2014-05-12 09:54:20

Umuhimu wa mawasiliano ya Jamii


Mawasiliano kwa ajili ya huduma ya utamaduni wa kweli wa kukutana ndiyo kauli mbiu itakayoongoza semina ya mawasiliano ya jamii kwa ajili ya Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Amerika ya Kusini, CELAM, kuanzia tarehe 12 hadi tarehe 15 Mei 2014. RealAudioMP3

Askofu mkuu Cladio Maria Celli, Rais wa Baraza la Kipapa la Mawasiliano ya Jamii katika ujumbe wake kwa njia ya video anasema, bila shaka mwelekeo wa semina hii hautajikita katika suala la teknolojia peke yake, lakini kama sehemu ya tafakari ya kina inayofanywa na Mama Kanisa kwa kutoa kipaumbele cha kwanza katika maboresho ya matumizi ya njia za mawasiliano ya jamii.

Maaskofu wanapaswa kutambua kwamba, wanadhamana na wajibu nyeti katika matumizi sahihi ya vyombo vya mawasiliano ya Jamii. Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kuwachangamotisha viongozi wa Kanisa kuwa mstari wa mbele katika matumizi sahihi ya vyombo vya mawasiliano ya Jamii, ili kuhakikisha kwamba, Injili ya Furaha inatangazwa hadi pembezoni mwa maisha ya watu ndani ya Jamii husika.

Mawasiliano yanapaswa kuwa ni huduma inayowawezesha watu kukutana na kushirikishana mang’amuzi na vipaumbele vya maisha. Semina hii itawashirikisha Maaskofu mabingwa katika masuala ya njia za mawasiliano ya kijamii kutoka Hispania na Amerika ya Kusini.

Askofu mkuu Claudio Maria Celli anawatakia kheri na baraka tele Maaskofu Katoliki Amerika ya Kusini, katika mchakato wa kuendeleza utajiri mkubwa ambao maendeleo ya sayansi na teknolojia unatoa kwa Mama Kanisa katika jitihada zake za kichungaji za kutangaza Ufalme wa Mungu na Injili ya Kristo hadi miisho ya dunia.








All the contents on this site are copyrighted ©.