Ushuhuda wa umoja miongoni mwa Wakristo ni hitaji muhimu!
Umefika wakati kwa Wakristo kuonesha kwa matendo matunda ya majadiliano ya kiekumene
yaliyokwishafikiwa baina ya Makanisa katika kipindi cha miaka hamsini iliyopita, kama
kielelezo cha mwanzo mpya wa maisha na utume wa Kanisa sehemu mbali mbali za dunia.
Ni wakati muafaka wa kujikita zaidi na zaidi katika hija na mshikamano miongoni mwa
Makanisa.
Ni maneno
ya Patriaki Bartolomeo wa kwanza wakati alipokuwa anahojiwa na Gazeti la Croix linalochapishwa
nchini Ufaransa wakati wa hija yake ya kichungaji nchini Ufaransa, mintarafu mkutano
wake na Baba Mtakatifu Francisko wakati wa hija ya Papa kwenye Nchi Takatifu kuanzia
tarehe 24 hadi tarehe 26 Mei 2014 kama kumbukumbu ya Miaka 50 tangu Papa Paulo VI
alipotembelea na hatimaye kukutana na Patriaki Anathegoras mjini Yerusalemu.
Viongozi
wa Makanisa wanataka kujikita katika mchakato wa ujenzi wa umoja kamili miongoni mwa
Wakristo, kwa kuvunjilia mbali kuta za chuki na uhasama ziliojengwa katika historia
ya Kanisa ili kujenga umoja thabiti wa Kanisa kwa kujikita katika majadiliano. Kanisa
la Kiorthodox na Kanisa Katoliki kwa sasa yamekwishafikia ukomavu mkubwa katika mahusiano
yao, kiasi cha kuweza kukutana na kujadiliana katika misingi ya ukweli na uwazi; haya
ni matunda ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican.
Miaka 50 imeyawezesha Makanisa
kufanya hija ya majadiliano ya Kiekumene, sasa yanachangamotishwa kutafuta maneno
yatakaoyawezesha kuandika historia ya Kanisa katika umoja na utofauti wake; kwa kutambua
imani moja katika Kristo na Kanisa lake, ili siku moja, Makanisa haya yaweze kuadhimisha
Fumbo la Ekaristi Takatifu kwa pamoja kama kielelezo cha umoja na utume wa Kanisa.
Hakuna haja kwa wakristo kuendelea kugawanyika, kiasi cha kudhani kwamba, Maadhimisho
ya Fumbo la Ekaristi Takatifu kwa Wakristo wote ni jambo lisilowezekana kutokana na
muda wa majadiliano kuwa mrefu. Umefika wakati wa kujipatanisha kwa kuwa na msimamo
wa pamoja katika masuala ya kitaalimungu.
Ili kutekeleza azma ya umoja wa Kanisa,
Patriaki Bartolomeo wa kwanza hapo tarehe 9 Machi 2014 ameitisha mkutano wa Viongozi
wakuu wa Makanisa ya Kiorthodox kukutana pamoja ili kujadili kuhusu umoja wa Kanisa
unaopaswa kurutubishwa kwa njia ya Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu, kama
kielelezo halisi cha umoja miongoni mwa Wakristo.
Utunzaji bora wa mazingira,
ekolojia, mshikamano na maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii ni kati
ya mambo msingi yanayoweza kuwashikamanisha Wakristo katika mikakati ya Uinjilishaji
Mpya sanjari na ushuhuda wa Kiinjili, ili kwa pamoja waweze kusimama kidete kulinda
na kutetea misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano.
Mazingira ni kazi
ya uumbaji ambayo Mwenyezi Mungu amemdhaminisha mwanadamu kuitunza na kuiendeleza
kwa ajili ya mafao ya wengi, sanjari na kutetea utu na heshima ya binadamu aliyeumbwa
kwa sura na mfano wa Mungu. Lengo ni kusaidia mchakato wa toba na wongofu wa ndani
kwa walimwengu, ushuhuda wa umoja miongoni mwa Wakristo.