Biashara haramu ya silaha na watu kulazimika kuzikimbia nchi zao ni mambo yanayohatarisha
amani na utulivu!
Baba Mtakatifu Francisko, Alhamisi, tarehe 15 Mei 2014 amepokea hati za utambulisho
kutoka kwa Mabalozi wapya wa Uswiss, Liberia, Ethiopia, Sudan, Jamaica, Afrika ya
Kusini na India, wanaoziwakilisha nchi zao mjini Vatican. Baba Mtakatifu amewapongeza
na kuwashukuru wakuu wa nchi kwa maamuzi yao na kwamba, anawakumbuka na kuwaombea
amani na ustawi kwa nchi zao!
Baba Mtakatifu katika hotuba yake amekazia kwa
namna ya pekee amani ambayo haina budi kufanyiwa kazi na wanadiplomasia, ili kuiwezesha
familia ya binadamu kukuwa na kustawi katika haki, changamoto ya kujibidisha zaidi
na zaidi kwani amani ni kati ya mambo ambayo Jumuiya ya Kimataifa haijawahi kuifikia,
kumbe kuna haja ya kuendelea kuitafuta pamoja na kukabiliana na changamoto mbali mbali
zinazokinzana na amani.
Baba Mtakatifu anasema, amani na utulivu haviwezi kupatikana
ikiwa kama Jumuiya ya Kimataifa itashindwa kudhibiti biashara ya silaha duniani pamoja
na uhamiaji wa lazima. Biashara haramu ya silaha duniani inakwamisha juhudi za kutafuta
amani na usalama kati ya watu. Vatican kwa upande wake, itaendelea kuihamasisha Jumuiya
ya Kimataifa kutafuta na kudumisha amani, kwa kufanya maamuzi mazito ili kukomesha
kuenea kwa biashara ya silaha duniani.
Baba Mtakatifu anasema, maafa ya watu
wanaolazimika kuzikimbia nchi zao ni kati ya mambo yanayokwamisha upatikanaji wa amani
na utulivu duniani. Wadau mbali mbali wamejitahidi kudhibiti hali hii lakini bado
hakuna mafanikio ya kuridhisha hadi sasa. Pengine umefika wakati wa kuanzisha mikakati
mipaya ya kupambana na hali hii si tu wakati wa dharura, bali kwa kuwa na sera makini
na zinazowajibisha na kuwashirikisha watu katika ngazi mbali mbali.
Tatizo
hili lina sehemu kuu mbili, sehemu ya kwanza ni ile ineyoonesha upendo, ukarimu na
mshikamano wa binadamu kwa kuwakirimia wahamiaji na wakimbizi huduma msingi na sehemu
ya pili ni vikwazo wanavyowekewa wahamiaji na wakimbizi hawa katika mchakato wa kutafuta
hifadhi ya maisha na kufanya kazi kwa amani: Hawa ni watu wanaohatarisha maisha yao,
wanaoteswa, kudhulumiwa na kunyanyaswa utu wao na hatima yake ni kufa katika hali
ya utupu jangwani au baharini.
Baba Mtakatifu anasema, baadhi ya watu wanalazimika
kuyakimbia makazi yao kutokana na vita na kinzani za kijamii pamoja na kuenea kwa
biashara ya silaha duniani. Baba Mtakatifu anasema, haya ni madonda ya ulimwengu yanayopaswa
kuponywa, ili kulinda na kudumisha utu, heshima na haki msingi za binadamu. Amani
na biashara ya silaha anasema Baba Mtakatifu ni mambo ambayo hayawezi kupikika katika
chungu kimoja! Haki msingi za binadamu hazina budi kuheshimiwa kwa vitendo vinavyoongozwa
na mshikamano wa kimataifa.
Vatican itaendelea kushirikiana na Jumuiya ya Kimataifa
ili kweli: haki, amani na haki msingi za binadamu ziweze kuheshimiwa na kuthaminiwa
na wengi. Baba Mtakatifu amewahakikishi Mabalozi wapya ushirikiano wa dhati kutoka
Vatican katika utekelezaji wa majukumu na dhamana yao hapa mjini Vatican.