Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya baada ya mkutano wake wa kawaida wa mwaka uliokuwa
unafanyika kwenye Seminari kuu ya Mtakatifu Thoma wa Akwino, Nairobi wametoa tamko
linalozungumzia kuhusu kuibuka kwa utamaduni wa kifo nchini Kenya, rushwa na ufisadi
pamoja na vita Sudan ya Kusini.
Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya likizungumzia
kuhusu utamaduni wa kifo unaoendelea kushika kasi nchini humo linabainisha kwamba
wananchi wengi wanaendelea kupoteza maisha kutokana na mashambulizi ya kigaidi, ajali
barabarani, ujambazi, wizi, tabia ya watu kujinyonga kwa kujikatia tamaa, baa la njaa
na ulevi wa kupindukia. Hii inatokana na ukweli kwamba, kumekuwepo na silaha za moto
zilizozagaa miongoni mwa wananchi wa Kenya, kiasi kwamba, leo Kenya imekuwa ni uwanja
wa vitendo vya kigaidi, vinavyoendelea kuwajengea wananchi hofu kubwa.
Baraza
la Maaskofu Katoliki Kenya linaikumbusha Serikali wajibu wake msingi wa kulinda usalama
wa raia na mali zao pamoja na wananchi kuonesha ushirikiano wa dhati na vyom bo vya
ulinzi na usalama kwani usalama wa nchi uko mikononi mwa raia wenyewe. Ulinzi na usalama
vipewe msukumo wa pekee kwani hata askari wenyewe maisha yao yako hatarini, lakini
hata hivyo watekeleze wajibu na dhamana yao kwa kuzingatia utawala wa sheria.
Baraza
la Maaskofu Katoliki Kenya linasema kwamba, rushwa na ufisadi wa mali ya umma kwa
sasa ni saratani inayotisha nchini Kenya kutokana na ubinafsi wa kutisha unooneshwa
na baadhi ya viongozi na wafanyakazi wa Serikali. Kumekuwepo na tabia ya ukabila inayoendelea
kupandikizwa miongoni mwa wananchi wa Kenya, jambo ambalo ni hatari kwa usalama na
maendeleo ya nchi pamoja na vitisho vya mara kwa mara.
Maaskofu wanasema hakutakuwepo
na utawala bora, ikiwa kama watu watashindwa kujenga na kudumisha utamaduni wa kuvumiliana
na kuheshimiana badala yake wanajikita katika masuala ya kutishiana maisha. Serikali
iwe makini na matumizi ya fedha ya umma na kwamba, rushwa na ufisadi ni masuala yanayopaswa
kukomeshwa kwa nguvu zote, vinginevyo, wananchi wa Kenya wataendelea kunyonywa!
Rushwa
katika Jeshi la Polisi ni chanzo kikuu cha ajali barabarani, changamoto ya kuondokana
na vitendo hivi vinavyodhohofisha kanuni na misingi ya utawala bora na badala yake
wajikite katika huduma makini kwa ajili ya wananchi wa Kenya. Ni wajibu wa Serikali
kukomesha mahusiano yaliyoko kati ya rushwa, biashara haramu ya silaha na wakimbizi;
pia kuna uhusiano mkubwa kati ya ongezeko la hali ya umaskini, ukosefu wa fursa za
ajira pamoja na ongezeko la vitendo vya wizi na ujambazi nchini Kenya.
Baraza
la Maaskofu Katoliki Kenya katika tamko lake kwa vyombo vya habari linasema kwamba,
maskini ndio wanaobebeshwa mzigo wa ukosefu wa amani na utulivu. Vita inayoendelea
Kusini mwa Sudan ni jambo linalokera sana na kwamba, Bara la Afrika haliwezi kuyafumbia
macho mateso na mahangaiko ya wananchi wa Sudan ya Kusini! Raia wengi wasiokuwa na
hatia wamepoteza maisha yao na wengine wengi wanaendelea kukimbia makazi yao kwa kuhofia
usalama wa maisha na mali zao.
Bara la Afrika bado lina kumbu kumbu ya mauaji
ya kimbari yaliyofanyika nchini Rwanda, miaka ishirini iliyopita! Maaskofu wanasema,
wasingelipenda kuona maafa haya yanatendeka tena Barani Afrika. Baraza la Maaskofu
linachukua fursa hii kuonesha mshikamano wake wa dhati na wananchi wa Sudan ya Kusini
katika kipindi hiki kigumu katika historia ya nchi yao.
Kanisa Katoliki nchini
Sudan ya Kusini limewekeza sana katika mchakato wa maendeleo endelevu nchini humo.
Maaskofu wanaiomba Jumuiya ya Kimataifa kusaidia harakati za kuwapatanisha wahusika
wakuu katika vita Sudan ya Kusini, ili amani iweze kutawala pamoja na kuokoa maisha
ya watu wasiokuwa na hatia!