2014-05-12 09:43:55

Ebo! Mnataka kurudi tena makaburini?


Mpendwa msikilizaji wa kipindi chetu cha Kanisa la nyumbani, TUMSIFU YESU KRISTO. RealAudioMP3

Tukiwa bado shangweni mwa Paska, tunaendelea kumwomba Kristo Masiha, atujalie amani siku zote, atuimarishie utashi wetu ili tudumu katika heri ya Upasaka. Katika mafundisho yake ya Juma, Baba Mtakatifu Fransisko alitufundisha akituhimiza tusitafute uzima katika mambo mafu; kwa mwangwi wa neno lile ‘kwa nini mnamtafuta aliye hai kati ya wafu’.

Mpendwa Msikilizaji, kipindi chote cha kwaresma, tulikuwa tunajibidisha kurekebisha mwenendo wetu na kukuza zaidi maisha ya fadhila. Ikumbukwe kwamba ‘hatukuwa likizo ya dhambi’ na sasa ndiyo tunafungulia, hapana. Tulikuwa tunajijenga ili tupande kiwango katika maisha yetu ya imani na maadili na katika juhudi yetu ya kumwendea Mungu.

Katika kipindi hiki, tuendelee kuhimizana juu ya kuongeza bidii ya kubaki katika wema wa Pasaka. Mara nyingi huwa tunaitafuta amani kwa juhudi sana, ila kwa bahati mbaya yetu, huwa tunasahau kuitunza. Vipindi vilivyopita tulitafakari kuwa maisha ya dhambi ndiyo kaburi letu. Kwa neema ya Mungu na kwa nguvu ya Yesu Mfufuka anayetushirikisha uzima wake, sisi nasi tumetoka katika kaburi hilo la dhambi na mauti. Sasa tunaalikwa kuongeza jitihada za kubaki katika uzima huu mpya, uzima wa kimungu tunaoupata katika Kristo.

Hutokea mara nyingi sana, wengi wetu tunafanya jitihada za makusudi za kurudi makaburini. Ni kama tulikuwa likizo ya dhambi, sasa likizo imekwisha tunarudi tena madhambini kwetu. Katika kipindi kile tulichambua makaburi yetu kama vile, uzembe katika imani, uvivu, magomvi na mafarakano, nk. Tukasema tumefufuka pamoja na Kristo, hatupo huko tena. Sisi tu hai, hatupatikani tena kati ya wafu. Tuna uzima wa kimunngu, tuna imani na amani katika Yesu, tuna matumaini tele na tumejawa upendo kwa Mungu na jirani. Hayo yote ndiyo hali ya neema.

Huwa inakuwaje basi katika maisha yetu, tukatafuta amani, tunakuwa nayo wiki mmoja au muda mfupi, baadaye fujo zinarudi kwa kasi mpya kana kwamba zilikuwa likizo vile. Hata katika familia zetu, tutatafuta maelewano mema, tutaombana misamaha na kusameheana na hali njema inaonekana kwa muda fulani tu, baadaye tunarudi katika ubaya uleule. Katika juhudi za kujirekebisha, tunatafuta kuwa watu wema, kisha tunakuwa wema kwa muda mfupi halafu baadaye tunarudia ukorofi kwa spidi kali, na kuwa wakorofi zaidi kuliko pale mwanzoni. Kufanya hivyo ndiyo kujirudisha makaburini. Je, inawezekana kujijenga katika wema na kuendelea kuwa mwema zaidi? Hali yoyote njema, hujengwa, hutunzwa na huendelezwa.

Mpendwa msikilizaji, ikumbukwe kwamba, daima tunapigana na nguvu ya uovu iliyomo ndani mwetu. Tunataka tushinde kabisa hila za mwovu ambaye daima anatusukumia makaburini na anapenda kutuvutia makaburini daima. Tukiwa katika hali njema, tukiwa jirani na Mungu, mwovu hapendi. Tufanyeje basi?

Kwanza kabisa tutambue kuwa, zoezi la kiroho la Kwaresma, ni wajibu wa nyakati zote. Tujibidishe daima katika matendo ya upendo, sadaka na majitoleo mbalimbali. Daima tujibidishe kuwa watu wa sala, watu wa kufunga na kutoa sadaka kuwapa maskini. Masikini hawapo kipindi cha Kwaresma tu. Wapo nyakati zote. Baba Mtakatifu katika mafundisho yake, daima ametualika kufumbua maacho kumtazama jirani mhitaji.

Daima tunapiga mbio bila kuchoka, kujitahidi kuvitawala vilema vyetu vya roho na mwili. Vilema vyetu visipotawaliwa, vitatutesa na kutuweka katika hali ya u-kaburi-kaburi daima. Katika moja ya tafakari tulisema, kila mmoja anajua kaburi lake ni nini na liko wapi. Tupo ambao kaburi letu ni kilema cha wivu. Tuna wivu uliopitiliza. Tupo ambapo kaburi letu kubwa ni uwongo, umbea, uzushi na majungu. Haipiti siku bila kusema uwongo. Tupo ambao kaburi letu ni wizi, udokozi na dhuluma. Tupo ambao kaburi letu ni ukorofi, daima tunakuwa wakorofi wa kuzua fujo kati ya watu, kila ulipo lazima watu wakose raha. Tupo ambao kaburi letu ni uvivu, madeni na njaa. Tupo ambao kaburi letu ni kukosa imani kwa Mungu, nk.

Baada ya zoezi lote la Kwaresma, sasa ‘tumefufuka pamoja na Kristo, na tutafute yaliyo juu Kristo aliko...(Kol. 3:1-17). Tupende kujiweka karibu na Mungu kwa njia ya sala, kusoma, kuyajifunza na kuongozwa na maandiko matakatifu. Tujijenge katika dhamiri yenye hofu ya Mungu daima, ili tusitumikishwe na kongwa la yule mwovu. Ni kwa njia hiyo tu, tunaweza kubaki katika furaha na mng’ao wa kipasaka. Na mng’ao wa utukufu wa kipasaka, unatujaza tumaini jema, furaha, amani na baraka tele.

Ni kwa utukufu huo sote tunaomsadiki Kristo tunatumwa sasa kutangaza habari njema ya ufufuko. Na popote tulipo tuwe ishara ya furaha, amani na tumaini jema. Ni kwa utukufu huo sisi nasi tunafanywa kuwa baraka kwa watu wengine, kwani tumefanywa kuwa uzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu na watu wa milki ya Mungu, tuliyoitwa ili tupate kuzitangaza fadhili za Bwana, aliyetutoa gizani (Rej. 1Pet. 2:9). Kutoka Studio za Radio Vatican, ni mimi Padre Pambo Martin Mkorwe OSB.








All the contents on this site are copyrighted ©.