Ifuatayo ni hotuba iliyotolewa na Rais Jakaya Kikwete wa Tanzania kwenye ufunguzi
wa nne wa wadau wa Shirika la Taifa la hifadhi ya Jamii, NSSF, tarehe 13 Mei 2014.
Nakushukuru
Mheshimiwa Waziri na Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa NSSF kwa kunikaribisha kufungua
mkutano wa nne wa wadau wa Hifadhi ya Jamii unaoanza leo hii hapa jijini Arusha. Mkutano
wa mwaka huu una umuhimu wa kipekee kwani ni fursa ya kujipongeza kwa NSSF kutimiza
miaka 50 tangu kuanzishwa kwake mwaka 1964. Wakati ule ikijulikana kama Mfuko wa Akiba
ya Wafanyakazi (NPF).
Nakupongeza Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini na wajumbe
wako, Mkurugenzi Mkuu na Menejimenti ya shirika pamoja na wafanyakazi wote wa NSSF
kwa kazi nzuri mnayoifanya na mafanikio yaliyopatikana. Kazi yenu inaonekana na inapimika.
Kutokana na kazi yenu nzuri, mnawatia moyo wanachama wenu na kuwapa imani kuwa amana
zao walizowekeza kwenu ziko salama, na kwamba mko tayari kukabiliana na changamoto
za leo, na za miaka 50 ijayo.
Umuhimu wa Mikutano ya Wadau
Mheshimiwa
Waziri na Wadau; Nimefurahishwa na utamaduni wenu wa kuwa na mikutano hii ya wadau
kila mwaka. Ni utamaduni mzuri kwani unatoa fursa ya wadau kushiriki katika kufanya
tathmini ya mwaka hadi mwaka na kupeana mrejesho wa hali ilivyo miongoni mwa wadau.
Utaratibu huu unasaidia kuamsha ari ya kutekeleza malengo. Ni fursa nzuri pia ya kuhuisha
malengo yenu kuendana na mabadiliko ya mazingira, maana tofauti na zamani, mabadiliko
katika dunia ya sasa yanakwenda kwa kasi kubwa. Huu ni utamaduni ambao hamna budi
kuudumisha na kuuendeleza.
Umuhimu wa Hifadhi ya Jamii
Mheshimiwa Waziri
na wadau wa hifadhi ya jamii, Hifadhi ya Jamii ni haki ya msingi na asili ya kila
mwanadamu. Msingi wa haki yenyewe ni kulinda thamani ya utu wa binadamu. Haki hii
inazingatia kuwa binadamu kwa asili ni mwanajamii, anastawi tu akiwa miongoni mwa
jamii na anachangia katika maendeleo ya jamii yake, hivyo, anayo haki ya kusitiriwa
na kupata hifadhi kutoka kwa jamii pale uwezo wake wa kuchangia unapokoma kutokana
na uzee, ulemavu au janga lisilotazamiwa.
Hifadhi ya jamii ina faida kwa mwanajamii
na jamii yenyewe. Kwa upande mmoja inamkinga mwanajamii dhidi ya kupoteza utu na thamani
katika jamii, na upande wa pili inaikinga na kuinusuru jamii dhidi ya madhara ya kiuchumi
na kiusalama yanayoweza kusababishwa na kuwa na jamii iliyokata tamaa.
Upo
uhusiano mkubwa kati ya ustawi wa jamii na hifadhi ya jamii. Ndio maana, Mkataba wa
Kimataifa wa Haki za Binadamu wa mwaka 1948 umetambua haki ya binadamu kupata hifadhi
na Katiba ya nchi yetu ya mwaka 1977, nayo imetambua haki ya kupata hifadhi ya jamii.
Katika Ibara ya 11, ibara ndogo (i). Katiba inatamka kuwa “Mamlaka ya nchi itaweka
utaratibu unaofaa kwa ajili ya kufanikisha utekelezaji wa haki ya mtu kufanya kazi,
haki ya kupata elimu na haki ya kupata msaada kutoka kwa jamii wakati wa uzee, maradhi
au hali ya ulemavu, na katika hali nyinginezo za mtu kuwa hajiwezi...” Huu ni wajibu
wetu kikatiba na tutaendelea kuutekeleza.
Hali ya Sekta ya Hifadhi ya Jamii
Nchini
Ndugu Wadau; Shughuli za Hifadhi ya Jamii nchini imeanza miaka 50
iliyopita na hatua kubwa imepigwa katika kipindi hicho. Sisi sote ni mashahidi wa
mapinduzi makubwa yaliyofanyika katika Sekta hii. Idadi ya mifuko, wigo wa wanachama
na idadi ya mafao.
Tulianza na Mfuko mmoja tu wa akiba ya wafanyakazi maaarufu
kwa jina la NPF mwaka 1964. Leo tuna mifuko 6 ya NSSF, PPF, LAPF, GEPF, PSPF na NHIF.
Wigo wa wanachama wa mifuko hii nao umetanuka. Mwanzoni ilihusu watumishi walioajiriwa,
tena walichaguliwa mfuko wa kujiunga nao kutokana na sekta zao lakini leo tunao wanachama
kutoka sekta binafsi waliojiajiri, na wako huru kuchagua mfuko wanaoupenda kujiunga
nao. Hali kadhalika, mafao yaliyokuwa yakitolewa wakati ule yalikuwa ni mafao ya pensheni
tu, tena kwa mkupuo mmoja, hivi sasa kuna mafao mengi na malipo ni kwa mwezi katika
uhai wote wa mwanachama. Mafao mengine hufaidisha hata wategemezi wa mwanachama.
Mafanikio
yaliyopatikana katika sekta ya Hifadhi ya Jamii yamekuwa na mchango mkubwa katika
uchumi wa taifa letu. Sekta hii ilichangia wastani wa asilimia 11 ya pato la taifa
kwa mwaka 2011/2012. Mtaji wa mifuko hii sasa umefikia shilingi trilioni 5,242 kutoka
trilioni 1.36 mwaka 2005/2006. Kutokana na hali nzuri ya ukwasi tayari mifuko hii
imewekeza kiasi cha shilingi trilioni 4.4 mwaka 2012 ambapo asilimia 19 imewekezwa
kwenye sekta ya ujenzi na makazi, asilimia 18 kwenye hisa na asilimia 63 kwenye amana
za serikali na mikopo.
Miaka 50 kutoka Mfuko wa Akiba ya Wafanyakazi (NPF)
hadi Mifuko wa Hifadhi ya Jamii (NSSF).
Ndugu Wadau wa Hifadhi ya Jamii; Serikali,
kupitia Sheria Na. 28 ya mwaka 1997, ilianzisha Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii
– NSSF, kwa kuboresha Shirika la Akiba ya Wafanyakazi (NPF) lililoanzishwa mwaka 1964.
Maboresho hayo yalilenga kuongeza ubora na idadi ya mafao, kupanua wigo wa wanachama
na kuisaidia Serikali katika kutoa huduma za hifadhi ya jamii. Mabadiliko haya yaliliwezesha
Shirika la NSSF kutoa mafao ya pensheni ya uzeeni, urithi na ulemavu kwa wanachama
wake pamoja na mafao mengine kama vile matibabu, uzazi, fidia ya kuumia kazini na
gharama za mazishi.
NSSF imeendelea kukua na kuimarika mwaka hadi mwaka. Thamani
ya mfuko imeongezeka kutoka shilingi trilioni 1.97 katika mwaka 2011/2012 hadi kufikia
shilingi trilioni 2.24 mwaka 2012/2013. Kuongezeka huko kwa thamani ya mfuko kumeambatana
na kuongezeka kwa mafao yanayolipwa na NSSF kutoka shilingi bilioni 178 mwaka 2011/2012
hadi shilingi bilioni 228 mwaka 2012/2013.
NSSF imekuwa mchangiaji muhimu
kwa maendeleo ya nchi yetu kwa kuwekeza kwenye miradi ya maendeleo inayochochea ukuaji
wa uchumi na kuongezeka kwa ajira. Tumeona manufaa ya uwekezaji wa NSSF katika ujenzi
wa Chuo Kikuu cha Dodoma, daraja la Kigamboni, ujenzi wa Chuo Kikuu cha Nelson Mandela
na miradi ya ujenzi wa nyumba za watumishi wa umma na nyumba za wafanyakazi.
Inafurahisha
kusikia kuwa shirika limetunukiwa cheti cha kimataifa cha utoaji wa huduma bora (ISO
9001:2008 CERTIFICATION), na hivi karibuni, kutunukiwa cheti cha utawala bora kwa
kufuata kanuni bora za manunuzi na ugavi (PPRA Award). Kwa haya mawili nawapongeza
sana na kuwaomba muendelee na viwango hivi vya ueledi. Maana shirika lenu ni nyeti
katika uchumi wa taifa, kwa kuwa mmeaminiwa kuhifadhi na kuwekeza kwa fedha za akiba
za wanachama. Umakini mkubwa unahitajika katika kuwekeza. Hamna budi kuwekeza vizuri
ili mfuko uendelee kustawi na wanachama wake waendelee kupata hifadhi kutoka kwenu.
Wajibu wa Serikali: Usimamizi na Uendeshaji wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii
Ndugu
Wadau wa Hifadhi ya Jamii; Sisi katika Serikali tunao wajibu wa msingi wa kulea
mifuko hii ili iweze kustawi na kuwa endelevu. Katika kutekeleza wajibu wetu huo,
na kwa kuzingatia ukuaji wa sekta yenyewe, Serikali ilianzisha Mamlaka ya Udhibiti
wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii (SSRA) mwaka 2010. Lengo kuu la kuanzishwa kwa SSRA
ni kusimamia na kuratibu shughuli zote katika Sekta ya Hifadhi ya Jamii hapa nchini,
ikiwa ni pamoja na kufanya maboresho katika nyanja za uwekezaji na mafao yanayotolewa
kwa wanachama.
Naipongeza Wizara ya Kazi na Ajira pamoja na Msimamizi na Mdhibiti
wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii (SSRA) kwa kazi nzuri wanayoifanya katika kusimamia
mageuzi ya kiutendaji na ya uendeshaji wa Mifuko hii ya Hifadhi ya Jamii. Naiomba
SSRA iendelee kuboresha mazingira ya ushindani katika mifuko kwani ushindani hatimaye
huleta unafuu kwa wanachama. Tumeona namna ambavyo ushindani umechochea kila Mfuko
kuongeza ubunifu katika utoaji wa huduma na aina ya mafao yanayotolewa. Kazi kubwa
waliyonayo sasa, ni kubuni mkokotoo mpya utakaosaidia kuoanisha mafao yatolewayo na
mifuko hiyo. Wito kwa NSSF na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii
Ndugu wadau wa
hifadhi ya jamii, Pamoja na mchango mkubwa wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii katika
uchumi na maendeleo ya taifa kwa ujumla, bado ni sehemu ndogo sana ya Watanzania wanapata
kinga dhidi ya majanga kupitia Mifuko hii. Takwimu zinaonyesha kwamba kati ya Watanzania
milioni 22.4 wenye uwezo wa kuzalisha kipato, waliomo katika Mifuko yote 6 si zaidi
ya asilimia 6 tu. Idadi hii ni ndogo sana ukilinganisha na idadi ya Watanzania ambao
wanafanya kazi zenye kipato. Aidha idadi hii ni ndogo ikilinganishwa na wastani wa
asilimia 10kwa nchi za Afrika na Kusini mwa Asia.
Kwa mujibu wa tathmini ya
Sekta ya Viwanda na Biashara Ndogondogo (SMEs) ya mwaka 2013, sekta isiyo rasmi ilichangia
asilimia 39.7 ya pato la taifa kwa mwaka 2010. Vile vile, ilikadiriwa kuwa zipo SMEsmilioni
3 zinazoajiri wananchi milioni 5.2. Wito wangu kwenu ni mifuko ya hifadhi ya jamii
kutoka maofisini kwenda kuhamasisha wananchi wengi wajiunge na mifuko hii.
Waelezeni
manufaa yake, na watoeni hofu zao juu ya fikra potofu walizonazo kuhusu hifadhi ya
jamii. Wengi wanaamini hifadhi ya jamii ni stahili ya wafanyakazi wajiriwa tu, tena
wafanyakazi wa kipato kikubwa. Wajulisheni kuwa hivi sasa hifadhi ya jamii ni fursa
huru kwa wote, wale walioajiriwa na wale waliojiajiri. Wafafanulieni wale walio kwenye
sekta isiyo rasmi kuwa, utaratibu wa wao kujiunga, kuchangia na kunufaika. Waonyesheni
mifano hai ya wale wakulima na wajasiriamali namna wanavyochangia na wanavyofaidika.
Natoa rai hii nikitambua kuwa wako wananchi wengi katika sekta ya kilimo na
sekta isiyo rasmi ambao kwa vipato vyao wangeweza kujiunga na hifadhi ya jamii. Nawapongeza
NSSF kwa mpango wake wa kuwafikia wakulima na wachimbaji wa madini ambapo hadi sasa
wakulima 29,000 wachimbaji madini 7000 wamejiunga na NSSF na wanafaidika na mafao
yanayotolewa.
Uzoefu wa NSSF unatuonyesha kwamba wananchi wengi wamekosa tu
uelewa na taarifa sahihi. Wakumbusheni kuwa hifadhi ya jamii si jambo jipya au la
kigeni, hata katika jamii zetu kabla ya kuja kwa mifumo hii rasmi, kumekuwepo na utaratibu
wa jamii kujiwekea mifumo ya hifadhi ya jamii. Katika jamii zetu kumekuwa na utaratibu
wa kuwahudumia wazee, wasiojiweza na watoto. Mtu hakupoteza heshima na thamani yake
katika jamii kwa kuwa amepoteza uwezo wake wa kuchangia katika jamii, ama kwa kustaafu,
kwa ajali au kwa kutojaaliwa uwezo wa kuchangia.
Mabadiliko ya kidunia yameifanya
mifumo hiyo sasa isiweze kuhimili jukumu hilo. Hivyo, mifuko ya hifadhi ya jamii ndio
mbadala na salama ya ustawi wa mtu katika dunia ya leo. Wakumbusheni kuwa shida na
majanga huwafika watu wakati ambao hawajajiandaa. Hivyo, ni vyema kujisitiri kabla
hujasitiriwa.
Ndugu wadau wa hifadhi ya jamii, Ni vizuri kukumbushana pia
kwamba, uhai wa mifuko ya hifadhi ya jamii unategemeana pia na uendelevu wa michango
ya wanachama. Hivyo, hatuna budi pia kutoa kipaumbele katika kuelimishana juu ya umuhimu
na wajibu wa waajiri kuwasilisha michango ya wanachama kwa wakati. Mifuko ya hifadhi
ya jamii inatakiwa kuhakikisha inakusanya michango ya wanachama wake bila ajizi. Wahamasisheni
wanachama wa mifuko juu ya umuhimu wa kuhakikisha michango yao inawasilishwa, na inabaki
katika mifuko ya hifadhi ya jamii ili iwafae wakati wa matatizo na maisha ya uzeeni.
Waelemisheni juu ya athari ya tabia ya sasa ya baadhi ya watumishi kuamua kushirikiana
na waajiri wasio waaminifu kutopeleka michango hiyo, au baadhi ya wanachama kujitoa
katika mifuko ya awali pale inapotokea amebadilisha ajira kutoka kwa mwajiri mmoja
kwenda kwa mwingine.
Mchango wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kuelekea Dira ya
2025
Ndugu Wadau wa Hifadhi ya Jamii; Mifuko ya hifadhi ya jamii ina wajibu
mkubwa wa kuchangia juhudi za Serikali katika kufikia dira yetu ya kuwa nchi yenye
uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025. Mifuko hii imeonyesha uwezo wa kuwekeza katika
sekta na miradi ya uwekezaji wa muda mrefu ambayo sekta binafsi imekuwa ikikwepa.
Miradi ya aina hii kama miundombinu msingi na nishati ndio inayoweza kukwamua nchi
katika umasikini, na kuleta mapinduzi kimaendeleo.
Uzoefu huu unashawishi kuwa
mifuko hii sasa itazame katika sekta ya Kilimo. Kilimo ndio sekta mama ya uchumi wetu
na inaajiri zaidi ya asilimia 70 ya wananchi wetu, lakini ukuaji wake ni asilimia
4.4 ambayo ni chini ya kiwango kinachotakiwa cha asilimia 6 kwa mwaka kutokana na
kukosa uwekezaji wa kutosha. Ndio sababu, pamoja na kasi nzuri ya ukuaji wa uchumi
ya wastani wa asilimia 7, umasikini umepungua kwa asilimia 2 tu.
Umasikini
huzuia pia kasi ya ukuaji wa mifuko ya hifadhi ya jamii. Hivyo, uwekezaji wenu katika
sekta itakayosaidia kuondoa umasikini, ni kujitengenezea pia fursa kwa mifuko yenu
kupata wanachama wengi zaidi siku za usoni. Tumeshuhudia namna ambavyo uwekezaji wa
pamoja wa NSSF, PPF na PSPF wa kiasi cha asilimia 45katika Kiwanda cha Sukari cha
Kagera kumezalisha ajira 3,500. Mbali na ajira, wataalam wanasema pia kuwa katika
kila shilingi moja inayowekezwa vizuri kwenye kilimo, huzalisha faida ya hadi shilingi
3.2. Nawatia shime muangalie uwezekano wa kuwekeza katika kilimo hususan kwenye viwanda
vya pembejeo za kilimo na vya kusindika na kuongeza thamani ya mazao. Tukiweza kuongeza
thamani na kuepuka kuuza nje mazao ghafi, tutakuwa tumewatoa Watanzania wengi kutoka
kwenye umasikini na mifuko yetu itapata wanachama wengi zaidi na wenye uwezo mkubwa
zaidi wa kuchangia mifuko hiyo.
Hitimisho Ndugu wadau wa hifadhi ya jamii, Kwa
kumalizia napenda kwa mara nyingine tena kukushukuru Mheshimiwa Waziri kunialika na
nikupongeze kwa namna unavyilea vizuri mifuko yetu ya hifadhi ya jamii. Nakupongeza
Mwenyekiti wa Bodi ya NSSF kwa uongozi wenu mzuri. Natoa pongezi nyingi kwa Mkurugenzi
Mkuu, Dkt. Ramadhani Dau kwa kazi nzuri unayoifanya, na mafanikio makubwa yaliyopatikana
katika NSSF chini ya uongozi wako. Nifikishie pongezi hizi pia menejimenti na wafanyakazi
wote wa NSSF. Kazi mnayoifanya inaonekana na tuna matarajio ya kuona mengi na makubwa
zaidi miaka hamsini ijayo.
Baada ya kusema hayo, napenda kutangaza kwamba
mkutano huu wa nne wa wadau wa Shirika la Taifa Hifadhi ya Jamii (NSSF) umefunguliwa
rasmi. Nawatakia mkutano mwema. Ahsanteni sana kwa kunisikiliza.