2014-05-16 09:29:27

Imani na vita ni mambo ambayo hayawezi kupikika chungu kimoja!


Kardinali Jean Louis Tauran, Rais wa Baraza la Kipapa la majadiliano ya kidini katika safari yake ya kikazi nchini Yordan iliyomwezesha kuzungumza na viongozi mbali mbali wa kidini nchini humo amesema kwamba, imani na vita ni mambo mawili ambayo yanasigana sana na kamwe hayawezi kupikika chungu kimoja! Hakuna mtu yeyote anayeweza kuhalalisha vita ya kidini, dhana ambayo imetawala sana huko Mashariki ya Kati, jambo linalosababisha maafa makubwa kwa watu na mali zao!

Dhana ya vita ya kidini inajengeka katika ujinga wa watu kutofahamiana vyema pamoja na kuendekeza mawazo potofu kuhusu mambo ya dini na imani. Dini zinapaswa kuwa ni chombo kikuu cha kusaidia kuleta amani, upendo na mshikamano kati ya watu na wala si chanzo cha vita, kinzani na migogoro ya kijamii.

Kardinali Tauran anasema, wananchi wa mji wa Amman wanaendelea kujiandaa vyema kwa ajili ya kumpokea Baba Mtakatifu Francisko wakati wa hija yake ya kiekumene huko Mashariki ya Kati. Waamini na watu wenye mapenzi mema, wanaendelea kusali na kumwombea Baba Mtakatifu Francisko katika hija yake ya kitume, ili waweze kumwonjesha ukarimu na upendo, watu wana shauku kubwa ya kuonana na Baba Mtakatifu Francisko.

Kardinali Tauran alikuwa mjini Amman kuanzia tarehe 13 hadi tarehe 14 Mei 2014, kama sehemu ya maandalizi ya hija ya kiekumene ya Baba Mtakatifu Francisko Nchi Takatifu ambako pia alipata nafasi ya kuweza kujadiliana na viongozi mbali mbali wa kidini kuhusu changamoto zinazojitokeza katika sekta ya elimu huko Mashariki ya Kati. Waamini na watu wenye mapenzi mema wanamwona Baba Mtakatifu Francisko kuwa ni alama ya matumaini kwa wananchi walioko Mashariki ya Kati.







All the contents on this site are copyrighted ©.