2014-05-09 07:49:22

Vatican yalaani utekaji nyara unaofanywa na Boko Haram nchini Nigeria


Padre Federico Lombardi, msemaji mkuu wa Vatican anabainisha kwamba, vitendo vya Kikundi cha kigaidi cha Boko Haram nchini Nigeria kuendelea kuwateka wasichana ni uvunjifu mkubwa wa haki msingi za binadamu, ambao umekuwa ukifanywa na Kikundi hiki nchini Nigeria.

Udhalilishaji na udhalilishaji wa utu na heshima ya binadamu na mbaya zaidi kati ya watu wasiokuwa na hatia ni jambo ambalo linapaswa kushutumiwa sana na watu wote wenye mapenzi mema. Wasichana hawa wanadhalilishwa kimwili na kiroho, vitendo ambavyo kamwe haviwezi kuvumiliwa.

Padre Lombardi anasema, Vatican inaungana na watu wote wenye mapenzi mema kuomba kuachiliwa mara moja kwa wasichana wa shule waliotekwa nchini Nigeria, ili waweze kuendelea na maisha yao ya kawaida. Vatican inaendelea kusali na kutumainia kwamba, mchango wa watu wenye nia njema utaweza kusaidia kumaliza kabisa vitendo vya kigaidi ambavyo vimeendelea kuwa ni chanzo kikuu cha maafa makubwa kwa watu na mali zao!







All the contents on this site are copyrighted ©.