Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya limeitaka Serikali ya Kenya kusimama kidete kulinda
na kutetea maisha ya wananchi wake, kwani katika siku za hivi karibuni watu wengi
wamepoteza maisha yao kutokana na mashambulizi ya kigaidi, ajali barabarani, ujambazi
na unyang'anyi, baadhi ya watu kujinyonga hadi kufa, ulevi wa kupindukia na baa la
njaa kwa baadhi ya watu.
Hii inatokana na kuzagaa kwa silaha za moto kiasi
cha kutishia amani na usalama kwa Nchi ya Kenya ambayo kwa miaka mingi ilikuwa ni
inajivunia amani na utulivu, lakini sasa imegeuka kuwa ni uwanja wa vitendo vya kigaidi
na ukosefu wa: usalama, amani na utulivu.
Kamwe, Kanisa haliwezi kukubali
kuona vitendo hivi vinaendelea katika Jamii, changamoto kwa kila raia wa Kenya kushirikiana
kikamilifu na vyombo vya ulinzi na usalama ili kuweza kutokomeza vitendo vinavyochafua
hali ya ulinzi na usalama nchini humo. Ni mwaliko kwa wanasiasa na viongozi wa Serikali
kuwa macho na kauli zao, ili zisiwe ni chanzo cha kuwagawa wananchi, kwani kwa sasa
kipaumbele cha kwanza ni kujenga na kuimarisha umoja na mshikamano wa kitaifa.
Hayo
yamesemwa hivi karibuni na Kardinali John Njue, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki
Kenya, ambaye pia amelaani vitendo vya rushwa na ufisadi kuanzia katika ngazi ya taifa
hadi kwenye vitongoji. Maaskofu wanasema, watu wanataka kuona maendeleo, lakini wapi!
Jambo la kushangaza ni viongozi Serikalini kujiongezea mishahara na marupurupu manono,
wakati wananchi wa kawaida wanaendelea kuogelea katika umaskini na hali ya kukata
tamaa.
Ustawi, maendeleo na mafao ya wengi yapewe msukumo wa pekee katika
mikakati ya Serikali ya Kenya. Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya linawataka wananchi
wote kuungana kwa pamoja ili kupambana kufa na kupona dhidi ya rushwa na ufisadi;
viongozi walioko madarakani waache mchezo mchafu wa uchu wa mali na madaraka na badala
yake waanze kujielekeza katika utoaji huduma kwa wananchi wa Kenya.