali mbali wakati ambapo majadiliano ya kidini yanawahusisha waamini wa dini mbali mbali duniani.

Haya ni maamuzi yaliyofikiwa hivi karibuni kwenye mkutano wa Tume ya Imani ya Baraza la Makanisa Ulimwenguni katika mkutano wake uliofanyika hivi karibuni nchini Uswiss. Wajumbe wameangalia uhusiano, utofauti na malengo yaliyomo katika mchakato wa majadiliano ya kiekumene na kidini yanayotekelezwa na Baraza la Makanisa Ulimwenguni.

Wadau wakuu katika majadiliano, watajengewa uwezo kwa njia ya semina na vitini mbali mbali ili kusaidia mchakato wa majadiliano ya kiekumene na kidini katika Makanisa mahalia. Mkutano huu uliwashirikisha wajumbe kutoka sehemu mbali mbali za dunia.

Kwa mara ya kwanza katika mikakati yake ya kichungaji, Baraza la Makanisa Ulimwenguni linaonesha nia ya kuanza kwa kasi kubwa zaidi majadiliano ya kidini, ili kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani na utulivu kati ya watu, kwa kuheshimu uhuru wa kuabudu kama ilivyokaziwa wakati wa maadhimisho ya mkutano mkuu wa kumi wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni uliofanyika mwaka 2013 huko Korea ya Kusini.








All the contents on this site are copyrighted ©.