2014-05-15 08:57:31

Tamko la pamoja ili kujenga mshikamano wa kimataifa!


Kardinali Jean Louis Tauran, Rais wa Baraza la Kipapa la Majadiliano ya kidini pamoja na Mfalme El Hassan bin Talal kutoka Amman Yordan, katika mazungumzo yao yaliyofanyika kuanzia tarehe 13 hadi tarehe 14 Mei 2014, kuzungumzia kuhusu changamoto katika elimu, wakati huu wananchi wa Yordan wanapoendelea kujiandaa kwa ajili ya hija ya kichungaji ya Baba Mtakatifu Francisko, kama cheche ya matumaini kwa wananchi wanaoishi huko Mashariki ya Kati, wametoa tamko la pamoja kama njia ya kujenga na kudumisha mshikamano duniani.

Katika sala zao wamewakumbuka wasichana waliotekwa nyara na kikundi cha kigaidi cha Boko Haram, Kaskazini mwa Nigeria na kutaka waachiliwe mara moja, ili waweze kujiunga tena na familia zao. Wameitaka Jumuiya ya Kimataifa kujikita katika mchakato wa majadiliano katika ukweli na uwazi ili kudumisha amani katika maeneo ambayo bado yanakabiliwa na vita pamoja kinzani za kijamii.

Viongozi hawa kwa pamoja wamekubaliana kimsingi kwamba, familia na shule ni mahali ambapo watoto wanarithishwa elimu, maadili na tunu msingi za maisha ya kiroho na kijamii. Kumbe, kuna haja kwa watoto kuelimishwa kuhusu utu na heshima ya binadamu; umuhimu wa kuzingatia haki msingi hususan uhuru wa kuabudu pamoja na kujikita katika kulinda na kudumisha misingi ya haki, amani, umoja na mshikamano kwa kupambana na: ujinga, umaskini pamoja na mmong'onyoko wa maadili na utu wema.

Jamii zijitahidi kujenga mchakato wa upatanisho pale ambako kumekuwepo na vita, migogoro na kinzani za kijamii, ili amani ya kweli iweze kupatikana na kuendelezwa. Viongozi hawa wanatambua kwamba, mustakabali wa mwanadamu na maendeleo yake uko mikononi mwa vijana wa kizazi kipya wanaopaswa kukuza kipaji cha udadisi na ujasiri ili kuondokana na woga; kujenga na kudumisha moyo wa unyenyekevu badala ya majivuno na kiburi; ni wajibu wa vijana kudumisha ukomavu na uhuru kwa kujiaminisha katika uwezo wa kufikiri pamoja na kujitahidi kuwa wakweli kwa kutambua kwamba, tofauti zilizopo ni utajiri mkubwa kati ya watu!.







All the contents on this site are copyrighted ©.