2014-05-15 07:00:52

Ubatizo Mto Yordani!


Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican inaendelea kukuletea tafakari kuhusu maeneo matakatifu yatakatotembelewa na Baba Mtakatifu Francisko wakati wa hija yake ya kitume na kiekumene huko Nchi Takatifu kuanzia tarehe 24 hadi tarehe 26 Mei 2014. Leo tuko Yordani.
Baada ya kuzaliwa, kukimbilia Misri na kurudi toka huko, Yesu akaenda na wazazi wake kukaa Galilaya (nyumbani kwake) kwa miaka hii 33. Kabla ya kuanza utume rasmi Yesu anaenda Yordani kubatizwa na Yohane. Baada ya kubatizwa anaenda Kafarnaum na huko ndiko anaanza kazi ya kuhubiri. RealAudioMP3

Ebu tuangalie pahali hapa alipobatizwa Yesu. Kwa kawaida, Yohane mbatizaji alikuwa upande wa mashariki, ng’ambo ya mto Yordani (Galilaya ya Upagani). Huko akawabatiza watu na kuwataka wauvuke tena mto Yordani na kuingia Magharibi yaani nchi ya ahadi. Akawasadikisha watu kwamba sehemu hiyo ya ubatizo ilikuwa ni sehemu halisi ambayo Musa angewaingiza watu katika nchi ya ahadi, walipofika toka utumwani Misri.

Kwa hiyo, wale wote waliojidhani kwamba wameingia nchi ya ahadi kumbe walikuwa bado hawajakuingia kidhati. Kwa hiyo, Yohane akawaita watu toka Yudea warudi tena ng’ambo ya Yordani ili wabatizwe upya, na kuingia nchi ya ahadi kama ilivyokuwa walipotoka Misri. Watu wakafika pahala hapo palipokuwa panaitwa kwa kiyahudi Bethabàra maana yake ni mahali pa kukatisha, pahala pa kusimama na kuangalia kwa mbali au nyumba ya Bwana.

Yaonekana kwamba, mahali hapa alisimama Musa juu ya mlima Nebo na kutafakari nchi ya ahadi na kuona ni mahali gani ambapo angewaingiza Wayahudi katika nchi ya ahadi. Kwa bahati mbaya yeye mwenyewe hakuingia, badala yake Yoshua ndiye aliyeliingiza taifa katika nchi ya ahadi.

Bethbara iko karibu sana na Ziwa la mauti. Yesu anavuka mto na kuingia nchi Takatifu kuanza kufanya kazi ya kuhubiri na hatimaye kwenda kuteswa na kufa na kufufuka. Maelezo ya kitaalilimungu ya mahali hapa, ni kwamba yabidi kujiruhusu kuongozwa na Yesu toka nchi ya utumwa wa dhambi na kuingia katika nchi ya uhuru kamili wa kiroho.

Kabla ya kubatizwa, Yesu alibadilishana kauli kidogo na Yohane aliyekuwa anakataa. Kwa hoja kwamba kumbatiza huko kungeonesha kuwa Yesu ni mdhambi aliye mbali na Mungu. Yesu anasema: “Kubali hivi sasa, kwa kuwa ndivyo itupasavyo kuitimiza haki yote.” Hapa Yesu anataka kumwambia Yohane kuwa anayo picha tofauti ya haki yaani, haki anayoijua Yohane ni tofauti na haki ile ya Yesu. Haki ya Mungu anayotaka kuiingiza Yesu duniani ni ile inayowakomboa na kuwapenda watu wote.

Yohane anakubali na kumfanya Yesu avuke mto kwenda nchi ya ahadi yaani nchi ya uhuru. Kuingia huko kwa Yesu katika nchi ya Ahadi (Galilaya) ni kama kule kwa kutoka Misri alikokimbili. Sasa inaamana ya kuingia tena katika nchi ya Misri ya maisha yetu, yaani nchi ya utumwa wakaao Farao wanaotukandamiza na kunuonea. Sasa mkombozi anatujia na kutukomboa. Yesu ni Musa mpya.

Siku ile ya ubatizo wa Yesu pale Yordani kuna vituko vitatu vinavyoweza kutufundisha. Mosi, tunaambiwa kwamba mara tu baada ya kubatizwa, Yesu anapotoka majini anga linafunguka. Maelezo yake ni ya kihistoria ya mahusiano ya Mungu na binadamu. Kwamba, hapo mwanzo karibu katika karne kama tatu hivi, Mungu alikuwa anaongea na watu kwa njia ya manabii aliokuwa anawatuma kwao. Baadaye, akaacha kutuma manabii kwa sababu watu hawakuwa tena wanawasikiliza. Mungu akafunga mbingu zake zilizokuwa saba. Watu wakabaki wanateseka, wakalalamika kwamba hatuna tena nabii, itakuwaje, tutatambuaje mawazo ya Mungu kama hakuna nabii?

Unaona sasa kwa mara nyingine Yesu anapoibuka toka majini, anga linafunguka. Milango ya mbingu zote saba inafunguka.“Bwana ulikuwa na haki ya kutukasirikia, maana tulitenda dhambi; Lakini sasa, Ee Bwana, wewe u baba yetu; sisi tu udongo, nawe u mfinyanzi wetu, sisi sote ni kazi ya mikono yako. Ukifungua mbingu tutaokoka”. (Isaya 64). Kwa ujio wa Yesu, hatuhitaji tena nabii kwani tunaye Mungu hapahapa “Emmanueli”.

Pili, tunasikia kwamba Roho ya Mungu akamshukia Yesu kama njiwa. Njiwa huyo anatukumbusha Agano la Kale, baada ya tufani kuu, alitumwa njiwa kuangalia gharika kuu, baadaye anarudi akiwa na tawi la mzeituni mdomoni. Njiwa ni alama ya wema, uzuri, unyofu. Ndivyo Yesu anavyofika. Baada ya Tufani, Mungu anasema, sitaharibu tena nchi. Hakutakuwa tena tufani itakayoharibu nchi, bali atatuma roho aliye alama ya uzima mpya. Ndivyo sasa Yesu anapoibuka toka majini roho anaingia duniani.

Tatu, sauti ikasikika toka mbinguni. Sauti inayomtambua Yesu. Sauti inatambua kitendo kinachofanyika. Yaani ufunuo au epifania ya Mungu. Sasa ni wakati rasmi Mungu anapoanza shughuli yake mpya. Kwa hiyo anapoibuka toka majini, Mungu anatamtambua kuwa ndiye mwanae mpenzi. Mwana anafanana na wazazi wake katika sifa na thamani zote muhimu, hata namna ya kuongea na kutenda mambo. Sisi tumwangalie mwanae anayefanana na Mungu, nasi tutakuwa na roho hiyohiyo kwani tunafanana na Baba. Wote ni watoto wa Mungu, Yeye ni mwanae wa pekee mpendwa kwani ameleta habari njema ya upendo, na ya haki kwa watu wote.

Tujikubali kwamba tuko katika nchi ya utumwa mwa dhambi, tugeuke kwa kuvuka Yordani pamoja na Yesu, tutaibuka na roho wa Bwana, aliye roho wa unyenyekevu, upole, wema, upendo na haki. Roho atakayetupa nguvu ya kushinda majaribu ya maisha magumu ya humu jangwani (ulimwenguni). Kisha tutaibuka kidedea katika maisha mapya pamoja na Kristu Mfufuka.

Yesu anatuagiza kutenda mambo yote kwa kufuata mfano wa maisha yake. Ndivyo alivyowaagiza mitume wake siku ya karamu ya mwisho, “fanyeni hivi kwa kunikumbuka mimi.” Sasa twende tukakiangalie chumba ambacho Yesu alifanya sherehe mara ya mwisho hapa duniani na kuyatamka maneno hayo.
Tafakari hii imeandaliwa na
Padre Alcuin Nyirenda, OSB.








All the contents on this site are copyrighted ©.