2014-05-14 09:19:26

Uchaguzi mkuu nchini Sudan ya Kusini?


Wananchi wa Sudan ya Kusini hawataweza kufanya uchaguzi mkuu hapo mwakani kama ilivyokuwa imepangwa awali, bali uchaguzi huu unaweza kufanyika kati ya mwaka 2017 hadi mwaka 2018 kadiri hali itakavyoruhusu. Hatua hii imetangazwa na Rais Salva Kiir Mayardit wa Sudan ya Kusini, ili kusaidia mchakato wa upatanisho wa kitaifa baada ya machafuko ya kisiasa yaliyojitokeza nchini humo kuanzia Mwezi Desemba, 2013 na hivyo kupelekea watu wengi kupoteza maisha na wengine kulazimika kuyakimbia makazi yao.

Tamko hili linakuja siku chache tu tangu Serikali na wapinzani Sudan ya Kusini walipoamua kwa pamoja kusitisha vita ili kutoa nafasi kwa wakulima kuanza kushughulikia mashamba yao pamoja na uundwaji wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa, kama ilivyokubalika kwenye mkutano uliofanyika hivi karibuni mjini Addis Ababa, Ethiopia. Hata hivyo pande hizi mbili zimekuwa zikishutumiana kwa kuvunja mkataba wa kusitisha mapigano.

Wakati huo huo, Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana Ban Ki-Moon ameshauri kwamba, liundwe Baraza maalum litakalochunguza kuhusu mauaji ya kivita na vitendo dhidi ya ubinadamu vilivyofanywa wakati wa machafuko ya hali ya hewa nchini humo.







All the contents on this site are copyrighted ©.