Mwilisheni kanuni maadili ili kuyatakatifuza malimwengu!
Baba Mtakatifu Francisko amewashukuru na kuwapongeza wanachama wa Mfuko wa Centesimu
Annus kwa ajili ya Papa kwa kutekeleza wajibu wao kikamilifu katika kupambana na changamoto
katika ulimwengu mamboleo kwa njia ya Mafundisho Jamii ya Kanisa, kwa kukazia dhana
ya mshikamano inayoongozwa na kanuni ya auni iliyofanyiwa kazi kwa namna ya pekee
na Mtakatifu Yohane Paulo II na kuboreshwa zaidi na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto
XVI katika Waraka wake wa kichungaji, Upendo katika Ukweli!
Baba Mtakatifu
anasema katika mikakati ya uchumi mamboleo, dhana ya "mshikamano" ni neno linalosababisha
kichefuchefu kwa watu wengi na kusahau kwamba, mtikisiko wa uchumi kimataifa umesababishwa
kwa kiasi kikubwa na kumong'onyoka kwa tunu msingi za kimaadili, kwa kutokuwa na ugavi
sawa wa rasilimali na bila kutoa kipaumbele cha kwanza katika fursa za ajira. Umefika
wakati kwa wachumi na watunga sera kumwilisha tunu hizi msingi katika mchakato wa:
uzalishaji, kazi, biashara na masuala ya fedha!
Baba Mtakatifu anawapongeza
wanachama wa Centesimus Annus kwa kuweka nadharia katika matendo mintarafu uzoefu
na mang'amuzi yao. Wafanyabiashara wa Kikristo wanapaswa kuongozwa na kanuni msingi
za Injili katika utekelezaji wa majukumu yao, kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa
binadamu, mafao ya wengi, fursa za ajira na kazi nzuri; mambo yanayoweza kutekelezwa
ikiwa kama kanuni msingi za maadili na utu wema zinazingatiwa na kuthaminiwa na wengi!
Baba
Mtakatifu anasema, Jumuiya ya Kikristo, yaani Parokia, Jimbo, Chama cha Kitume ni
mahali muafaka ambako mfanyabiashara, mwanasiasa, mtaalam au mwanaharakati anapaswa
kuchota nguvu ya kuweza kujadiliana na jirani zake, vinginevyo, maeneo ya kazi yanakuwa
ni magumu, kiasi cha kujenga uadui na hatimaye kutokuwa safi kwa ajili ya maisha ya
kibinadamu.
Kwa kweli anasema Baba Mtakatifu, athari za myumbo wa uchumi kimataifa
zinawapatia majaribu makubwa wafanyabiashara, changamoto ya kutowatelekeza wale wote
wanaoteseka kutokana na athari hizi, kwa njia ya mshikamano na ushuhuda wa imani tendaji.
Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican wanawaalika waamini walei kujikita
katika dhamana ya kuyatakatifuza malimwengu kwa kushiriki kikamilifu katika masuala
ya kijamii, kiuchumi na kisiasa. Wanachama wa Centesimu Annus kwa njia ya msaada wa
Mungu na Kanisa wanaweza kutolea ushuhuda kwa kumwilisha kanuni maadili katika ulimwengu
wa wafanyakazi.
Baba Mtakatifu Francisko anasema ushuhuda huu ni muhimu sana
na anapenda kuwatia moyo ili waweze kusonga mbele katika imani, sala, ili kukabiliana
na changamoto za kila siku. Anawaalika waamini walei kumwomba Roho Mtakatifu ili aweze
kuwakirimia kipaji cha ushauri, ili waweze kufikiri na kutenda kwa ajili ya mafao
ya wengi. Mwishoni, Baba Mtakatifu amewaweka wanachama hawa chini ya ulinzi na usimamizi
wa Bikira Maria, Mama wa shauri jema.