2014-05-13 07:36:13

Twendeni Bethlehemu!


Katika dini nyingi iko desturi nzuri ya kiroho ya kufanya hija pahala patakatifu au sehemu za kihistoria za dini hiyo. Hija hiyo mara nyingi hufanyika kama moja ya kuadhimisha tukio fulani muhimu linalomhusu mtu binafsi ili kujichumia neema anayohitaji mhiji au alhaji. RealAudioMP3

Papa pia hufanya hija sehemu mbalimbali kama vile Lourdes, Fatima, Loreto, Namugongo, Nchi Takatifu, nakadhalika. Hija ya Papa haiwi kwa ajili yake binafsi tu, bali hasa ni kuchuma neema kwa ajili ya kanisa zima, pia inakuwa kwa ajili ya kuimarisha mahusiano ya kuletesha haki, amani na upendo kati ya nchi na nchi.

Mwaka huu kuna jubilei za dhahabu kadhaa za kikanisa zitokanazo na Mtaguso wa pili wa Vatican. Zaidi pia ni mwaka wa 50 tangu Papa Paulo VI alipohiji nchi ya ahadi na kuzungumza na Patriaki Anathagora wa Yerusalemu. Papa Fransis atahiji nchi ya ahadi ikiwa ni kuadhimisha jubilei ya dhahabu ya hija hiyo ya Papa Paulo VI. Katika hija hiyo, Papa atakutana na viongozi muhimu wa serikali na dini, atakutana pia na waumini wenzetu walioko huko.

Papa atazuru sehemu chache muhimu. Mosi, ataenda Bethlehemu kuzuru na kusali pahala alipozaliwa Yesu. Ataenda kuzuru na kusali kando ya mto Yordani alikobatizwa Yesu. Mwisho ataenda kuangalia chumba ambacho Yesu alikula Karamu ya Mwisho na mitume wake. Chumba hicho ni mandhali ya mwisho aliyokuwa Yesu kabla ya kuteswa na kufa kwake.

Kwa hiyo, Wakristu wote na watu wote wenye mapenzi mema tunaalikwa mosi, kuiombea hija hii ya Papa, kusudi asafiri salama, aende akatuombee na kufanikisha makusudio aliyojipangia kwa faida yake, na kwa manufaa ya kanisa zima na ulimwengu kijumla, na hatimaye arudi salama, kusudi Mungu atukuzwe katika yote.

Pili tunaalikwa sisi sote kutanguzana na Papa kwenda katika hija hiyo, usikose kuwepo katika msafara huo wa Baba Mtakatifu. Kutokana na msongamano wa watu na hasa kupanda gharama ya maisha, siyo wote watafanikiwa kwenda hiyo hija. Tunaalikwa kukata tiketi ya kiroho ambayo gharama yake ni bure sanasana inategemea uhuru wako mwenyewe, na mkatishaji tiketi ni Roho Mtakatifu mwenyewe ambaye hata Yeye mwenyewe ataenda kwenye hija hiyo ya awali tangu atoke huko alipokufa Yesu Msalabani. “Akainama kichwa akaitoa Roho yake”.

Kwa watakaoenda huko kwa tiketi ya Roho Mtakatifu, mnaalikwa kusoma ramani hii au mwongozo ufuatao, utakaowasaidia kujua sehemu mbalimbali mtakazotembelea na kuzihiji pindi mnaongozana na Papa. Hizo ni sehemu muhimu ambazo kulifanyika mambo makuu na mazito yahusuyo ukombozi wetu. Katika mwongozo huu tutajaribu kuzieleza kwa kifupi sana sehemu hizo kijiografia na kiteolojia. Tutaona pia matukio yaliyotokea sehemu hizo, yahusuhuyo Yesu au mitume wake na sisi tunaweza kupata fundisho gani toka sehemu hiyo.

Hebu twendeni kwanza Betlehemu alikozaliwa Yesu tuhimizane kwenda huko kwa maneno ya Wachungaji waliokuwa wanahimizana kwenda huko baada ya kupata taarifa toka kwa malaika: “Twendeni mpaka Betlehemu, tukashuhudie tukio hilo alilotujulisha Bwana.” (Lk 2:15).

Imeandaliwa na
Padre Alcuin Nyirenda, OSB.








All the contents on this site are copyrighted ©.