2014-05-12 10:51:34

Jeshi la Polisi nchini Kenya lifanyiwe marekebisho makubwa!


Askofu mkuu Zacchaeus Okoth, Mwenyekiti wa Tume ya Haki na Amani, Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya anasema kwamba, kuna haja ya kuharakisha mageuzi katika mfumo na utendaji wa Jeshi la Polisi nchini Kenya, ili Jeshi la Polisi liweze kuwajibika zaidi kwa wananchi, kwa kulinda maisha na mali zao. Ni wajibu wa raia kutambua kwamba, ulinzi na usalama uko mikononi mwao na kwamba, wanapaswa kushirikiana kikamilifu na Jeshi la Polisi, ili kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani na upatanisho wa kitaifa.

Askofu mkuu Okoth anasema, wananchi wa Kenya kwa sasa wanaishi katika mazingira hatarishi na wasi wasi mkubwa kutokana na ukosefu wa amani na utulivu, kwani kuna silaha nyingi za moto ambazo zimezagaa mikononi mwa wananchi. Ni wajibu wa Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na wananchi kuhakikisha kwamba, silaha hizi zinadhibitiwa, ili watu waweze kuwa na uhakika wa usalama wa maisha na mali zao.

Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya linasema, kuna haja kwa Serikali kuimarisha kikosi cha intelijensia kitaifa, ili kukabiliana na matukio ambayo yanataka kuvuruga misingi ya haki, amani na utulivu nchini Kenya. Jeshi la Polisi linapaswa kuwa makini kutokana na madhara ya ulevi wa kupindukia ambao umesababisha katika siku za hivi karibuni, watu wengi kupoteza maisha au kulazwa hospitalini, huko Nairobi.







All the contents on this site are copyrighted ©.