2014-05-10 08:52:33

Leo kimbembe mtupu!


Kila mwaka, Dominika ya nne ya Pasaka, inaitwa dominika ya Mchungaji Mwema, tungeweza pia kuiita dominika ya “Mchungaji mzuri” kwa sababu kuna pia wachungaji wabaya wanaoweza kuwafanya kuwa wabaya wale wanaowaongoza. Yesu ni mchungaji mzuri na wale wanaomfuata wanaweza kuwa wazuri na wakupendeza. Kwa wakristu wa zamani hata wa siku hizi Mfano wa Mchungaji Mwema ni mzuri sana kwa watu wote wa zamani bila kujali itikadi zao kadhali ni mfano mzuri kwa viongozi wa dini na serikali wa leo.

Katika Biblia, Mungu anafananishwa na mambo mengi sana, kama vile Mzabibu, Mkulima, Mfalme lakini hasa picha hii ya Mchungaji kwa sababu imechukuliwa kutokana na mazingira ya hali halisi ya wafugaji.

Farao mfalme wa Wamisri naye alikuwa anaitwa pia Mchungaji na watu wake, wakati wafalme wa Israeli hawakuwa wanaitwa hivyo. Kwa sababu yawezekana wafalme hawa hawakujionesha kuwa wachungaji wa watu wao, na badala ya kuliunganisha taifa la Mungu wao walilitawanya, na hivi Mungu anaahidi kumtuma mchungaji mwingine, au Yeye mwenyewe atakuja kuwa mchungaji wao.

Kama tusomavyo katika Zaburi na katika Kitabu cha Nabii isaya: “Bwana aliwaongoza watu wake kama kondoo, akawachunga kama kundi jangwani.” (Zab. 78:52); “Wewe uchungaye Israeli, usikie, wewe umwongozaye Yusufu kama kundi.” (Zab. 80:1); “Bwana ndiye mchungaji wangu sitapungukiwa na kitu.” (Zab. 23:1); “Atalilisha kundi lake kama mchungaji, atawakusanya wanakondoo mikononi mwake; na kuwachukua kifuani mwake, nao wanyonyeshao atawaongoza polepole.” (Isaya 40:11).

Picha ya mchungaji inaeleweka vizuri kabisa kwa mwafrika, kwa sababu tunayo makabila ya wafugaji, aidha kuna karibu kila familia hasa kijijini ina mfugo fulani (lakini siyo mfugo wa wanyama wadogo wadogo kama vile chawa, kunguni na panya wa nyumbani) bali mifugo kama mbuzi, kondoo na ng’ombe. Picha ya kibiblia ya mchungaji ina maana ya kulisha chakula, yaani kuangalia na kutunza. Mchungaji anatakiwa awalishe kondoo wake wote bila ubaguzi.

Mchungaji anategemewa pia kufahamu wapi kuna malisho mazuri na kuna maji ya kunywa. Mchungaji mzuri anaweza kuitambua tabia ya kila kondoo na kujua kondoo wanaoumwa, wanaochechemea, wadhaifu, wakorofi, wenye mbio na walio goigoi nk. Mchungaji anategemewa pia kuelewa ishara za hatari, au za mnyama mkali anayeweza kutokea na awe tayari kupambana na adui ili kuwatetea kondoo wake usiku na mchana.

Katika Injili ya leo, Yesu anatumia lugha ya mafumbo iliyojaa dharau na kwa bahati nzuri anaowafumbia lugha hiyo wanamshtukia na hivi kusababisha mtafaruku mkubwa hadi wanafikia hatua ya kumwambia kuwa ana mapepo na mwenda wazimu, na baadaye wanataka hata kumkamata ili kumtia ndani au labda kumrushia mawe. Hapo yaonekana dhahiri kwamba Yesu aliwapa vidonge vikali vilivyowafanya watafakari na wakakugundua mara moja “Fumbo mfumbie mjinga”. Hebu tuangalie Yesu aliongea nini hadi kuwachokoza: “Amin, amin, nawaambieni, yeye asiyeingia mlangoni katika zizi la kondoo… huyo ni mwivi naye ni m nyang’anyi”. Kwa nini maneno hayo yalete uchokozi?

Ili tuweze kuelewana maana ya fasuli hii vizuri budi kwanza tulione neno hili la kiswahili “zizi” ambalo tafsiri yake hapa imepotoshwa. Yaonekana neno hilo limefasiriwa moja kwa moja kutoka lugha ya kiingereza “Sheephold” au kwa kilatini “ovile” yenye kumaanisha kizizi. Kumbe, neno lililotumika katika lugha asilia ya kigiriki ni “aulen” neno ambalo katika Biblia lingetakiwa litafsiriwe “court” na kwa kiswahili ni ukumbi, ikimaanisha hasa ukumbi ule wa Hekalu la Yerusalemu uliokuwa umezungukwa na ukuta. Ukumbi huo walikuwa wanaingia waamini wa kawaida ili kusali na kutoa sadaka zao. Wahusika waliokuwa wanaianglia na kuitunza sehemu hiyo, walikuwa ni Wakuu wa kiyahudi waliohusika na mambo matakatifu. Ikumbukwe pia kwamba, tuko Yerusalemu, ambako kabla Yesu aliwafukuza wafanyabiashara kutoka humo hekaluni (Yoh 2:14-16).

Yesu anaposema wale wasiongia hapo ukumbini kwa kupitia mlangoni, hao ndiyo wevi na wanyang’anyi alitaka kusema kwamba katika ukumbi huo walikuwa waumini kama kondoo walaojisetiri au kutunzwa, nao wanajisikia kuwa katika mazingira matakatifu, matulivu, ya amani na ya kuwasiliana na Mungu. Hiyo ndiyo maana ya mfugo. Waumini hao wanategemea kulindwa, kutunzwa, kuangaliwa, kutetewa na kulishwa kiroho. Kulishwa kwa maneno mazuri, mifano mizuri. Lakini hatuna budi kuangalia pia hatari inayoweza kuupata mfugo uliofungiwa ndani bila kutolewa nje, mfugo huo unakosa uhuru. Kumbe, yabidi kondoo watoke nje ya kizizi ili wajisikie huru na waende malishoni wasijekufa njaa. Kondoo hao watatoka nje kwa kupitia mlangoni. Ndiyo sasa inaingia picha ya wevi.

Hao si wengine bali hao wahusika wakuu wa pahala hapo patakatifu (wakuu wa hekalu) waliowafungia waumini ndani ya ukumbi wa hekalu. Humo wanawapandikiza watu mafundisho yao. Wanawaeleza juu ya mungu ambaye anaweza kurubuniwa na sadaka zao, na majitoleo yao, na liturjia yao, na wanadaiwa kulipa mapesa kama vile ingekuwa kumnunua Mungu, au kutungiwa sala refu wanazobidi kuzisali la sivyo Mungu huyo atakasirika na kuwaadhibu. Kadhalika yabidi waumini kujitakasa makosa na kujitawadha ili kuogopa adhabu ya Mungu.

Hii ndiyo dini inayoingiza woga kwa watu. Huyo siyo Mungu kwani hakuna furaha katika kumfuata. Aina hii ya kuwaongoza watu Yesu anaiita “Wizi mtupu!” Wevi wa aina hiyo wanaweza kuwa viongozi wa dini, viongozi wa siasa hasahasa wa chama tawala cha wakati wa Yesu, ndiyo waliowanyonya watu, waliowakandamiza na kuwasababishia watu mateso ya kila aina. Aina nyingine ya viongozi wanaitwa wanyang’anyi.

Hawa ndiyo wanamapinduzi, au wakereketwa wa dini au kwa upande wa siasa wangeitwa viongozi wa vyama vya upinzani, au wenye siasa kali, wenye nia njema ya kutaka kuirekebisha jamii ili iwe huru na ya haki zaidi. Viongozi hao walikuwa na itikadi mpya na nzuri, na walifanikiwa kuwarubuni watu. Lakini kasoro yao ni kwamba walitumia mbinu potovu katika kuingiza sera zao. Yaani, walitengeneza chuki, uhasama, walihubiri kulipiza kisasi, walipendekeza hata matumizi ya silaha. Kuteka watu kwa mtindo huo Yesu anauita “Unyang’anyi mtupu!”

Wevi na wanyang’anyi hao wanashikilia ukuu, uongozi, utawala na kupigiwa magoti, lakini wanawadanganya watu. Hawa hawapiti mlangoni. Viongozi hao wanamwiba Mungu watu wake. Wanaiba furaha zao, wanaiba hali ya kujisikia watoto wa Mungu, na hali ya kupendwa na Mungu. Wevi ni wale wanaokufanya uwe mtumwa na usiwe huru, na hii ni picha mbaya ya Mungu. Kondoo wanashindwa kutoka nje kwa sababu wamefungiwa ndani, ni vipofu. Wanamhitaji mchungaji awaangaze, awafungue macho. Kutokana na sauti yake anayowaita wanafunguka masikio, wanamtambua anawaita na kuwaongoza nje. Yesu anataka kuwafungua watu watoke nje ya wigo huo.

Mlango ni ufahamu wetu, ni uelewa wetu. Hiyo ni nguvu aliyotupatia Mungu ya kupambanua mambo, au ya kutambua neno la kweli, Neno la Mungu au sauti ya adui anayetupeleka kwenye kifo. Uwezo aliotupatia Mungu wa kupambanua kati ya mwanga na giza, kati ya kifo na uzima huo ndiyo mlango. Uwezo ule uliokuwa umedumazwa sasa unaweza kusikia sauti ya Kristu anayefungua macho na kukufanya uutambue mlango upo wapi ili uweze kutoka nje.

Mfungua mlango huo si mwingine bali ni dhamiri ya mtu, anayeweza kuelewa sauti ya Mchungaji na kufungua moyo, kwa sababu anatambua anakupeleka kwenye uhuru, kwenye maisha. Kila mmoja wetu anayo dhamiri ambayo ningeweza kusema ni roho mtakatifu anayeweza kukuangaza uweze kupambanua sauti nyingi zinazoahidi mambo mazuri lakini ya uwongo kabisa.

Injili inarudia sana neno hili kusikiliza sauti. Watu wanasikiliza neno la Kristu. Anawaita kondoo wake kwa jina. Mchungaji anamfahamu kila mmoja wetu kwa jina, hatuelewi kama kikundi cha watu. Anawaongoza nje. Anawafungua kondoo wote na kuwaweka huru. Anawatoa watu wake kama vile alivyowatoa toka utumwani Misri. Mambo ya ulimwengu yanatufungia kwenye wigo, tunafungwa.

Lakini Yesu anatufungua. Kama hutoki toka ukumbi huo huwezi kuwa huru wala kuwa na furaha. Maisha yakufungwa kwenye wigo yanakuwa ya woga, yanakuwa ya mtumwa. Wengine wanajaribu wanajaribu kuutoroka ukumbi huo vibaya na wanajikuta wameingia kwenye ukumbi ulio mbaya zaidi. Mmoja unaweza ukajikuta umeingia kwenye ukumbi wa mali, wa maraharaha, wa kazi, wa uongozi, au ukumbi wa vyama vya kisiasa.

Kadhalika unaweza ukatumbukia kwenye wimbi la mambo ya kisasa ambako watu wameridhika na kusema: “wote wanafanya hivi”. Aidha unaweza kuingia kwenye ukumbi wa tabia yako mbovu au vionjo vyako. Hatimaye ukajikuta bila kujitambua kwamba wewe ndiye mwizi na mnyang’anyi mkuu wa wewe mwenyewe.

Yesu anasema: “Mimi ni mlango wa kondoo” maana yake siyo wa ukumbi mpya, bali mlango wa kondoo ambao kondoo wanaweza kupita. Ni mlango wanapoweza kutoka, na ambapo mchungaji mzuri wanaweza kupita vizuri katika mlango ambao ni Kristu. Anayeingia kwa njia ya Yesu ataokoka kutoka utumwani. Yesu Mchungaji mwema anatualika kusikiliza sauti yake. Sauti inayoweza kutusaidia kupambunua sauti mbalimbali hasa ile sauti ya wevi na wanyang’anyi. “Ee Mungu Mwenyezi wa milele, utuelekeze kwenye furaha za mbinguni, kusudi sisi kondoo wako wanyonge tufike huko alikotoka mchungaji wetu shujaa. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristo Bwana wetu. Amina”

Padre Alcuin Nyirenda, OSB.








All the contents on this site are copyrighted ©.