2014-05-12 10:06:05

Haki, amani, mazingira na mshikamano kati ya binadamu!


Chuo Kikuu cha Kipapa cha Mtakatifu Anthony, kilichoko mjini Roma, kuanzia tarehe 29 Aprili hadi tarehe 9 Mei, 2014 kimekuwa kikiendesha kozi maalum kuhusu haki, amani na ukamilifu wa uumbaji. Ni kozi ambayo imewashirikisha Watawa wa Shirika la Mtakatifu Francisko wa Assisi ambao utunzaji wa mazingira ni sehemu ya karama na maisha yao ya kiroho. Wanafunzi na wadau mbali mbali wa mazingira wamehudhuria kwa wingi. RealAudioMP3

Takwimu za Umoja wa Mataifa zinaonesha kwamba, kuna zaidi ya watu millioni 232 ambao wamelazimika kuzihama nchi zao kwa sababu mbali mbali, moja ya sababu hizi ni kutafuta ajira katika medani za kimataifa. Kuna watu millioni 16, kati yao kuna watu wanaotafuta hifadhi ya kisiasa; kuna watu millioni 28. 8 ambao hawana makazi maalum kutokana na vita na kinzani za kijamii; watu millioni 15 wamejikuta wanakuwa ni wakimbizi kutokana na madhara ya maafa asilia na wengine millioni 15 ni wale wanaojikuta wametumbukia katika kundi la wakimbizi na wahamiaji kutoka na sakata la maendeleo ya mwanadamu!

Padre Gabriele Bentoglio, Katibu mkuu msaidizi wa Baraza la Kipapa la haki na amani wakati akitoa muhadhara Chuoni hapo anasema, makundi yote haya yanahitaji huduma maalum ya kichungaji sanjari na kusimama kidete kupambana kufa na kupona na watu wanaojihusisha na biashara haramu ya binadamu. Kanisa litaendelea kuweka mbinu mkakati wa kusaidia kusitisha biashara hii pamoja na kuwasaidia waathirika.

Makanisa mahalia hayana budi kuliangalia tatizo la wakimbizi na wahamiaji ili kujiwekea mikakati ya kichungaji, kwa kukuza na kudumisha majadiliano, kwa kuonesha ushuhuda wa upendo, utu na heshima ya binadamu; kwa kuwajengea uwezo wakimbizi na wahamiaji, ili waweze kujitegemea pamoja na kujenga mazingira bora zaidi yanaonesha ukarimu, mshikamano na umoja wa kidugu; mambo ambayo yanapaswa kuendelezwa na waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema.

Mama Kanisa hana budi kujielekeza zaidi katika majadiliano na wadau mbali mbali ili kupata suluhu ya kinzani za kijamii, kisiasa na kikabila ambazo zimepelekea mauaji ya kimbari pamoja na kuibua makundi makubwa ya wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum. Uhuru wa kidini ni jambo ambalo linapaswa kuangaliwa kwa umakini mkubwa, kwani migogoro na kinzani za kidini zimekuwa ni chanzo cha maafa makubwa kwa watu na mali zao. Watu wengi kwa sasa wanahofu na wala hawana uhakika wa usalama wa maisha yao kutokana na fujo pamoja na vurugu za kidini sehemu mbali mbali za dunia. Kanisa bado linahamasishwa kujielekeza zaidi katika utamadunisho, ili kweli Injili ya Kristo iweze kupewa msukumo wa pekee katika maisha na vipaumbele vya waamini.

Ikumbukwe kwamba, imani ni zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu, kumbe, hata waamini wanahamasishwa kuwashirikisha wengine zawadi hii, kama ilivyo hata kwa wahamiaji na wakimbizi, ambao wamesaidia kuleta ari na mwamko wa maisha ya kiroho katika nchi zile ambazo wamepokelewa kwa heshima na taadhima.

Padre Bentoglio anasema, Kanisa haliangalii makundi makubwa ya wahamiaji na wakimbizi wala idadi yao, katika masuala kama haya, Kanisa linaona kwa kila mkimbizi na mhamiaji ile sura na mfano wa Mungu, changamoto na mwaliko wa kuwaheshimu na kuwathamini wakimbizi na wahamiaji kama binadamu, wanaopaswa kuheshimiwa na kupewa haki zao msingi. Kila mtu anawajibika kutekeleza wajibu wake katika kudhibiti, kulinda na kuwatetea wakimbizi na wahamiaji.

Padre Gabriele Bentoglio amewapongeza waamini walei wanaoendelea kujisadaka kwa ajili ya kuwahudumia wakimbizi na wahamiaji wanaotafuta nafuu ya maisha ugenini. Hili ni kundi ambalo linapaswa kusaidiwa kukuza ukarimu huu kwa njia ya majiundo makini na endelevu. Kanisa liangalie uwezekano wa kuwaandaa wachungaji watakaojikita katika kuwahudumia wakimbizi na wahamiaji, kwa kuwapatia elimu na majiundo kamili.








All the contents on this site are copyrighted ©.