Baba Mtakatifu ametuma salam za rambi rambi kwa Askofu mkuu Francesco Moraglia kufuatia
kifo cha Kardinali Marco Cè, Patriak mstaafu wa Jimbo kuu la Venezia, Italia kilichotokea
Jumatatu usiku tarehe 12 Mei 2014. Baba Mtakatifu anapenda kutoa salam zake za rambi
rambi kwa Familia ya Mungu Jimboni Venezia na wale wote walioguswa na msiba huu.
Baba
Mtakatifu anasema, Marehemu Kardinali Cè ni kiongozi aliyelihudumia Kanisa kwa furaha,
kwanza kabisa Jimboni mwake Cremona alikozaliwa, Jimbo kuu la Bologna, akiwa msaidizi
mkuu wa Kardinali Poma na kama kiongozi wa kiroho wa Vijana Wakatoliki Italia na baadaye
kama kiongozi mwenye busara na mnyenyekevu wa Jimbo kuu la Venezia.
Baba Mtakatifu
anakumbuka kwa namna ya pekee huduma za maisha ya kiroho zilizotolewa na Marehemu
Kardinali Cè, katika kutangaza Neno la Mungu kwa njia ya mafungo kwa Makleri na vijana
pamoja na kushiriki katika kumwilisha maadhimisho makini ya Liturujia ya Kanisa katika
maisha ya waamini. Kwa maombezi ya Bikira Maria, Baba Mtakatifu anapenda kuiweka roho
ya Marehemu Kardinali Marco Cè huko Yerusalemu ya mbinguni. Anawapatia wote baraka
zake za kitume kwa wote wanaoomboleza.
Ratiba ya mazishi ya Marehemu Kardinali
Cè, inaonesha kwamba Jumatano asubuhi, waamini watafanya maandamano ili kutoa heshima
zao za mwisho na mazishi yatafanyika, Jumamosi asubuhi, tarehe 17 Mei 2014 kwenye
Kanisa kuu la Mtakatifu Marko, Venezia.