Mama Kanisa anapoadhimisha Siku ya 51 ya Kuombea Miito Mitakatifu ndani ya Kanisa,
leo Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican inakuletea ushuhuda kutoka kwa Askofu Telesphor
Mkude wa Jimbo Katoliki Morogoro, Askofu Gervas Nyaisonga wa Jimbo Katoliki Mpanda,
Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa pamoja na Padre John Francis Mratibu wa utume na malezi,
Shirika la Wamissionari wa Mtakatifu Claret, Afrika Mashariki.
Askofu Telesphor
Mkude wa Jimbo Katoliki Morogoro katika mahojiano maalum na Radio Vatican anasema
kwamba, Mwenyezi Mungu anaendelea kuwaita watu ili kushiriki katika kazi ya kutangaza
Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia, kwa kuwajalia neema na baraka wanazohitaji
katika utekelezaji wa dhamana hii. Mwenyezi Mungu anamwita kila mtu kwa namna tofauti
kabisa, kwa chambo na nyenzo pengine tofauti na mwenzake. Kuna baadhi ya watu wamevutwa
na mandhari ya Seminari, maisha mazuri ya Kipadre na Kitawa; Ibada na Liturujia ya
Kanisa.
Askofu Mkude anasema, yeye alivutwa zaidi kwenda Seminari Ndogo ya
Bagamoyo kutokana na msisitizo uliotolewa na mwalimu wake walipokuwa shule ya msingi.
Aliambiwa kwamba, Bagamoyo ni mahali pa kuwafunda vijana ili kuwa Mapadre na kwamba,
Seminari ni kitalu cha vijana wenye adabu na heshima, kama ilivyokuwa inajionesha
kijijini kwake. Akapenda hata naye kuhesabika kuwa ni kati ya vijana waliokuwa na
adabu njema, kwa vile wamesoma Seminari Ndogo ya Bagamoyo.
Askofu Mkude anakiri
kwamba, mawazo ya mwanzo hayatoshi kukomaza wito na maisha ya Kipadre, kumbe, daima
kuna haja ya kuwapata watu kama Mzee Eli watakaofafanua wito huu ili kupata sura na
mwelekeo kamili. Hawa ni wazazi, walimu na walezi mbali mbali. Maisha na wito wa Kipadre
daima una changamoto na magumu yake, lakini una raha zake pia. Mtu akipenda kuwa Padre
mwema na mtakatifu anaweza kabisa!
Askofu Gervas Nyaisonga wa Jimbo Katoliki
Mpanda anasema, imani na hatimaye wito wa maisha yake ya Kipadre ni matunda na sadaka
ya Mama yake Mzazi pamoja na Kaka yake aliyemwonesha uzuri wa kutumikia Kanisani.
Akatamani, akapenda na kujitosa kwa kusoma masomo Kanisani pamoja na kutumikia Ibada
ya Misa Takatifu. Huu ukawa ni mwanzo wa wito na maisha yake ya Kipadre. Akabahatika
kuchaguliwa kwenda Seminari ndogo Kahengesa, kati ya vijana 10 waliotoka Parokiani
kwake, wawili tu ndio waliofaulu kwa neema ya Mungu kufikia Daraja takatifu la Upadre.
Askofu Nyaisonga anasema, aliendelea na masomo ya kidato cha V na VI katika
Shule ya Sekonadri ya Sangu, Jimbo Katoliki Mbeya. Mkurugenzi wa miito Jimbo Katoliki
Mbeya alikuwa karibu na kijana wake katika malezi. Baada ya kidato cha VI akishawishiwa
kuendelea na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mujibu wa sheria ili baadaye aendelee na Chuo
Kikuu, lakini Mkurugenzi wa miito alimtaka aende Jeshini ili baadaye aendelee na masomo
ya Seminari. Akamua kwenda Jeshini na hatimaye, Seminari kuu kwa masomo ya Falsafa.
Huko kaendelea na majiundo ya Kipadre, leo hii ni Askofu wa Jimbo Katoliki Mpanda
baada ya kuhamishiwa kutoka Jimbo katoliki Dodoma.
Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa,
Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania ambaye pia ni Askofu wa Jimbo Katoliki
Iringa anasema kwamba, Kristo ndye mchungaji mkuu, kiongozi mwaminifu na mkweli, mtiifu
na mnyenyekevu; mwingi wa upendo na huruma, changamoto kubwa kwa Mapadre kujitahidi
kumuiga Yesu Kristo, Mwalimu na Bwana.
Mapadre wanapaswa kujenga na kudumisha:
uaminifu, unyofu, unyenyekevu, huruma na upendo. Hizi ni tunu ambazo zinaleta mvuto
na mashiko kwa waamini na hivyo kumkimbilia Kristo kwa njia ya Mapadre wake, kutokana
na ushuhuda amini. Mapadre wawe ni vyombo makini vya kuwawezesha watu kumkimbilia
Mungu na Kristo wake. Mapadre watambue kwamba, Kristo ni mfano na kielelezo cha kuigwa,
ili kuendeleza utume na huduma takatifu ulimwenguni.
Padre John Francis Mratibu
wa utume na malezi, Shirika la Wamissionari wa Mtakatifu Claret anasema, Shirika lake
lilianza kuingia Afrika Mashariki kunako mwaka 1993, wanashirika wakiwa wanatokea
Nigeria na hivyo wakatua nanga Jimbo kuu la Mombasa, Kenya na baadaye Wamissionari
wa Claret kutoka India, walifika nchini Tanzania na wengine wakaenda Uganda. Leo hii
wana mapadre 11 wazalendo ambao wako tayari kutangaza Injili ya Furaha sehemu mbali
mbali za dunia kadiri ya mahitaji ya Shirika.
Imeandaliwa na Padre Richard
A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.