Askofu Bernadin Mfumbusa wa Jimbo Katoliki Kondoa ambaye pia ni msimamizi wa kitume
wa Jimbo Katoliki Dodoma amewataka watawa kuonesha ushuhuda wa mashauri ya Kiinjili
kwa kujikita katika ufukara, utii na usafi kamili kama kielelezo makini cha majitoleo
yao kwa Mungu na jirani katika maisha ya kuwekwa wakfu ndani ya Kanisa.
Watawa
wanapaswa kujenga moyo wa usikivu na utii kwa viongozi wao halali, kwa kusali na kutafakari
Neno la Mungu linalowawezesha kuisikia sauti ya Mungu ikizungumza kutoka katika undani
wa maisha yao! Watambue kwamba, wanaitwa na kutumwa na Kanisa kuwahudumia watu katika
medani mbali mbali za maisha, hata kama wakifanya kazi Serikalini wanapaswa kuwa kweli
ni mfano bora wa kuigwa na wafanyakazi wengine!
Askofu Mfumbusa ameyasema hayo
hivi karibuni wakati wa maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa kuu la
Mtakatifu Paulo wa Msalaba Jimbo Katoliki la Dodoma ambapo watawa wanne wa Shirika
la Masista wa Mtakatifu Gemma Galgan waliweka nadhiri zao za daima. Watawa wa Mtakatifu
Gemma Galgan na waamini kwa ujumla wao, wanapaswa kujifunza na kuiga maisha ya Mtakatifu
Gemma Galgan ambaye ameacha urithi mkubwa katika maisha na utume wa Kanisa.
Kwa
upande wake, Askofu mstaafu Joseph Mathias Isuja wa Jimbo Katoliki Dodoma amewataka
watawa kuthamini wito, maisha na utume wao kwa ajili ya Mungu na Kanisa, daima wakijitahidi
kujenga na kudumisha fadhila ya uvumilivu, imani, mapendo na matumaini kwa Kristo
na Kanisa lake. Watawa wajifunze kuwa ni watu wa sala na Ibada ya kuabudu Ekaristi
Takatifu kama alivyofanya Mtakatifu Gemma Galgan.
Katika shida na magumu ya
maisha, wajitahidi kuyaunganisha na Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika
wafu, kwani huyu ndiye dira na mwongozo wao wa maisha ndani ya Kanisa. Watawa wajenge
na kudumisha moyo wa kimissionari na kitume, tayari kujisadaka kwa ajili ya ustawi
na maendeleo ya Kanisa mahalia!