Waamini walei waliojiweka wakfu kwa Kristo na Kanisa lake ni wana mapinduzi!
Baba Mtakatifu Francisko amewapongeza na kuwashukuru waamini walei wanaojisadaka kwa
kujiweka wakfu mbele ya Kristo na Kanisa lake na kwa njia hii wanakuwa ni wana mapinduzi
wa kweli kwa njia ya ushuhuda wa maisha yanayomwilisha upendo wa Mungu kati ya watu.
Baba Mtakatifu ameyasema hayo, Jumamosi tarehe 10 Mei 2014 alipokutana na
kuzungumza na Baraza la Waamini Walei waliojiweka wakfu nchini Italia. Baba Mtakatifu
amesema, ilikuwa ni tarehe 2 Februari 1947 wakati Papa Pio XII alipoandika Waraka
wa kichungaji ujulikanao kama "Provida Mater Ecclesia" ulioliwezesha Kanisa kuanzisha
miundo mbinu ya kitaasisi kwa ajili ya Mashirika ya Waamini walei waliokuwa wanajiweka
wakfu kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake. Hili lilikuwa ni tukio la kishupavu lililofanywa
na Papa Pio XII kwa wakati ule.
Tangu wakati huo, Waamini walei waliojiweka
wakfu kwa Kristo na Kanisa lake wamekuwa ni msaada mkubwa kwa Kanisa, kwani wametumia
muda wao binafsi kwa ajili ya kutafakari, kusali pamoja na kushiriki katika utume
na maisha ya Kanisa wakiendelea kuwa uraiani bila kufungwa na maisha ya kijumuiya
au utume maalum kama ilivyo kwa watawa!
Kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao
anasema Baba Mtakatifu, wanaendelea kushiriki katika mambo ya kisiasa, kiuchumi, elimu
na maisha ya kifamilia na kwa njia hii wanashiriki kikamilifu katika wito wa kuyatakatifuza
malimwengu kwa kuendelea kuwa ni chachu ya imani, matumaini na mapendo kati ya watu.
Katika kiini cha maisha ya mwanadamu: changamoto za jamii mchanganyiko, ndiyo
kauli iliyokuwa inaongoza mkutano mkuu wa Baraza la Waamini Walei waliojiweka wakfu
nchini Italia. Huu ndio utume wa kinabii unaotekelezwa na waamini hawa, kwa kuwaonjesha
watu upendo wa Mungu anayeokoa; anayetibu na kuganga majeraha ya maisha ya mwanadamu
kama ilivyokuwa kwa Msamaria mwema, mwaliko wa kuendelea kujikita katika toba na wongofu
wa ndani pamoja na kuishi na watu wengine.
Baba Mtakatifu katika hotuba aliyowakabidhi
wanachama hawa anawakumbusha kwamba, Italia ni nchi ambayo ina idadi kubwa ya Mashirika
ya Waamini walei waliojiweka wakfu kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake, chachu ya imani,
matumaini na mapendo kwa wale waliokata tamaa. Maisha yao ni ushuhuda wa kinabii kati
ya watu, unaopaswa kujikita katika ari na mwamko mpya wa Kimissionari unaowasukuma
kuwaonjesha wengine imani na furaha ya kukutana na Yesu, bila kuelemewa na ubinafsi.
Baba
Mtakatifu anawahimiza waamini hawa kufanya tathmini ya kina kuhusu utambulisho wao
kama Jumuiya inayowawezesha kukutana na Mwenyezi Mungu, kwa kujikita katika fadhila
ya unyenyekevu na uvumilivu, ili kushuhudia maisha yao kati ya watu wanaoishi nao,
jambo ambalo linaweza kuwa kweli ni zawadi kubwa kwa nchi husika na Kanisa katika
ujumla wake.
Watambue kwamba, wao ni matunda ya kazi ya Roho Mtakatifu kwa
Kanisa, mwaliko wa kuwaendea watu wengi zaidi, kwa kuwa alama ya maskini kwa ajili
ya maskini, lakini wakiwa na moyo unaowaka mapendo, waendelee kufanya hija ya ushuhuda
wa maisha na tunu msingi za Kikristo unaojikita katika furaha.